Muhubiri 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mashauri juu ya maisha

1Sifa nzuri ni bora kuliko marasi ya bei kali.

Siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa.

2Afazali kwenda kwenye kilio,

kuliko kwenda kwenye karamu,

kwa sababu inawapasa wenye kuwa wazima kukumbuka kwamba kifo kinawangojea sisi wote.

3Huzuni ni afazali kuliko kicheko,

maana, kwa huzuni ya uso moyo unafurahishwa.

4Moyo wa mwenye hekima uko ndani ya nyumba ya kilio,

lakini moyo wa mupumbafu unapenda raha.

5Afazali kusikia maonyo ya wenye hekima

kuliko kusikiliza nyimbo za wapumbafu.

6Maana, kicheko cha mupumbafu

ni kama mulio wa miiba katika moto.

Hayo nayo ni bure.

7Mwenye hekima akimutesa mutu,

yeye anafanya kama mupumbafu.

Kupokea kituliro kunapotosha akili.

8Mwisho wa jambo ni afazali kuliko mwanzo wake.

Moyo muvumilivu ni bora kuliko moyo wa majivuno.

9Usikuwe mwepesi wa hasira,

maana, hasira inakaa ndani ya wapumbafu.

10Usiulize: “Kwa nini nyakati za zamani zilikuwa bora kuliko za sasa?”

Hauulizi hivyo kwa kutumia hekima.

11Hekima ni ya bei kubwa kama urizi;

ni ya mafaa kwa wale wote wanaokuwa wazima.

12Kulindwa na hekima ni kama kulindwa na feza.

Faida ya maarifa ni kwamba hekima inalinda maisha ya mutu anayekuwa nayo.

13Mufikiri vema juu ya kazi ya Mungu.

Ni nani anayeweza kunyoosha kitu Mungu alichokunja?

14Katika siku za kufanikiwa ukuwe na furaha. Katika siku za hasara ufikiri juu ya jambo hili: Mungu amefanya hiyo ya kwanza iambatane na ya pili kusudi mwanadamu asipate kujua mambo yatakayotukia nyuma yake.

15Katika maisha yangu ya bure, niliona kila kitu. Mutu wa haki anakufa ingawa ni wa haki, ambapo mutu mwovu anaendelea kuishi maisha marefu ingawa ni mwovu.

16Basi, usikuwe wa haki kupita kipimo, wala usikuwe mwenye hekima zaidi! Kwa nini kujiangamiza wewe mwenyewe?

17Lakini vilevile, usikuwe mwovu sana wala usikuwe mupumbafu! Kwa nini kufa mbele ya wakati wako?

18Inakupasa ushike neno la kwanza na la pili vilevile; maana anayemutii Mungu atayaepuka yote.

19Hekima inamufanya mwenye hekima kuwa na nguvu zaidi kuliko watawala kumi katika muji.

20Hakika, hakuna mutu wa haki katika dunia anayetenda vizuri siku zote bila kutenda zambi.

21Usifuate maneno yote wanadamu wanayosema, kusudi usisikie mutumishi wako akikutukana.

22Wewe mwenyewe unajua ndani ya moyo kwamba umetukana wengine mara nyingi.

Kuomba hekima

23Nimeyapima yale yote kwa hekima; nikajisemesha: “Ninataka kuwa mwenye hekima!” Lakini hekima iko mbali sana nami.

24Jinsi gani mwanadamu ataweza kutambua maana ya maisha? Jambo hilo ni zito na gumu sana kwetu.

25Hata hivyo, nilikusudia kujua na kuchunguza na kutafuta hekima na maana ya mambo yanayokuwa, na vilevile kujua kwamba uovu ni upumbafu na kwamba upumbafu ni wazimu.

26Jambo moja nililotambua linalokuwa baya zaidi kuliko kifo, ni mwanamuke ambaye moyo wake ni mutego na wavu, na mikono yake ni kama minyororo. Lakini anayemupendeza Mungu anamwepuka mwanamuke yule, lakini mwenye zambi ananaswa naye.

27Ninakuambia mimi Muhubiri, haya ndiyo niliyotambua nilipofanya uchunguzi wangu kidogokidogo.

28Niliendelea kutafuta mambo hayo, lakini sikupata. Kati ya wanaume elfu moja, nilipata kuona mwanaume mumoja anayestahili heshima, lakini kati ya wanawake wote, sikuona hata mumoja anayestahili heshima.

29Nimetambua jambo hili moja: kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wenye usawa, lakini wao wenyewe wamejitafutia matatizo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help