Waamuzi 6 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Nabii wa Yawe

1Waisraeli walitenda uovu mbele ya Yawe; naye akawatia katika mikono ya Wamidiani kwa muda wa miaka saba.

2Wamidiani waliwagandamiza sana Waisraeli, mpaka wakajichimbia mashimo na mapango kwenye milima kuwa makimbilio yao.

3Kila mara Waisraeli walipopanda mbegu katika mashamba, Wamidiani, Waamaleki na watu wengine wa kule upande wa mashariki walikuja kuwashambulia.

4Mataifa hayo yaliweka kambi katika inchi, yakawashambulia na kuharibu mazao yote ya inchi hata kwenye mupaka wa Gaza, hawakuwaachia Waisraeli chochote, ikuwe kondoo, ngombe au punda.

5Waadui waliozoea kuja kwa wingi kama nzige, pamoja na ngombe na ngamia wao na kufanya makao yao katika inchi ya Israeli, waliharibu inchi ya Israeli kwa vile walikuwa wengi sana wasiohesabika.

6Waisraeli wakafanywa kuwa wamasikini sana na Wamidiani hata wakamulilia Yawe awasaidie.

7Waisraeli walipomulilia Yawe awaondolee taabu walizopata kwa Wamidiani,

8Yawe akawapelekea nabii, naye akawaambia: “Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Niliwaondoa katika inchi ya Misri ambako mulikuwa watumwa,

9nikawakomboa toka katika mikono ya Wamisri wote waliowagandamiza. Nikawafukuza watu mbele yenu na kuwapa ninyi inchi yao.

10Kisha nikawakumbusha kwamba mimi ni Yawe, Mungu wenu, na kwamba musiiheshimu miungu ya Waamori, ambao inchi yao mumeitwaa, lakini hamukuisikiliza sauti yangu.’ ”

Mungu anamwamuru Gideoni awaokoe Waisraeli

11Malaika wa Yawe akaenda, akaikaa chini ya muti wa mwalo wa Yoasi Mwabiezeri, kule Ofura. Gideoni mwana wa Yoasi alikuwa anapepeta ngano ndani ya kikamulio cha kukamulia zabibu kusudi Wamidiani wasimwone.

12Malaika wa Yawe akamutokea, akamwambia: “Yawe yuko pamoja nawe, ewe shujaa.”

13Gideoni akamwambia: “Ee Bwana wangu, ikiwa Yawe yuko pamoja nasi, mbona mambo haya yote yametupata? Yako wapi matendo yake ya ajabu ambayo wazee wetu walituelezea, wakisema: ‘Yawe ndiye aliyetutoa katika inchi ya Misri.’ Lakini sasa Yawe ametutupilia na kututia katika mikono ya Wamidiani!”

14Yawe akamugeukia, akamwambia: “Kwenda kwa uwezo unaokuwa nao, uikomboe Israeli kutoka Wamidiani. Ni mimi ninayekutuma.”

15Gideoni akamujibu: “Tafazali Bwana, nitaweza namna gani kuikomboa Israeli? Ukoo wangu ndio wa bure zaidi katika kabila la Manase, na mimi mwenyewe ni mudogo kabisa katika jamaa yetu!”

16Yawe akamwambia: “Nitakuwa pamoja nawe; nawe utawaangamiza Wamidiani sawa vile wangekuwa mutu mumoja.”

17Gideoni akamwambia: “Basi, ikiwa nimepata rehema kwako, unionyeshe kitambulisho kusudi nijue kwamba ni wewe kweli uliyezungumuza nami.

18Ninakuomba usiondoke hapa mpaka nitakaporudi na kukuletea zawadi yangu na kuiweka mbele yako.”

Naye akamujibu: “Nitakaa hapa mpaka utakaporudi.”

19Gideoni akaenda kwake, akatayarisha mwana-mbuzi na mikate isiyotiwa chachu kutoka debe la unga. Akatia nyama ndani ya kikapu na muchuzi ndani ya chungu, kisha akamupelekea chini ya muti wa mwalo, akamupa.

20Malaika wa Mungu akamwambia: “Twaa nyama na mikate isiyotiwa chachu uviweke juu ya jiwe hili. Halafu tia muchuzi juu ya mikate na nyama.” Naye akafanya hivyo.

21Malaika wa Yawe akanyoosha fimbo yake, akagusa nyama na mikate kwa incha ya fimbo. Kwa rafla, moto ukatoka ndani ya jiwe, ukateketeza nyama na mikate. Mara moja malaika wa Yawe akatoweka mbele yake.

22Halafu Gideoni akatambua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yawe; akasema: “Ole wangu, ee Bwana wangu Yawe, maana nimemwona malaika wako uso kwa uso.”

23Lakini Yawe akamwambia: “Amani ikuwe nawe! Usiogope, hautakufa.”

24Gideoni akamujengea Yawe mazabahu kule na kuyaita, “Yawe ni Amani.” Mazabahu hiyo iko kule Ofura, muji wa Waabiezeri, mpaka leo.

Gideoni anaibomoa mazabahu ya mungu Bali

25Usiku ule, Yawe akamwambia Gideoni: “Twaa ngombe dume mumoja wa baba yako, ngombe dume yule wa pili wa umri wa miaka saba. Bomoa mazabahu ya mungu Bali baba yako anayokuwa nayo na kuvunja sanamu ya mungu Ashera inayokuwa karibu nayo.

26Halafu, unijengee mimi Yawe, Mungu wako, mazabahu nzuri juu ya mwinuko ule. Kisha unitolee sadaka ya kuteketezwa ya yule ngombe dume wa pili ukitumia kuni za ile sanamu ya Ashera uliyoivunja.”

27Basi, Gideoni akatwaa watumishi wake kumi, akafanya kama vile alivyoagizwa na Yawe. Lakini kwa sababu aliiogopa jamaa yake na watu wa muji, pahali pa kufanya hayo muchana, akayafanya wakati wa usiku.

28Wakaaji wa muji walipoamuka asubui mapema waliona mazabahu ya Bali na sanamu ya Ashera iliyokuwa karibu nayo vimeharibiwa. Yule ngombe dume wa pili alikuwa ameteketezwa juu ya mazabahu iliyokuwa imejengwa pahali pale.

29Wakaulizana: “Ni nani amefanya jambo hili?” Walipofanya uchunguzi wakagundua kwamba ni Gideoni mwana wa Yoasi ndiye aliyekuwa amefanya hayo.

30Wakaaji wa muji wakamwendea Yoasi, wakamwambia: “Umutoe mwana wako tumwue, maana ameharibu mazabahu ya mungu Bali na kuivunja sanamu ya mungu Ashera iliyokuwa karibu nayo.”

31Yoasi akawaambia wale wote waliomufuata: “Muko munamutetea Bali? Ninyi, mutamwokoa? Yeyote atakayemutetea atauawa mbele ya mapambazuko. Kama Bali ni mungu, basi, ajitetee mwenyewe maana mazabahu yake imebomolewa.”

32Siku hiyo wakamwita Gideoni “Yerubali” maana yake “Bali ajitetee”, maana aliibomoa mazabahu ya mungu Bali.

33Wamidiani, Waamaleki na watu wote wanaokaa pembeni ya muto Yordani wakapiga kambi zao katika bonde la Yezereheli.

34Lakini roho wa Yawe akamujaza Gideoni. Gideoni akapiga baragumu kwa kuwaita Waabiezeri wakuje kumufuata.

35Akatuma wajumbe katika inchi yote ya Manase wakuje kumufuata. Wajumbe wengine akawatuma kuwaita watu wa makabila ya Aseri, Zebuluni na Nafutali, nao wakakuja kujiunga naye.

36Gideoni akamwambia Mungu: “Ikiwa utaikomboa Israeli kwa mukono wangu kama ulivyosema,

37sasa ninaweka ngozi ya kondoo chini kwenye kiwanja cha kupepetea ngano. Ikiwa kutakuwa umande juu ya ngozi tu, na udongo unaouzunguka ikakuwa mukavu, basi, nitajua kwamba utawaokoa Waisraeli kwa mukono wangu kama ulivyosema.”

38Ikakuwa hivyo, kwa maana alipoamuka asubui kesho yake, alikamua umande uliokuwa juu ya ile ngozi, akajaza bakuli.

39Gideoni akamwambia Mungu: “Tafazali, usinikasirikie. Ninakuomba niseme mara moja tena. Ninakuomba uniruhusu nitumie ngozi hii kwa kufanya jaribio lingine. Ninakuomba juu ya ngozi kukuwe kukavu, lakini kwenye udongo kukuwe umande.”

40Mungu akafanya hivyo usiku ule, maana juu ya ngozi kulikuwa kukavu na kwenye udongo kulikuwa umande.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help