Kutoka 9 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Pigo la tano: Vifo vya nyama wa kufugwa

1Kisha Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa mufalme wa Misri umwambie kwamba mimi Yawe, Mungu wa Waebrania, ninasema hivi: ‘Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie.

2Kama ukikataa kuwaacha waondoke na ukiendelea kuwashikilia,

3nitanyoosha mukono wangu na kuleta ugonjwa mukali sana juu ya nyama wenu wote: ngombe, farasi, punda, ngamia, mbuzi na kondoo.

4Na nitaitenganisha mifugo ya Waisraeli na mifugo ya Wamisri kusudi nyama hata mumoja wa Waisraeli asikufe.’ ”

5Tena, Yawe akaweka wakati akisema: “Kesho mimi Yawe nitatimiza jambo hilo katika inchi ya Misri.”

6Kesho yake Yawe akafanya kile alichosema. Mifugo yote ya Wamisri ikakufa, lakini hakuna nyama hata mumoja wa Waisraeli aliyekufa.

7Mufalme wa Misri akauliza habari juu ya nyama wa Waisraeli. Wakamwambia kwamba hakuna nyama wao hata mumoja aliyekufa. Hata hivyo, Mufalme akabaki akifanya moyo wake kuwa mugumu, wala hakuwaruhusu Waisraeli waondoke.

Pigo la sita: Majipu

8Yawe akamwambia Musa na Haruni: “Mutwae kila mumoja wenu vitanga vya majivu ya furu, kisha Musa ayarushe juu katika hewa mbele ya mufalme wa Misri.

9Majivu hayo yatakuwa vumbi nyembamba itakayoenea juu ya inchi yote ya Misri. Yatasababisha majipu yatakayopasuka na kuwa vidonda kwa watu na nyama kila pahali katika inchi ya Misri.”

10Basi, wakatwaa majivu kutoka kwenye furu, wakamwendea mufalme wa Misri, naye Musa akayarusha juu katika hewa. Watu na nyama wakapatwa na majipu. Ang. Ufu 16.2

11Hata wale wachawi hawakuweza kujitokeza, maana wao pamoja na Wamisri wote vilevile walipatwa na majipu hayo.

12Lakini Yawe akafanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, naye hakuwasikiliza kama vile Yawe alivyomwambia Musa.

Pigo la saba: Mvua ya mawe

13Kisha, Yawe akamwambia Musa: “Kesho, amuka asubui mapema umwendee mufalme wa Misri, umwambie kwamba mimi Yawe, Mungu wa Waebrania, ninasema hivi: ‘Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie.

14Maana mara hii, wewe mwenyewe, wakubwa wako na watu wako mutapatwa na mapigo yangu makali. Nawe utatambua kwamba hakuna yeyote katika dunia anayekuwa kama mimi.

15Ningalikwisha kukuangamiza wewe na watu wako kwa ugonjwa mukali, nanyi mungalikuwa mumekwisha kuangamia.

16Lakini nimewaacha muishi kwa kuonyesha uwezo wangu. Kwa hiyo dunia yote itatambua kwamba mimi ni nani. Ang. Rom 9.17

17Lakini ungali unaonyesha kiburi juu ya watu wangu, wala hauwaachi waondoke.

18Kwa hiyo kesho, wakati kama huu, nitaleta mvua kubwa ya mawe ambayo haijatokea katika inchi ya Misri, tangu mwanzo wake mpaka leo.

19Kwa hiyo agiza kwamba mifugo yako na chochote kinachokuwa kule katika mashamba viwekwe pahali salama. Mvua ya mawe itamunyeshea kila mutu na nyama anayekuwa katika shamba na ambaye hayuko ndani ya nyumba. Wote watakufa.’ ”

20Wakubwa wamoja wa mufalme wa Misri wakaogopa maneno hayo ya Yawe, wakawapeleka watumwa na nyama wao ndani ya nyumba pahali pa usalama.

21Lakini yule ambaye hakujali neno la Yawe aliwaacha watumwa wake na nyama wake katika mashamba.

22Kisha, Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako juu mbinguni, kusudi mvua ya mawe inyeshe kila pahali katika inchi ya Misri. Imunyeshee mutu, nyama na kila mumea katika shamba.”

23Basi, Musa akainua fimbo yake kuelekea mbinguni. Naye Yawe akaleta mvua ya mawe na ngurumo, umeme ukapiga inchi. Yawe alinyesha mvua ya mawe juu ya inchi ya Misri,

24mvua kubwa ya mawe iliyofuatana na mufululizo wa umeme, ambayo hakuna mwanainchi yeyote wa Misri aliyepata hata kidogo kushuhudia mbele. Ang. Ufu 8.7; 16.21

25Mvua hiyo ya mawe ilivunjavunja kila kitu katika mashamba na kila pahali katika inchi ya Misri, nyama na watu. Mawe ya mvua yakavunjavunja mimea yote na miti katika mashamba.

26Mvua ya mawe haikunyesha tu katika inchi ya Goseni ambako Waisraeli walikuwa wanakaa.

27Basi, mufalme wa Misri akaagiza Musa na Haruni waitwe, akawaambia: “Mara hii nimetenda zambi. Yawe ana haki na mimi na watu wangu tumekosa.

28Mumwombe Yawe maana ngurumo hii na mvua ya mawe vimezidi. Mimi nitawaacha muondoke na wala hamutabakia tena.”

29Musa akamwambia: “Mara tu nitakapotoka inje ya muji nitainua mikono na kumwomba Yawe. Ngurumo itakoma na hakutakuwa mvua ya mawe tena kusudi utambue kwamba dunia ni ya Yawe.

30Lakini ninajua kwamba wewe na wakubwa wako mungali hamumwogopi Yawe Mungu.”

31(Kitani na mimea ya shayiri vyote vilikuwa vimeharibiwa, kwa sababu shayiri ilikuwa na masuke na kitani ilikuwa imechanua maua.

32Lakini ngano na jamii nyingine ya ngano havikuharibiwa kwa sababu hiyo inachelewa kukomaa).

33Basi, Musa akaondoka katika nyumba ya mufalme, akatoka inje ya muji. Kisha akainua mikono yake kumwomba Yawe. Ngurumo na mvua ya mawe vikakoma, mvua ikaacha kunyesha katika dunia.

34Lakini mufalme wa Misri alipoona kwamba mvua ya mawe na ngurumo vimekoma, akarudilia zambi yake tena. Akafanya moyo wake kuwa mugumu, yeye pamoja na wakubwa wake.

35Basi, kama vile Yawe alivyomwambia Musa, moyo wa mufalme wa Misri ulikuwa mugumu, yeye na wakubwa wake, akakataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help