1Ninachukia maisha yangu!
Malalamiko yangu nitayasema bila kizuizi.
Nitasema kwa uchungu wa moyo wangu.
2Nitamwambia Mungu:
Usinitendee sawa na mwenye makosa.
Unijulishe sababu ya kugombana nami.
3Ni sawa kwako kunionea,
kuzarau kazi ya mikono yako
na kupendelea mipango ya waovu?
4Uko na macho kama ya mwanadamu?
Unaona kama vile mwanadamu anavyoona?
5Siku zako ni kama za mwanadamu?
Miaka yako kama ya mwanadamu?
6Kwa nini unachunguza uovu wangu
na kuitafuta zambi yangu?
7Wewe unajua kwamba mimi sina kosa,
na hakuna wa kuniokoa toka katika mikono yako.
8Mikono yako ilinitengeneza na kuniumba,
lakini sasa unageuka kwa kuniangamiza.
9Kumbuka kwamba uliniumba kwa udongo.
Utanirudisha tena katika mavumbi?
10Si wewe uliyenimimia kama maziwa,
na kunigandisha kama siagi?
11Uliuumba mwili wangu kwa mifupa na mishipa,
ukaifunika mifupa yangu kwa nyama na ngozi.
12Ukanipa uzima na kunitendea mema,
ukalinda nafsi yangu kwa uangalifu.
13Hata hivyo mambo haya uliyaficha ndani ya moyo.
Lakini ninajua kwamba ile ilikuwa nia yako.
14Ulikuwa unangojea uone kama nitatenda zambi,
kusudi ukatae kunisamehe uovu wangu.
15Kama mimi ni mwovu, ole wangu!
Kama mimi ni mwenye haki, siwezi kujisifu;
maana nimejaa haya, nikiangalia mateso yangu.
16Nikiinua kichwa tu, unaniwinda kama simba
na kuniponda tena kwa maajabu yako.
17Kila mara uko na ushuhuda juu yangu,
unaongeza hasira yako juu yangu,
unaniletea waadui wapya wanishambulie.
18Ee Mungu, kwa nini ulinitoa katika tumbo ya mama?
Afazali ningekufa mbele ya watu kuniona,
19ningepelekwa katika kaburi,
na kuwa kama mutu asiyekuwa.
20Siku za maisha yangu si chache?
Uniachilie nipate kufurahi kidogo,
21mbele ya kwenda kule ambako sitarudi,
kule kwenye inchi ya huzuni na giza kubwa;
22inchi ya huzuni na fujo,
ambako mwangaza wake ni kama giza.
Masemi ya ZofariWho We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.