Hesabu 19 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Majivu ya ngombe mwekundu

1Yawe akawaambia Musa na Haruni:

2Haya ni masharti ya sheria ambayo mimi Yawe ninatoa. Uwaambie Waisraeli wawaletee ngombe dike mwekundu mukamilifu asiyekuwa na kilema chochote, na ambaye hajapata kufungwa nira.

3Ninyi mutamupa kuhani Eleazari ngombe huyo. Atatolewa inje ya kambi na kuchinjwa mbele ya kuhani huyo.

4Kisha kuhani Eleazari atatwaa sehemu ya damu na kuinyunyiza kwa kidole mara saba, kuelekea upande wa mbele wa hema la mukutano.

5Ngombe huyo muzima atateketezwa kwa moto mbele ya kuhani. Kila kitu chake kitateketezwa; ngozi, nyama, damu na mavi yake.

6Halafu kuhani atatwaa muti wa mwerezi, hisopo na sufu nyekundu na kuvitia katika moto huo.

7Nyuma ya hayo, kuhani atafua nguo zake na kuoga mwili kwa maji, halafu anaweza kuingia katika kambi; atakuwa muchafu mpaka magaribi.

8Mutu atakayemuteketeza ngombe huyo vilevile atafua nguo zake na kuoga mwili, lakini naye vilevile atakuwa muchafu mpaka magaribi.

9Mutu anayekuwa safi atazoa majivu ya ngombe huyo na kuyapeleka pahali safi inje ya kambi. Yatalindwa na kutumiwa na jamii nzima ya Israeli kwa kutengeneza maji ya utakaso kwa kuondoa zambi. Ang. Ebr 9.13

10Mutu atakayezoa majivu ya ngombe huyo anapaswa kufua nguo zake, lakini atakuwa muchafu mpaka magaribi. Sharti hili ni la kufuata siku zote kwa Waisraeli na watu wengine watakaoishi pamoja nao.

Sheria juu ya kutakaswa

11Mutu akigusa maiti ya mutu yeyote, atakuwa muchafu kwa siku saba.

12Siku ya tatu na ya saba mutu huyo atajitakasa kwa yale maji ya utakaso, naye atakuwa safi. Lakini akiacha kujitakasa katika siku ya tatu na ya saba, mutu huyo atabaki muchafu.

13Anayegusa maiti, ni kusema mwili wa mutu aliyekufa, asipojitakasa, anachafua hema la Yawe, naye atatengwa na watu wa Israeli. Mutu huyo atabaki muchafu kwa sababu hakunyunyiziwa yale maji ya utakaso.

14Na hii ndiyo sheria ya kufuatwa kama mutu akikufia ndani ya hema: Kila mutu atakayeingia ndani ya hema hilo, au aliyekuwa ndani ya hema hilo, atakuwa muchafu kwa siku saba.

15Kila chombo kinachokuwa wazi ambacho hakina kifuniko juu yake kitakuwa kichafu.

16Mutu yeyote akigusa mwili wa mutu aliyeuawa au aliyekufa kifo cha kawaida inje ya nyumba, au akigusa mufupa wa mutu au kaburi, atakuwa muchafu kwa siku saba.

17Kwa ajili ya wale waliojichafua, watatwaa majivu ya sadaka ya zambi iliyoteketezwa, majivu hayo yatachanganywa na maji ya muto.

18Mutu anayekuwa safi atatwaa hisopo, halafu ataichovya katika maji hayo, kisha atainyunyizia hema, vyombo vyote vinavyokuwa ndani ya hema na watu wanaokuwa ndani. Atamunyunyizia vilevile mutu aliyegusa mufupa wa mutu, au mwili wa mutu aliyeuawa au aliyekufa kifo cha kawaida, au aliyegusa kaburi.

19Katika siku ya tatu na ya saba, mutu anayekuwa safi atamunyunyizia mutu anayekuwa muchafu maji hayo; hivyo katika siku ya saba, atamutakasa mutu huyo anayekuwa muchafu, naye atafua nguo zake na kuoga, na magaribi atakuwa safi.

20Lakini mutu muchafu asipojitakasa, mutu huyo atatengwa mbali na jamii, kwa sababu anachafua hema la Yawe. Kwa vile hakunyunyiziwa maji ya utakaso, yuko muchafu.

21Hili ni sharti la kufuata siku zote. Mutu atakayenyunyiza maji ya utakaso atafua nguo zake; naye atakayegusa maji hayo atakuwa muchafu mpaka magaribi.

22Chochote mutu muchafu atakachogusa kitakuwa kichafu, na yeyote atakayekigusa kitu hicho atakuwa muchafu mpaka magaribi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help