1Saulo alikuwa na umri wa miaka alipoanza kuwa mufalme. Na alitawala Waisraeli kwa muda wa miaka miwili.]
2Saulo aliwachagua Waisraeli elfu tatu. Kati yao, elfu mbili alikuwa nao kule Mikimasi na katika inchi ya milima ya Beteli. Elfu moja aliwaweka kule Gibea katika eneo la Benjamina. Hao aliwaweka chini ya uongozi wa mwana wake Yonatani. Watu wengine wote waliobakia, aliwarudisha, kila mutu kwake.
3Yonatani alishinda kambi ya waaskari ya Wafilistini kule Geba, na Wafilistini wote walisikia juu ya habari hiyo. Hivyo Saulo alipiga baragumu katika inchi yote, akatangaza, akisema: “Waebrania wasikie.”
4Waisraeli wote walisikia kwamba Saulo alikuwa ameishinda kambi ya waaskari walinzi wa Wafilistini, na kwamba Wafilistini wanawachukia sana Waisraeli. Waliitwa kwenda kuungana na Saulo kule Gilgali.
5Wafilistini walikuwa na magari elfu makumi tatu, waaskari elfu sita wapanda-farasi na kikundi cha waaskari wa miguu wengi kama muchanga wa bahari. Wote walipanda juu na kupiga kambi yao kule Mikimasi, upande wa mashariki wa Beti-Aweni.
6Waisraeli walipoona wako katika taabu (maana walikuwa wanashambuliwa vikali), walianza kujificha. Wengine walijificha katika mapango, wengine ndani ya mashimo, wengine kwenye mawe makubwa, wengine kwenye makaburi na wengine kwenye visima.
7Wengine walivuka muto Yordani mpaka katika inchi ya Gadi na inchi ya Gileadi. Lakini Saulo alikuwa angali kule Gilgali pamoja na watu wote waliomufuata wakitetemeka.
8Saulo alimungojea Samweli kwa muda wa siku saba, kama vile Samweli alivyosema. Lakini Samweli hakukuja kule Gilgali na watu walianza kumwacha Saulo.
9Basi, Saulo akawaambia watu: “Muniletee sadaka yenu ya kuteketezwa na zile za amani.” Naye akatolea sadaka ya kuteketezwa.
10Mara tu alipokuwa anamaliza kutoa sadaka ya kuteketezwa, Samweli akafika. Saulo akatoka inje kwenda kumupokea Samweli na kumusalimia.
11Samweli akamwuliza: “Umefanya nini?”
Saulo akamujibu: “Nilipoona watu wananiacha, na wewe haukukuja katika muda wa siku ulizosema, na tena nilipoona Wafilistini wamejipanga tayari kwa vita kule Mikimasi,
12nikawaza kama Wafilistini watakuja kunishambulia kule Gilgali. Tena nilikuwa bado sijaomba rehema ya Yawe. Halafu nikalazimishwa kutolea mimi mwenyewe sadaka ya kuteketezwa.”
13Samweli akamujibu Saulo: “Umefanya kipumbafu. Haukutii mambo Yawe, Mungu wako, aliyokuamuru. Kama ungetii, Yawe angeudumisha milele ufalme wako juu ya Israeli.
14Lakini sasa ufalme wako hautadumu kwa sababu amri Yawe aliyokuamuru haukuitii. Yawe amejitafutia mutu mwingine ambaye atamutii kwa moyo wote, na huyo ndiye ambaye atamuchagua kuwa mutawala juu ya watu wake.”
15Samweli akaondoka kutoka Gilgali na kwenda kule Gibea katika inchi ya Benjamina.
Saulo alipowahesabu watu waliokuwa pamoja naye, akaona wako watu mia sita tu.
16Saulo na mwana wake Yonatani pamoja na watu waliokuwa pamoja nao, walikaa kule Gibea katika inchi ya Benjamina na Wafilistini walipiga kambi kule Mikimasi.
17Wafilistini walitoka kwenye kambi yao kwenda kuwashambulia wakiwa katika vikundi vitatu. Kikundi kimoja kilielekea Ofura katika inchi ya Suali.
18Kikundi kingine kilielekea Beti-Horoni, na kikundi kingine kikageukia njia inayoelekea bonde la Zeboimu, kuelekea katika jangwa.
19Wakati huo hakukuwa mufuaji yeyote wa vyuma katika inchi nzima ya Israeli, maana Wafilistini walikusudia kuwazuia Waebrania wasipate kujitengenezea mapanga au mikuki.
20Kila Mwisraeli alilazimishwa kuwaendea Wafilistini kunoa majembe yake au sururu au shoka au kisu cha kuvuna.
21Waisraeli walikuwa wanalipa feza sehemu mbili ya tatu za shekeli kwa kunoa majembe na sururu. Na bei ya kunoa shoka au kuchongoa chuma ilikuwa sehemu moja ya tatu ya shekeli.
22Kwa hiyo, siku ya vita hakuna mutu kati ya wote waliokuwa pamoja na Saulo na Yonatani aliyekuwa na upanga au mukuki isipokuwa Saulo na mwana wake Yonatani.
23Wafilistini walipeleka kikundi cha waaskari kwenda kulinda njia ya Mikimasi.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.