Isaya 24 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yawe ataiazibu dunia

1Sasa Yawe anaiharibu dunia

na kuifanya tupu.

Atavuruga uso wa dunia

na kuwatawanya wakaaji wake.

2Kila mutu atapatwa na mambo yaleyale:

mutu wa kawaida na kuhani;

mutumwa na bwana wake;

mujakazi na bibi wake;

mwenye kununua na mwenye kuuzisha;

mukopeshaji na mukopaji;

mwenye kudai na mwenye kudaiwa.

3Dunia itaharibiwa kabisa na kuangamizwa.

Ni Yawe amesema hayo.

4Dunia inakauka na kunyauka;

ulimwengu unafazaika na kunyauka;

mbingu zinafazaika pamoja na dunia.

5Watu wameichafua dunia

maana wamezivunja sheria za Mungu,

wamegeuka mbali na masharti yake,

wamelivunja agano lake la milele.

6Kwa sababu hiyo laana inaiteketeza dunia,

wakaaji wake wanateseka kwa ajili ya makosa yao.

Wakaaji wa dunia wamepunguka,

ni watu wachache tu waliobaki.

7Mizabibu inanyauka,

divai inakosekana.

Wote waliokuwa wenye furaha

sasa wanaugua kwa huzuni.

8Mudundo wa ngoma umekoma,

makelele na fujo vimetoweka;

midundo ya vinubi imekomeshwa.

9Hakuna tena kunywa divai na kuimba;

kinywaji cha kulewesha kimekuwa uchungu kwa wakunywaji.

10Muji wa fujo umejaa uharibifu;

kila nyumba imefungwa kusudi mutu asiingie.

11Kuna kilio katika barabara kwa kukosa divai;

shangwe yote imekoma,

furaha imetoweka katika dunia.

12Muji ni mabomoko matupu;

milango yake imevunjwavunjwa.

13Kama vile zeituni chache tu juu ya mizeituni

au tini chache tu juu ya muti wa tini,

kisha kumaliza mavuno,

ndivyo inavyokuwa katika inchi zote.

14Watu wanalalamika,

wanaimba kwa shangwe.

Kutoka upande wa magaribi, wanatangaza ukubwa wa Yawe,

15na wale wa upande wa mashariki wanamusifu.

Watu wa mbali wanalisifu

jina la Yawe, Mungu wa Israeli.

16Tunasikia nyimbo za sifa kutoka miisho ya dunia,

nyimbo za kumusifu Mungu anayekuwa mwenye haki.

Lakini mimi ninasema: Ninakonda,

kweli ninakonda.

Ole kwangu mimi!

Wadanganyifu wanaendelea kuwa wadanganyifu,

udanganyifu wao unazidi kuwa mubaya zaidi.

17Woga, mashimo na mitego,

hivi ndivyo vinavyowangojea, enyi wakaaji wa dunia.

18Mutu atakayekimbia sauti ya woga atatumbukia ndani ya shimo;

na mutu atakayetoka ndani ya shimo atanaswa katika mutego.

Madirisha ya mbinguni yamefunguliwa,

misingi ya dunia inatikisika.

19Dunia inavunjikavunjika,

inapasuka na kutikiswatikiswa.

20Inapepesuka kama mulevi,

inayumbayumba kama kibanda.

Imelemewa na muzigo wa zambi zake

nayo itaanguka wala haitasimama tena.

21Siku ile Yawe ataliazibu jeshi la anga

vilevile na wafalme wa dunia.

22Wote watakusanywa kama wafungwa katika shimo;

watafungwa katika kifungo pamoja kwa miaka mingi,

na kisha muda huo atawaazibu.

23Kisha mwezi utafezeheka,

nalo jua litapata haya ya kuangaza,

maana Yawe wa majeshi

atatawala kule Yerusalema katika mulima Sayuni;

ataonyesha wazee wa watu wake utukufu wake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help