1Katika mwaka wa pili wa utawala wa mufalme Dario wa Persia, siku ya kwanza ya mwezi wa sita, kwa njia ya nabii Hagai, neno la Yawe liliwafikia Zerubabeli mwana wa Saltieli pamoja na Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki kusema hivi:
2Yawe wa majeshi anasema hivi: Watu hawa wanasema kwamba wakati wa kuijenga upya nyumba ya Yawe haujafika.
3Neno la Yawe lilifika kwa njia ya nabii Hagai kusema hivi:
4Ni sawa kwenu kukaa katika nyumba zenu nzuri wakati nyumba yangu ni mabomoko matupu?
5Basi, Yawe wa majeshi anasema hivi: Mufikiri vizuri juu ya namna munavyofanya!
6Munapanda mbegu kwa wingi, lakini munavuna kidogo.
Munakula, lakini hamushibi.
Munakunywa divai, lakini hamutosheki.
Munavaa nguo, lakini bado munasikia baridi.
Mushahara wa mutumishi unakuwa kama umetumbukizwa katika mufuko uliotoboka.
7Yawe wa majeshi anasema hivi: Mufikiri vizuri juu ya namna munavyofanya!
8Sasa basi muende kwenye milima mulete miti, muijenge upya nyumba yangu, nipate kuifurahia na kutukuzwa. –Ni Yawe anayesema hivyo.
9Mulitazamia mavuno mengi, lakini mulipata kidogo tu. Mulipoyaleta kwenye nyumba, niliyapeperusha mbali. Kwa nini? Kwa sababu nyumba yangu ni mabomoko matupu wakati kila mumoja wenu anashugulikia nyumba yake.
10Ndiyo maana mbingu zimeacha kunyesha mvua, nao udongo hauoteshi mavuno.
11Nimeleta ukavu katika inchi, juu ya vilima na mashamba ya ngano, mashamba ya mizabibu na mashamba ya mizeituni na kila mumea, watu na nyama, na chochote mulichokitoshea jasho. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.
12Halafu Zerubabeli mwana wa Saltieli, na Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki, pamoja na watu wote waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho wakafanya kama vile Yawe, Mungu wao alivyowaambia na kama vile walivyoambiwa na Hagai, yule nabii aliyetumwa na Yawe, Mungu wao. Watu wakamuheshimia Yawe.
13Kisha Hagai, mujumbe wa Yawe, akawapa watu ujumbe huu kutoka kwa Yawe: Mimi niko pamoja nanyi.
–Ni ujumbe wa Yawe.
14Basi, Yawe akamutia moyo mutawala Zerubabeli wa Yuda pamoja na Kuhani Mukubwa Yoshua na watu wote waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho. Wakaanza kazi hiyo ya kuijenga upya nyumba ya Yawe wa majeshi, Mungu wao,
15katika siku makumi mbili na ine ya mwezi wa sita, mwaka wa pili wa utawala wa mufalme Dario.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.