Yeremia 27 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yeremia anavaa nira

1Katika mwanzo wa utawala wa mufalme Zedekia mwana wa Yosia juu ya inchi ya Yuda, Yawe alimutolea Yeremia ujumbe, akisema:

2Yawe aliniambia hivi: Yeremia, ujitengenezee kamba na nira na kuvifungia kwenye shingo.

3Kisha, upeleke ujumbe kwa mufalme wa Edomu, mufalme wa Moabu, mufalme wa Amoni, mufalme wa Tiro na mufalme wa Sidona. Uutume kwa mukono wa wajumbe waliokuja Yerusalema kwa kumwona Zedekia mufalme wa Yuda.

4Uwaamuru wajumbe hao wawaambie wakubwa wao kwamba:

Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi:

5Ni mimi niliyeumba dunia, watu na nyama wanaokuwa ndani yake kwa uwezo wangu na kwa nguvu zangu kubwa. Nami ninaitoa kwa yeyote ninayetaka.

6Sasa nimetoa inchi zote kwa mutumishi wangu Nebukadneza mufalme wa Babeli. Vilevile nimemupa nyama wa pori wamutumikie.

7Mataifa yote yatamutumikia yeye, pamoja na mwana wake na mujukuu wake mpaka wakati inchi yake itakapoanguka. Kisha mataifa mengi na wafalme wengi wakubwa watamufanya kuwa mutumwa wao.

8Lakini kama taifa lolote au utawala wowote hautajiweka chini ya mamlaka ya Nebukadneza mufalme wa Babeli, na kukataa kubeba katika shingo yao zile nira atakazowalazimisha kubeba, basi nitaliazibu taifa hilo kwa vita, njaa na magonjwa makali mpaka nitakapoliangamiza kabisa kwa njia yake.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

9Basi, ninyi musiwasikilize manabii wenu, wapiga ramuli wenu, wafasiriaji wenu wa ndoto, waaguzi wenu au wachawi wenu, wanaowaambia kwamba musimutii mufalme wa Babeli.

10Hao wanawatabiria uongo. Jambo hilo litawasababisha ninyi kuhamishwa mbali na inchi yenu. Nitawafukuza mbali, nanyi mutaangamia.

11Lakini watu wa taifa lolote litakalobeba kwenye shingo nira mufalme wa Babeli atakayolazimisha kubeba na kumutumikia, nitawaacha wakae katika inchi yao, walime udongo na kuishi humo.

–Ni ujumbe wa Yawe.

12Yeremia akamwambia Zedekia mufalme wa Yuda, mambo hayohayo, akisema: Mukubali kubeba nira mufalme wa Babeli atakayowalazimisha kubeba. Mumutumikie yeye na watu wake, kusudi mupate kuishi.

13Kwa nini wewe na watu wako munataka kufa kwa vita, njaa na magonjwa makali? Maana, hivi ndivyo Yawe alivyosema juu ya yale yatakayolipata taifa lolote litakalokataa kumutumikia mufalme wa Babeli.

14Usisikilize maneno ya manabii wanaokuambia kwamba hautamutumikia mufalme wa Babeli, kwa sababu wanakutabiria uongo.

15Mimi sikuwatuma manabii hao. Lakini wanatabiri uongo kwa jina langu. Kwa hiyo nitawafukuza, nanyi mutaangamia, pamoja na hao manabii wanaowatabiria uongo.

–Ni ujumbe wa Yawe.

16Kisha, Yeremia akawaambia makuhani na watu wote:

Yawe anasema hivi: Musiwasikilize manabii wenu wanaowatabiria, wakisema: “Vyombo vya nyumba ya Yawe vinakaribia kurudishwa kutoka Babeli,” kwa maana wanawadanganya ninyi.

17Musiwasikilize. Mumutumikie mufalme wa Babeli, kusudi mupate kuishi. Kwa nini muji huu ufanywe kuwa mabomoko?

18Ikiwa wao ni manabii, na ikiwa wana ujumbe kutoka kwa Yawe, basi wamusihi Yawe wa majeshi, kusudi vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Yawe na katika nyumba ya mufalme wa Yuda, na katika Yerusalema, visitwaliwe na kupelekwa Babeli.

19Kwa maana Yawe wa majeshi anasema hivi juu ya nguzo, birika la shaba na misingi ya kuliwekea, vinara na vyombo vingine vilivyoachwa katika muji huu,

20ambavyo Nebukadneza, mufalme wa Babeli, hakuvichukua wakati alipowapeleka Yekonia mwana wa Yoyakimu, mufalme wa Yuda na waheshimiwa wote wa Yuda na Yerusalema kwenda katika uhamisho.

21Kweli, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi juu ya vile vyombo vilivyoachwa katika nyumba ya Yawe, katika nyumba ya mufalme wa Yuda na katika Yerusalema:

22Vyombo hivyo vitapelekwa Babeli, navyo vitabaki huko mpaka siku nitakapovishugulikia. Hapo ndipo nitakapovirudisha na kuviweka tena pahali hapa.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help