1Kisha Kora mwana wa Isihari mwana wa Kohati mwana wa Lawi, akatwaa watu pamoja na watu watatu wa ukoo wa Rubeni: Datani na Abiramu, wana wa Eliabu, na Oni mwana wa Peleti. Ang. Yuda 11
2Hao wote waliungwa mukono na viongozi wenye heshima mia mbili makumi tano waliochaguliwa na Waisraeli, wakamwasi Musa.
3Wakakusanyika mbele ya Musa na Haruni, wakawaambia: Ninyi mumepitisha kipimo! Waisraeli wote pamoja ni watakatifu; kila mumoja ni mutakatifu. Yawe yuko pamoja nasi wote. Mbona sasa ninyi munajifanya wakubwa kushinda watu wengine wa Yawe?
4Musa aliposikia hayo, akajitupa uso mpaka chini.
5Kisha akamwambia Kora na wafuasi wake: Kesho asubui, Yawe ataonyesha ni nani anayekuwa wake na ni nani anayekuwa mutakatifu, na yule atakayemuchagua, atamuwezesha kukaribia kwenye mazabahu.
6Basi, mufanye hivi: asubui, wewe pamoja na wafuasi wako, mutatwaa vyetezo,
7muweke makaa ya moto ndani na kutia ubani juu yake, kisha mutavipeleka mbele ya Yawe. Halafu tutaona ni nani aliyechaguliwa na Yawe. Ninyi Walawi mumepitisha kipimo!
8Musa akaendelea kumwambia Kora: Musikilize, enyi Walawi!
9Munaona ni jambo dogo kwenu kwamba Mungu wa Israeli amewachagua ninyi kati ya Waisraeli wote, kusudi muweze kumukaribia na kutumika katika hema la Yawe na kushugulika na kutumikia Waisraeli wote?
10Amewapatia heshima ya kuwa karibu naye, ninyi pamoja na Walawi wenzenu wote. Sasa munataka vilevile kazi ya ukuhani?
11Si Haruni tu munayemunungunikia, wewe na kundi lako, lakini kwa kweli munamwasi Yawe.
12Musa akatuma ujumbe kwa Datani na Abiramu wana wa Eliabu kusudi waitwe, lakini wao wakasema: Hatutakuja!
13Ni jambo dogo kwamba umetutoa Misri, inchi inayotiririka maziwa na asali, kusudi ukuje kutuua humu katika jangwa? Tena, unajifanya mukubwa wetu!
14Zaidi ya hayo, haukutuleta katika inchi inayotiririka maziwa na asali, wala kutupatia urizi wa mashamba na mashamba ya mizabibu. Unafikiri utawafanya hawa watu kuwa vipofu? Hatutakuja!
15Musa akakasirika sana, akamwambia Yawe: Usikubali sadaka za watu hawa. Mimi sijatwaa punda wa mutu yeyote, wala sijamuzuru mutu!
16Musa akamwambia Kora: Kesho usikose kuja pamoja na wafuasi wako mbele ya Yawe. Haruni vilevile atakuwa pale.
17Kila mumoja wenu atwae chetezo chake, na kutia ubani, kisha atakipeleka mbele ya Yawe; kwa jumla vitakuwa vyetezo mia mbili makumi tano; wewe vilevile na Haruni, kila mumoja atakuwa na chetezo chake.
18Basi, kila mumoja wao akatwaa chetezo chake, akatia makaa ya moto na ubani, kisha wakaenda na kusimama kwenye mulango wa hema la mukutano, pamoja na Musa na Haruni.
19Naye Kora akawakusanya watu wote pamoja, wakasimama mbele ya Musa na Haruni ambao walikuwa kwenye mulango wa hema la mukutano. Halafu utukufu wa Yawe ukawatokea watu wote.
20Hapo Yawe akamwambia Musa na Haruni:
21Mujitenge na watu hawa, niwaangamize sasa hivi.
22Lakini Musa na Haruni wakajitupa uso mpaka chini na kusema: Ee Yawe unayekuwa asili ya uzima wa wanadamu wote. Mutu mumoja akikukosea, utakasirikia watu wote pamoja?
23Yawe akamwambia Musa:
24Uwaambie watu waondoke karibu na makao ya Kora, Datani na Abiramu.
25Basi, Musa akaenda kwa Datani na Abiramu, akifuatwa na wazee wa Israeli.
26Alipofika, akawaambia watu: Tafazali muondoke kwenye hema za watu hawa waovu na musiguse kitu chao chochote, musiangamizwe pamoja nao kwa sababu ya zambi zao zote.
27Watu wakaondoka kwenye makao ya Kora, Datani na Abiramu.
Datani na Abiramu wakatoka katika mahema yao na kusimama kwenye mulango wakiandamana na wake zao na watoto wao wote hata wale wanaonyonya.
28Hapo Musa akawaambia watu: Hivi ndivyo mutakavyotambua kwamba Yawe ndiye aliyenituma kufanya mambo haya yote, wala siyo kwa mapenzi yangu mwenyewe.
29Watu hawa wakikufa kifo cha kawaida, au wakipatwa na hasara kama watu wengine, basi mujue kwamba Yawe hakunituma.
30Lakini Yawe akifanya jambo ambalo halijapata kutendeka, udongo ukifunguka na kuwameza watu hawa pamoja na kila kitu chao, na kwenda kuzimu wakiwa uzima, basi mutajua kwamba watu hawa wamemuzarau Yawe.
31Mara tu alipomaliza kusema maneno hayo yote, udongo chini ya Datani na Abiramu ikafunuka
32na kuwameza watu hao, jamaa zao, pamoja na wafuasi wote wa Kora na mali zao zote.
33Basi, wao, pamoja na vyote vilivyokuwa vyao wakashuka kuzimu wakiwa wangali wazima. Udongo ukawafunika, wote wakatoweka.
34Waisraeli wote wengine waliokuwa karibu waliposikia vilio vyao wakakimbia wakisema: Tukimbie, kusudi udongo usitumeze na sisi vilevile.
35Kisha Yawe akashusha moto ukawateketeza wale watu mia mbili makumi tano waliokwenda kufukiza ubani.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.