Muhubiri 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Kisha nikaona mateso yote yanayofanyika chini ya jua. Watu wanaogandamizwa wanalia machozi, lakini hakuna mutu yeyote anayewafariji. Wagandamizaji wao wana nguvu, ndiyo sababu hakuna wa kuwafariji.

2Basi, nikafikiri ndani ya moyo kwamba heri wafu waliokwisha kufa kuliko watu wanaokuwa wazima.

3Lakini heri zaidi kuliko wafu na wanaokuwa wazima, yule ambaye bado hajazaliwa na kuona maovu yote yanayotendeka hapa chini ya jua.

4Tena nilitambua kwamba mutu anatoa jasho na kutumia ujuzi wake juu ya wivu tu kwa mwenzake. Hayo nayo ni bure sawa na kutaka kukamata upepo.

5Mupumbafu hafanyi kazi na mwisho anajiua na njaa.

6Ni afazali kuwa na kidogo tu, pamoja na amani ndani ya moyo,

kuliko kutoa jasho kwa ajili ya kukamata upepo.

7Tena, niliona jambo moja la bure chini ya jua.

8Nilimwona mutu mumoja anayekuwa peke yake, hana mwana wala ndugu. Hata hivyo, haachi kutoa jasho. Hatosheki hata kidogo na mali yake wala hatulii na kujiuliza: “Ninatoa jasho kwa ajili ya nani na kujizuiza kuwa na raha?” Hayo nayo ni bure. Ni shuguli inayosikitisha.

9Ni afazali kuwa wawili kuliko mutu kuwa peke yake. Kwa sababu wawili watapata matunda ya jasho yao.

10Na mumoja akianguka, huyo mwenzake atamusimamisha. Lakini ole wake mutu anayekuwa peke yake akianguka! Huyo hatakuwa na mutu wa kumusimamisha!

11Vilevile watu wawili wakilala pamoja watapata joto. Lakini mutu akiwa peke yake atajipatia joto namna gani?

12Mutu akiwa peke yake anaweza kushindwa na adui, lakini wakiwa wawili watashinda adui. Kamba tatu zikisokotwa pamoja hazikatiki upesi.

13Afazali kijana masikini mwenye hekima kuliko mufalme muzee mupumbafu, ambaye hasikilizi shauri jema,

14hata ikiwa alikuwa mufungwa na sasa ni mufalme, au alizaliwa masikini na sasa ni mufalme.

15Niliwaona watu wote wanaoishi chini ya jua wakishikamana na yule kijana ambaye angekamata nafasi ya mufalme.

16Hesabu ya watu haikukuwa na mwisho, naye aliwatawala wote. Hata hivyo, wale wanaozaliwa nyuma hawatamufurahia. Hakika hayo nayo ni bure sawa na kutaka kukamata upepo.

Angalisho kwa kutoa ahadi

17Ukuwe mwangalifu unapokwenda katika nyumba ya Mungu na ukaribie kwa kusikiliza kwa uangalifu, kuliko kutoa sadaka kama vile wapumbafu wanavyofanya, watu wasiojua kwamba wanafanya mabaya.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help