Kumbukumbu la Sheria 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kushika sheria ya Mungu

1Musa akaendelea kusema: “Mushike basi na kufuata masharti na maagizo niliyowafundisha, kusudi mupate kuishi na kurizi inchi ambayo Yawe, Mungu wa babu zenu, anawapa.

2Musiongeze chochote katika amri ninazowapa, wala musipunguze kitu. Mushike amri za Yawe, Mungu wenu, ambazo ninawapa.

3Ninyi muliona kwa macho yenu mambo ambayo Yawe aliyafanya juu ya Bali-Peori. Yawe, Mungu wenu, aliwaangamiza watu wote kati yenu waliomwabudu huyo mungu Bali-Peori.

4Lakini ninyi muliokuwa waaminifu kwa Yawe, Mungu wenu muko wazima mpaka leo.

5“Muangalie! Nimewafundisha masharti na maagizo kama vile Yawe, Mungu wangu alivyoniamuru nifanye, kusudi muyashike katika inchi munayokwenda kuirizi.

6Mushike na kutimiza masharti na maagizo hayo maana mukifanya hivyo watu wa mataifa mengine watakapopata kujua masharti hayo, watatambua kwamba ninyi ni wenye hekima na akili. Watasema hivi: ‘Kweli watu wa taifa hili kubwa wana hekima na akili!’

7“Hakuna taifa lolote hata likuwe kubwa namna gani, ambalo mungu wake yuko karibu nalo, kama vile Yawe, Mungu wetu, anavyokuwa karibu nasi tunapomwomba musaada.

8Wala hakuna taifa lingine lolote hata likuwe kubwa namna gani, lenye masharti na maagizo ya haki, kama hayo ambayo nimewafundisha siku hii ya leo.

9“Lakini mukuwe waangalifu na kufanya angalisho sana kusudi musisahau mambo yale muliyoona kwa macho yenu wenyewe, kusudi isitokee hata mara moja katika maisha yenu mambo hayo kusahaulika ndani ya mioyo yenu. Muwaelezee watoto wenu na wajukuu wenu

10juu ya siku ile ambayo mulisimama mbele ya Yawe, Mungu wenu, kule Horebu, ndio Sinai, aliponiambia: ‘Muwakusanye hao watu mbele yangu, niwaambie maneno yangu kusudi wajifunze kuniogopa mimi siku zote za maisha yao, na kuwafundisha watoto wao kufanya hivyo’.

11“Basi, mulikaribia na kusimama chini ya ule mulima ambao wakati huo ulikuwa unawaka moto uliofika mpaka mbinguni ukiwa umetanda giza na wingu zito.

12Kisha Yawe akasema nanyi kutoka katikati ya moto huo. Mukasikia maneno aliyosema lakini hamukumwona. Mulisikia tu sauti yake.

13Naye akawatangazia agano lake akawaamuru mulishike maana yake mutii zile amri kumi ambazo aliandika juu ya vibao viwili vya mawe.

14Wakati huo Yawe akaniamuru niwafundishe masharti na maagizo yote ambayo munapaswa kutimiza katika inchi munayokwenda kuirizi.

Onyo juu ya kuabudu sanamu

15“Kwa hiyo mukuwe waangalifu kusudi musisahau kwamba Yawe aliposema nanyi kule kwenye milima ya Horebu katikati ya moto hamukumwona kwa umbo. Kwa sababu hiyo mufanye angalisho sana,

16musipotoke kwa kujifanyia sanamu yoyote ya kuchonga, au ya umbo au mufano wowote, mufano wa wanaume au wanawake,

17wa nyama yeyote katika dunia au ndege,

18au mufano wa nyama anayetambaa juu ya udongo au wa samaki ndani ya maji.

19Mufanye angalisho kusudi wakati mutakapoangalia na kuona nyota, vitu vyote vya mbinguni, musivutwe kuviabudu na kuvitumikia. Vitu hivyo Yawe amewaachia watu wengine waviabudu.

20Lakini ninyi ndio watu aliowakomboa kutoka Misri katika furu la chuma. Aliwatoa huko kusudi mukuwe watu wake kama vile munavyokuwa hivi leo.

21Kwa sababu yenu Yawe, Mungu wenu, alinikasirikia, akaapa kwamba mimi sitavuka muto Yordani kuingia katika inchi ile nzuri anayowapa ikuwe mali yenu.

22Mimi nitakufia katika inchi hii wala sitauvuka muto, lakini ninyi muko karibu kuuvuka na kwenda kurizi inchi ile nzuri.

23Mufanye angalisho sana kusudi musisahau agano ambalo Yawe, Mungu wenu, amefanya nanyi. Musijifanyie sanamu ya kuchonga katika umbo la kitu chochote ambacho Yawe, Mungu wenu, amewakataza kumufananisha nacho,

24maana Yawe, Mungu wenu, ni moto unaoteketeza. Yeye ni Mungu mwenye wivu.

25-26“Mimi leo ninaita mbingu na dunia zishuhudie juu yenu. Mutakapokuwa mukikaa katika inchi hiyo, mukipata watoto na wajukuu na kuwa wazee, kama mukianza kupotoka na kujifanyia sanamu katika umbo la kitu chochote, mukifanya uovu mbele ya Yawe, Mungu wenu, na kumukasirikisha, mara moja mutaangamia kabisa katika inchi ambayo munaenda kurizi huko ngambo ya muto Yordani. Hamutaishi huko muda murefu, lakini mutaangamizwa kabisa.

27Yawe atawatawanya kati ya mataifa mengine, na ni wachache tu wenu watakaobakia huko ambako Yawe atawafukuzia.

28Huko mutatumikia miungu ya miti na mawe ambayo imetengenezwa kwa mikono ya watu na ambayo haiwezi kuona, haisikii, haikuli wala kunusa.

29Kisha kutoka humohumo katika inchi mutamutafuta Yawe, Mungu wenu, nanyi mutamupata kama mukimutafuta kwa moyo wote na roho yote.

30Mambo haya yote yatakapowapata huko, kisha mukipata taabu, mutamurudilia Yawe na kumutii.

31Yawe, Mungu wenu, ni Mungu mwenye rehema, hatawaachilia wala kuwaangamiza, wala kusahau agano ambalo alifanya na wazee wenu kwa kiapo.

32“Mufikiri sana juu ya matukio ya zamani, mambo yaliyotukia mbele ninyi hamujazaliwa, tangu siku ile Mungu alipomwumba mutu katika dunia. Muulize katika ulimwengu wote, toka pembe moja mpaka nyingine, kama jambo la ajabu la namna hii limepata kutokea au kusikilika!

33Watu walikwisha kusikia sauti ya Mungu ikisema toka katikati ya moto, kama ninyi mulivyosikia, wakabaki wazima?

34Kuna Mungu yeyote mwingine aliyejaribu hata kidogo kwenda kujitwalia taifa lake kutoka taifa lingine, kama vile Yawe, Mungu wenu, alivyofanya, kwa kutumia majaribio, vitambulisho, maajabu, vita, na vitisho? Hapana. Lakini mulishuhudia kwa macho yenu namna Yawe alivyofanya kwa mukono wake wenye nguvu kabisa kule Misri.

35Ninyi mulijaliwa kuona mambo hayo, kusudi mupate kutambua kwamba Yawe ndiye peke yake Mungu na wala hakuna mwingine.

36Aliwafanya muisikie sauti yake kutoka mbinguni kusudi aweze kuwafundisha; na hapa katika dunia akawafanya muone moto wake mukubwa na kusikia maneno yake kutoka katikati ya moto huo.

37Kwa kuwa aliwapenda wazee wenu, yeye amewachagua ninyi wazao wao, akawatoa yeye mwenyewe katika inchi ya Misri kwa nguvu yake kubwa.

38Alifukuza mbele yenu mataifa makubwa na yenye nguvu kuliko ninyi, kusudi awalete na kuwapa inchi yao ikuwe urizi wenu, kama vile inavyokuwa mpaka leo!

39Basi, mukumbuke leo na kuweka ndani ya mioyo yenu, kwamba Yawe ndiye Mungu juu mbinguni na chini katika dunia. Hakuna mwingine.

40Kwa hiyo mushike masharti yake na amri zake ambazo ninawapa leo kusudi mufanikiwe, ninyi pamoja na wazao wenu, na kuishi siku nyingi katika inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapa ikuwe yenu milele.”

Miji ya kukimbilia upande wa mashariki wa Yordani

41Halafu Musa akatenga miji mitatu upande wa mashariki ya muto Yordani,

42ambamo mutu ataweza kukimbilia na kujiponyesha, kama ameua mutu ambaye si adui yake kwa bahati mbaya. Mutu kama huyo ataweza kukimbilia katika muji mumoja na kuyaokoa maisha yake.

43Alitenga muji wa Beseri katika bonde la jangwa kwa ajili ya kabila la Rubeni, muji wa Ramoti katika inchi ya Gileadi kwa ajili ya kabila la Gadi, na muji wa Golani katika inchi ya Basani kwa ajili ya kabila la Manase.

Utangulizi wa sheria ya Mungu

44Hii ndiyo sheria ambayo Musa aliwapa Waisraeli.

45Haya ndiyo maagizo, masharti na maamuzi ambayo Musa aliwaambia Waisraeli walipotoka Misri,

46wakiwa ngambo ya muto Yordani, katika bonde linalokuwa mbele ya Beti-Peori, katika inchi iliyokuwa ya mufalme Sihoni wa Waamori, aliyetawala kutoka katika muji wa Hesiboni, ambaye Musa na Waisraeli walimushinda walipotoka Misri.

47Walitwaa inchi yake na inchi ya mufalme Ogi wa Basani. Wafalme hao wawili wa Waamori walitawala huko upande wa mashariki wa muto Yordani.

48Inchi hiyo ilienea toka Aroeri kwenye ukingo wa muto Arnoni, mpaka mulima Sirioni, ni kusema Hermoni,

49pamoja na eneo lote upande wa mashariki wa muto Yordani mpaka bahari ya Chumvi, kwa mwisho wa miteremuko ya mulima Pisiga.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help