Isaya 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu ataazibu Babeli

1Haya ni maono, ambayo nabii Isaya mwana wa Amozi, aliyofunuliwa na Mungu juu ya inchi ya Babeli:

2Mungu anasema:

Musimike bendera juu ya mulima usiokuwa na miti,

muwapigie waaskari kelele,

muwapepee watu kwa mukono,

mukiwaita waingie kwenye milango ya muji wa wakubwa.

3Mimi nimewaamuru wachaguliwa wangu,

nimewaita mashujaa wangu,

hao wenye kunitukuza wakishangilia,

wakuje kutimiza hasira yangu.

4Musikilize kelele kwenye milima

kama za kundi kubwa la watu!

Musikilize kelele za falme,

na mataifa yanayokusanyika!

Yawe wa majeshi

analichunguza kundi linalokwenda kwa vita.

5Wanakuja kutoka inchi za mbali,

wanatoka hata miisho ya dunia:

Yawe na silaha za hasira yake

anakuja kuiangamiza dunia.

6Mulie, maana siku ya Yawe imekaribia;

inakuja kama uharibifu kutoka kwa Mungu Mwenye Nguvu.

7Kwa hiyo mikono ya kila mutu itaregea,

kila mutu atavunjika moyo.

8Watu watafazaika,

watashikwa na hofu na maumivu,

watakuwa na uchungu kama mama anapozaa.

Wataangalia kwa mashaka,

nyuso zao zitaungua kwa haya.

9Siku ya Yawe inakuja,

siku kali, ya kasirani na hasira kali.

Itaifanya inchi kuwa uharibifu,

itawaangamiza wenye zambi ndani yake.

10Nyota na vikundi vyake katika anga hazitaangaza;

jua linapochomoza litakuwa giza,

na mwezi hautatoa mwangaza wake.

11Yawe anasema hivi:

Nitauazibu ulimwengu kwa uovu wake,

waovu kwa sababu ya makosa yao.

Nitakikomesha kiburi cha wenye majivuno,

na kuporomosha mazarau ya watu wakali.

12Nitawafanya watu kuwa wachache kuliko zahabu safi;

wanadamu watakuwa wachache kuliko zahabu ya Ofiri.

13Nitazitetemesha mbingu

nayo inchi itatikisika katika misingi yake

kwa sababu ya kasirani ya Yawe wa majeshi,

siku ile ya hasira yangu kali.

14Kama swala anayewindwa,

kama kondoo wasiokuwa na muchungaji,

kila mumoja atajiunga na watu wake,

kila mutu atakimbilia katika inchi yake.

15Yeyote atakayeonekana atapigwa mukuki,

atakayekamatwa atauawa kwa upanga.

16Watoto wao wachanga watapondwapondwa mbele yao,

watanyanganywa nyumba zao,

na watalala na wake zao kwa kinguvu.

17Ninawachochea Wamedi juu yao;

watu ambao hawajali feza

wala hawavutwi na zahabu.

18Mishale yao itawaua vijana,

hawatarehemu watoto,

wala kuwahurumia watoto wachanga.

19Babeli ni utukufu wa falme zote

na sifa na majivuno ya Wakaldea

utakuwa kama Sodoma na Gomora,

wakati Mungu alipoiangamiza.

20Hautakaliwa tena na watu hata kidogo,

watu hawataishi humo katika vizazi vyote.

Hakuna Mwarabu atakayesimamisha hema yake humo,

wala muchungaji atakayechunga nyama wake humo.

21Pahali pake ni nyama wakali wa pori ndio watakuwa ndani yake,

bundi watajaa katika nyumba zake.

Mbuni wataishi humo,

pepo watachezea huko.

22Fisi watalia ndani ya pango zake,

mbweha wataonekana ndani ya nyumba zao za raha.

Wakati wa Babeli umekaribia,

wala siku zake hazitaongezwa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help