Walawi 17 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maagizo juu ya damu

1Yawe akamwambia Musa:

2Uwaambie Haruni, wana wake na watu wote wa Israeli maagizo haya:

3Kama mutu yeyote kati ya Waisraeli akichinja ngombe au mwana-kondoo au mbuzi ndani au inje ya kambi,

4bila kumuleta nyama huyo kwenye mulango wa hema la mukutano kwa kumutolea Yawe mbele ya makao yake, mutu yule atakuwa na kosa ya kumwanga damu. Amemwanga damu na atatengwa na watu wake.

5Agizo hili linalazimisha Waisraeli kuletea Yawe nyama ambao wanawachinja katika mashamba. Wataleta nyama wale kwa kuhani kwenye mulango wa hema la mukutano, naye atawachinja na kumutolea Yawe sadaka za amani.

6Basi, kuhani atanyunyizia damu kwenye mazabahu ya Yawe inayokuwa kwenye mulango wa hema la mukutano na kuteketeza yale mafuta yakuwe harufu nzuri ya kumupendeza Yawe.

7Kwa hiyo Waisraeli watakoma kabisa kuwatambikia miungu ya uongo wenye umbo la beberu, jambo ambalo limewafanya wakose uaminifu kwangu. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyao vyote.

8Uwaambie kwamba mutu yeyote kati ya Waisraeli au mugeni anayeishi kati yao, anayetoa sadaka ya kuteketezwa au sadaka ingine,

9lakini haileti mbele ya mulango wa hema la mukutano kwa kumutolea Yawe, mutu yule atatengwa na watu wake.

10Kama mutu yeyote wa jamii ya Israeli au mugeni anayeishi kati yao anakula damu yoyote, mimi nitamukasirikia mutu yule aliyekula damu na kumutenga mbali na watu wake. Ang. Mwa 9.4; Law 7.26-27; 19.26; Kumb 12.16,23; 15.23

11Itakuwa hivyo kwa sababu uzima wa kiumbe uko katika damu. Nimewaagiza kutolea damu kwenye mazabahu kwa kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya roho zenu, kwa sababu damu inafanya upatanisho, nao uzima uko katika damu. Ang. Ebr 9.22

12Ndiyo maana nimewaagiza Waisraeli hivi: mutu yeyote kati yenu wala mugeni anayeishi kati yenu asikule damu.

13Mutu yeyote kati ya Waisraeli au mugeni anayekaa kati yao akienda kuwinda nyama au ndege, anapaswa kumwanga damu chini na kuifunika kwa udongo.

14Maana, uzima wa kila kiumbe uko katika damu. Ndiyo maana nimewaagiza Waisraeli, wasikule damu ya kiumbe chochote maana uzima wa kiumbe chochote ni damu yake. Yeyote atakayekula damu atatengwa.

15Mutu yeyote akuwe ni mwenyeji au mugeni, anayekula chochote kilichokufa chenyewe au kilichouawa na nyama wa pori anapaswa kufua nguo zake na kuoga. Atakuwa muchafu mpaka magaribi. Nyuma ya hapo atakuwa safi.

16Lakini kama hafui nguo zake na kuoga, mutu huyu atabeba lazima ya uovu wake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help