Zaburi 94 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu mwamuzi wa wote

1Ee Yawe, Mungu mwenye kulipiza kisasi,

ewe Mungu mwenye kulipiza kisasi,

ujitokeze!

2Usimame, ee mwamuzi wa watu wote;

uwaazibu wenye kiburi inavyowastahili!

3Waovu wataona utukufu mpaka wakati gani?

Watajisifia mpaka wakati gani, ee Yawe?

4Mpaka wakati gani waovu watajigamba kwa maneno?

Watajivuna na kujitapa mpaka wakati gani?

5Wanaangamiza watu wako, ee Yawe,

wanawagandamiza hao wanaokuwa mali yako.

6Wanaua wajane na wageni;

wanachinja wayatima.

7Wanasema: “Yawe haoni,

Mungu wa Yakobo hajui.”

8Enyi wajinga wa mwisho, mufikiri kidogo!

Enyi wapumbafu, mutapata akili wakati gani?

9Aliyefanya sikio, yeye hawezi kusikia?

Aliyeumba jicho, yeye hawezi kuona?

10Mwenye kuonya mataifa, yeye hawezi kuazibu?

Mwenye kufundisha wanadamu, yeye hana akili?

11Yawe anajua mawazo ya watu;

anajua kwamba hayafai kitu.

12Heri mutu unayemwadibisha, ee Yawe,

mutu unayefundisha sheria yako,

13kusudi siku ya taabu apate utulivu,

mpaka waovu wachimbiwe shimo.

14Yawe hatawaachilia watu wake;

hatawatupa hao wanaokuwa mali yake.

15Maana hukumu zitatolewa kwa haki tena,

na wote wenye moyo wa usawa watazifuata.

16Nani aliyenisaidia kumupinga mutu mwovu?

Nani aliyekuwa upande wangu juu ya wabaya?

17Yawe asingalinisaidia,

ningalikwisha kwenda kwenye inchi ya wafu.

18Nilipotambua kwamba ninateleza,

wema wako, ee Yawe, ulinikingia.

19Mahangaiko ya moyo wangu yanapozidi,

wewe unanifariji na kunifurahisha.

20Wewe hauwezi kushirikiana na waamuzi wapotovu,

wanaotunga masharti za kutetea maovu.

21Wao wanapatana kuwaangamiza watu wa haki,

na kuwahukumu watu wasiokuwa na kosa wauawe.

22Lakini Yawe ni kimbilio langu;

Mungu wangu ni kikingio changu.

23Atawarudishia uovu wao wenyewe,

atawateketeza kwa sababu ya ubaya wao.

Yawe, Mungu wetu, atawateketeza kabisa!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help