1 Timoteo 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Angalisho na walimu wa uongo

1Roho Mutakatifu anasema wazi kwamba katika nyakati za mwisho, watu wengine watapotoka katika imani yao na kufuata roho za udanganyifu na mafundisho ya pepo.

2Wanadanganywa na watu wenye uongo na wanafiki wenye zamiri iliyokufa, iliyoharibika kabisa kama vile imeteketezwa kwa moto.

3Wao wanafundisha kwamba ni vibaya kuoana, na wanawakataza watu kula vyakula fulani fulani. Lakini Mungu aliumba vyakula vile kusudi watu waliokwisha kumwamini na kutambua ukweli wapate kuvitumia wakisha kumushukuru.

4Kila kitu Mungu alichokiumba ni kizuri, wala hakuna kile kinachopaswa kukataliwa, lakini inafaa kumushukuru Mungu mbele ya kukikula.

5Kwa maana kwa njia ya neno la Mungu na ya maombi, chakula kinatakaswa mbele yake.

Mashauri mbalimbali

6Kama ukiwaelezea waziwazi wandugu maneno hayo, utakuwa mutumishi mwema wa Kristo Yesu, mwenye kukulishwa kiroho na maneno ya imani na mafundisho mazuri uliyoshika kabisa.

7Lakini ukatae hadisi za uongo zilizotungwa na wanawake wazee. Ujizoeze katika maisha yako kumwabudu Mungu kwa ukweli.

8Mazoezi ya mwili yana mafaa kidogo, lakini kushikamana na ibada kuna mafaa katika mambo yote, kwa maana kunatupatia ahadi ya kuishi kwa wakati huu wa sasa na kwa wakati utakaokuja.

9Neno hilo ni la kuaminiwa, nalo linastahili kukubaliwa kabisa.

10Na ni kwa hiyo tunasumbuka na kupigana, kwa maana tunamutumainia Mungu Mwenye Uzima, Mwokozi wa watu wote na hasa zaidi Mwokozi wa waamini.

11Hayo ndiyo maneno unayopaswa kuagiza na kufundisha.

12Usijiachilie kuzarauliwa na mutu yeyote kwa sababu ungali bado kijana. Lakini ukuwe mufano kwa waamini, katika masemi yako, katika mwenendo wako, katika upendo, katika imani na katika maisha safi.

13Kwa kungojea mpaka nitakapofika, ujitolee kwa kuwasomea watu Maandiko Matakatifu kwa kuwaonya na kuwafundisha.

14Usiache kutumia ile zawadi ya kiroho inayokuwa ndani yako, uliyopokea kutokana na maneno ya manabii na kwa njia ya kuwekewa mikono na wazee wa kanisa.

15Ufikiri sana juu ya mambo hayo na ujitolee kwa kuyatimiza hata watu wote waone waziwazi maendeleo yako.

16Ujiangalie wewe mwenyewe na kuangalia mafundisho yako, nawe ushikamane nayo. Kwa maana ukifanya hivi, utajiokoa wewe mwenyewe na kuokoa wale wanaokusikiliza.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help