1Ule mungu Bali ameanguka;
mungu Nebo anainama.
Sanamu zao zinabebwa juu ya nyama,
juu ya nyama wanaobeba mizigo!
Vitu ninyi mulivyokuwa mukiviinua juu, vinakuwa sasa mizigo,
vinakuwa mizigo mizito juu ya nyama wenye kuchoka.
2Wanajiinamisha, wanainama pamoja.
Hawakuweza kuziokoa sanamu zao.
Wao wenyewe vilevile wamepelekwa katika utumwa!
3Musikilize, enyi wazao wa Yakobo,
munisikilize, enyi mabaki ya watu wangu wa Israeli.
Mimi niliwatunza ninyi tangu mulipozaliwa;
niliwabeba ninyi tangu katika tumbo la mama yenu.
4Mimi nitabaki yuleyule hata katika uzee wenu;
hata katika wakati wenu wa imvi mimi nitawabeba.
Nilifanya hivyo kwanza,
nitafanya hivyo tena.
Nitawabeba ninyi na kuwaokoa.
5Mutanifananisha na nani na kunisawanisha naye?
Mutanilinganisha na nani nipate kuwa sawasawa naye?
6Watu wanapoteza zahabu kutoka mifuko yao,
wanapima feza kwenye mizani zao,
wanamulipa mufuaji wa zahabu awatengenezee sanamu ya mungu,
kisha wanainama mbele yake na kuiabudu!
7Wanajibebesha sanamu hiyo juu ya mabega na kuipeleka,
kisha wanaiweka pahali pake, nayo inakaa palepale;
haiwezi hata kidogo kusogea kutoka pale inapokuwa.
Mutu akiililia, haiwezi kumwitikia,
wala haiwezi kumwokoa mutu katika taabu zake.
8Mukumbuke jambo hili na kufikiri,
mujiulize ndani ya mioyo yenu enyi waasi.
9Mukumbuke mambo niliyotenda hapo zamani!
Mimi ni Mungu.
Hakuna Mungu mwingine.
Mimi ni Mungu.
Hakuna mwingine kama mimi.
10Nilitangaza mambo ya mwisho tangu mwanzo,
tangu zamani nilitangaza mambo yatakayotukia.
Kusudio langu litatimia;
mimi nitatimiza nia yangu yote.
11Ninamwita tai wangu kutoka mashariki,
ambaye atatimiza kusudi langu toka inchi ya mbali.
Mimi nimesema na nitafanya;
mimi nimepanga nami nitatimiza.
12Musikilize, enyi wenye vichwa vigumu,
munisikilize enyi munaokuwa mbali na ukombozi.
13Siku ya kuwakomboa inakaribia,
haiko mbali tena;
siku ya kuwaokoa ninyi haitachelewa.
Nitauokoa Sayuni,
nitaleta utukufu kwa Israeli.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.