Habakuki 1 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Haya ni maono ambayo nabii Habakuki aliyofunuliwa na Mungu.

Malalamiko ya nabii

2Ee Yawe, nitakulilia mpaka wakati gani,

nawe usinisikilize na kunisaidia?

Kwa nini ninalia “Mateso makali!”

nawe hautuokoi?

3Kwa nini unaniachilia kuona mabaya na taabu?

Uharibifu na mateso makali vinanizunguka,

ugomvi na mabishano yanatokea.

4Hivyo sheria haina nguvu,

wala haki haifuatiliwi.

Waovu wanawazunguka wenye haki,

hivyo hukumu inatolewa na sheria imepotoshwa.

Jibu la Mungu

5Mungu akasema:

Muangalie mataifa, muone!

Mustaajabu na kushangaa.

Maana ninatenda kitu ukiwa bado unaishi,

kitu ambacho ungeambiwa haungesadiki.

6Maana ninawachochea Wakaldea,

taifa lile kali na lenye nguvu,

taifa linalopita katika inchi yote,

kwa kunyanganya makao ya watu wengine.

7Wao ni watu wa kuchukiza na kutisha;

wao wanajiamulia sheria wenyewe na kujipatia mamlaka.

8Farasi wao ni wepesi kuliko chui,

wakali kuliko imbwa wa pori wenye njaa.

Waaskari wapanda-farasi wao wanatoka mbali,

wanaruka mbio kama tai anavyorukia nyama.

9Wote wanakuja kwa kutesa kwa ukali;

wanafukuzia wakikaza macho mbele,

wanakusanya wafungwa wengi kama muchanga.

10Wanawachekelea wafalme,

na kuwazarau watawala.

Kila kuta kwao ni muzaha,

wanailundikia udongo na kuiteka.

11Kisha wanasonga mbele kama upepo,

wanapita na kufanya makosa.

Nguvu zao ndio mungu wao!

Habakuki analalamika tena

12Wewe si ndiwe Yawe,

tangu zamani sana?

Wewe ndiwe Mungu wangu, Mutakatifu wangu, usiyekufa.

Ee Yawe, umewachagua Wakaldea watuhukumu!

Ewe kimbilio letu, umewaimarisha kusudi watuazibu!

13Wewe ni mutakatifu kabisa, hauwezi kutazama uovu,

hauwezi kuvumilia hata kidogo kuona mabaya.

Mbona basi unawaona wafanya maovu na kunyamaza,

kwa nini unanyamaza waovu wanapowamaliza

wale watu wanaokuwa wenye haki kuliko wao?

14Umewafanya watu kama samaki katika bahari,

kama viumbe vinavyotambaa visivyokuwa na mwongozi!

15Wakaldea wanawavua watu kwa ndoana,

wanawakokotea inje kwa nyavu zao,

wanawakusanya wote katika wavu wao,

kisha wanafurahi na kushangilia.

16Kwa hiyo, wanazitambikia nyavu zao,

na kuzifukizia ubani;

maana kwa njia ya vitu hivyo mapato yao yanaongezeka,

na wanakuwa na chakula kingi.

17Hawataacha hata kidogo kuvuta upinde wao?

Wataendelea tu kuwanasa watu,

na kuyaangamiza mataifa bila huruma?

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help