2 Wakorinto 11 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Ingekuwa heri muvumilie kidogo masemi yangu ya upumbafu! Ninawaomba kweli munivumilie!

2Mimi ninasikia wivu kwa ajili yenu sawa vile Mungu anavyousikia vilevile. Kwa maana ninyi ni kama binti mukamilifu niliyemwowesha kwa mume mumoja, ndiye Kristo.

3Lakini ninaogopa kwamba sawa vile nyoka alivyomudanganya Eva kwa werevu wake, mawazo yenu vilevile yasipotoshwe hata mupate kupoteza uaminifu na ukamilifu wenu kwa Kristo.

4Hii inatokana na kuona jinsi munavyomukubali mutu yeyote anayekuja kwenu na kuwahubiri habari za Yesu mwingine asiyekuwa yule sisi tuliyemuhubiri. Na zaidi ya hii munakubali upesi kupokea roho ingine na ujumbe mwingine vinavyokuwa tofauti na Roho au Habari Njema muliyopokea toka kwetu.

5Ninazani kwamba wale mitume wanaohesabiwa kuwa wakubwa zaidi hawanipiti kitu kabisa.

6Inaonekana kuwa mimi si mutu anayeelewa kusema, lakini kwa ngambo ya elimu, mimi ninaielewa sana. Nasi tumeonyesha hayo yote kila wakati na katika mambo yote.

7Mimi niliwatangazia Habari Njema ya Mungu bila kudai mushahara. Nilijinyenyekeza kusudi mupate kutukuzwa. Basi kwa kujinyenyekeza vile, nilifanya kosa?

8Nilipokuwa nikitumika kati yenu nililipwa na makanisa mengine. Ni kama vile nilinyanganya mali ya makanisa yale na kuitumia kwa kuwasaidia.

9Wakati nilipokuwa kwenu, sikumulemea mutu yeyote nilipohitaji kitu fulani, kwa maana wandugu waliotoka Makedonia waliniletea vitu vyote nilivyohitaji. Nilijiangalia vizuri katika mambo yote kusudi nisiwalemee, nami nitaendelea kujiangalia vema.

10Kufuatana na vile ninavyosema ukweli kama vile Kristo, ninaapa kwamba hakuna anayeweza kunizuiza kujivuna juu ya jambo hilo katika jimbo lote la Akaya.

11Kwa sababu gani ninasema hivi? Kwa sababu siwapendi? Hapana, Mungu anajua kwamba ninawapenda.

12Nitaendelea kufanya sawasawa ninavyofanya kwa sasa, kusudi niwafungie njia zote wale wanaotafuta kujivuna kwamba wanatumika sawa sisi.

13Watu wale ni mitume wa uongo, wanafanya kazi yao kwa udanganyifu wakijisingizia kuwa mitume wa kweli wa Kristo.

14Na jambo hilo si la kushangaza kwa maana Shetani mwenyewe anajisingizia kuwa malaika wa mwangaza.

15Basi si jambo la ajabu kama watumishi wake vilevile wanajigeuza kuwa watumishi wa haki. Kwa mwisho wao watalipwa kufuatana na matendo yao.

Paulo anavumilia mateso yake ya kitume

16Mimi ninasema tena: mutu asinizanie kuwa mupumbafu. Kama si vile, basi munihesabu kama mupumbafu, kusudi nami nipate kujivuna kidogo vilevile.

17Maneno haya ninayosema sasa hayafuatani na mapenzi ya Bwana, lakini ninayasema tu kama mupumbafu kuelekea jambo hili la kujivuna.

18Watu wengi wanajivuna kwa namna ya kimwili, kwa sababu hiyo mimi nitajivuna vilevile.

19Ninyi munajidai kuwa wenye hekima na ndiyo maana munapenda kuwavumilia wapumbafu!

20Munavumilia hata mutu anayewatia katika utumwa, anayeiba mali zenu, anayewagandamiza, anayewazarau na anayewapiga kofi kwenye uso.

21Ninasikia haya ya kuisema: tumekuwa zaifu kwa kufanya vile!

Lakini kama watu wengine wanasubutu kujivuna juu ya kitu chochote, mimi vilevile nitajivuna. Sasa ninasema kama vile mupumbafu.

22Watu wale ni Waebrania? Mimi vilevile. Wao ni Waisraeli? Mimi vilevile. Wao ni wa uzao wa Abrahamu? Mimi vilevile.

23Sasa nitasema kama mwenda-wazimu: wao ni watumishi wa Kristo? Mimi ni mutumishi wake zaidi kuliko wao. Nimetumika kazi nyingi zaidi, nimefungwa mara nyingi zaidi, nimepigwa zaidi, na mara nyingi nimekuwa katika hatari ya kufa.

24Mara tano Wayuda wamenipiga viboko makumi tatu na tisa.

25Waroma wamenipiga fimbo mara tatu na mara moja walitaka kuniua kwa kunitupia mawe. Mara tatu chombo nilichosafiri nacho kilizama kwa kuvunjika. Mara moja, nilishinda ndani ya bahari kwa muda wa siku nzima.

26Katika safari zangu nyingi nimepata hatari ya mafuriko ya mito, hatari ya wanyanganyi, hatari kutoka kwa wanainchi wenzangu na kutoka kwa watu wa mataifa mengine. Nilikuwa katika hatari ndani ya miji, katika jangwa, katika bahari na kati ya wandugu za uongo.

27Nimesumbuka kwa kufanya kazi ngumu, nimepata magumu, nimekesha mara nyingi. Mara nyingi niliteswa na njaa na kiu; mara nyingi nililazimishwa kutokula. Nimeteseka na baridi na ukosefu wa nguo.

28Na bila kutaja mambo yote mengine kama hayo, kila siku ninashugulika na makanisa yote.

29Kukiwa mutu anayepatwa na uzaifu, mimi ninajisikia muzaifu vilevile. Kukiwa mutu anayeanguka katika zambi, ninasikia uchungu.

30Kama ikinipasa kujivuna nitajivuna kwa ajili ya uzaifu wangu.

31Mungu Baba ya Bwana Yesu, anayetukuzwa hata milele, anajua kwamba sisemi uongo.

32Wakati nilipokuwa Damasiki, liwali wa mufalme Areta aliweka walinzi katika muji ule kusudi wanikamate.

33Lakini wakanitia ndani ya kitunga na kunishusha kwenye ukuta wa muji, tokea ndani ya dirisha, nami nikapata kuponyoka.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help