Waroma 15 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Namna ya kuwatendea wengine

1Sisi tunaokuwa na nguvu katika imani tunapaswa kubeba muzigo wa uzaifu wa wale wasiokuwa na nguvu. Tusifanye tu mambo yanayotupendeza wenyewe.

2Lakini kila mumoja wetu anapaswa kumupendeza mwingine kwa kumutendea mema na kuweza hivi kumujenga katika imani.

3Kwa maana hata Kristo hakufanya mambo yanayomupendeza mwenyewe sawa vile ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Matusi wanayokutukana, yananiangukia.”

4Na yote yaliyoandikwa zamani katika Maandiko Matakatifu yameandikwa kwa ajili ya kutufundisha sisi, kusudi tuendelee kuchunga tumaini kwa njia ya kuvumilia na kufarijiwa sawa tunavyofundishwa katika Maandiko Matakatifu.

5Basi, Mungu anayewapa watu nguvu ya kuvumilia na kufarijika awape kuwa na nia moja mukifuata mufano wa Kristo Yesu.

6Hivi kusudi mutaweza kwa nia moja na kwa sauti moja kumutukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.

Habari Njema kwa watu wote

7Basi mupokeane kwa upendo sawa vile Kristo alivyotupokea kusudi Mungu apate kutukuzwa.

8Kwa maana ninawaambia wazi kwamba Kristo alifanya utumishi kwa ajili ya Wayuda kwa kuhakikisha kuwa Mungu ni mwaminifu na kusudi atimize ahadi zile babu zetu walizopewa.

9Vilevile ilikuwa kusudi watu wa mataifa mengine wamutukuze Mungu kwa huruma yake, kama inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu:

“Kwa hiyo nitakutukuza kati ya mataifa,

nitakuimbia sifa.”

10Na tena Maandiko yanasema:

“Ninyi watu wa mataifa yote mufurahi pamoja na taifa lake!”

11Na tena hivi:

“Enyi mataifa yote, mumusifu Bwana;

enyi watu wote, mumusifu!”

12Isaya naye anasema:

“Muzao wa Yese atatokea,

atatawala watu wa mataifa,

nao watamutumainia.”

13Basi, Mungu anayekuwa musingi wa matumaini, awajaze furaha kamili na amani kutokana na imani yenu; hata tumaini lenu lipate kuongezeka kwa nguvu ya Roho Mutakatifu.

Utumishi wa Paulo

14Wandugu zangu, kwa ngambo yangu ninajua hakika kwamba ninyi munajaa wema, nanyi munafahamu yote yanayofaa na munaweza kushauriana vizuri.

15Lakini mara moja moja nimewaandikia kwa uhodari juu ya mambo fulani kusudi niwakumbushe tena mambo yale. Nimefanya vile kutokana na neema ile niliyopewa na Mungu

16kuwa mutumishi wa Yesu Kristo kwa watu wa mataifa mengine. Ninafanya kazi ya ukuhani ya kuhubiri Habari Njema ya Mungu, kusudi watu wa mataifa mengine wapate kuwa kama sadaka inayokubaliwa na Mungu na iliyotakaswa na Roho Mutakatifu.

17Basi katika kuungana kwangu na Kristo, ninaweza kujisifu kwa ajili ya kazi hii ninayomutumikia Mungu.

18Kwa maana sitasubutu kuongeza kitu kingine, isipokuwa tu kile Kristo alichotimiza kwa njia yangu kusudi watu wa mataifa wapate kumutii Mungu. Alifanya vile kwa njia ya yale aliyoniwezesha kusema na kutenda,

19kwa njia ya uwezo wa vitambulisho na maajabu, na kwa uwezo wa Roho Mutakatifu. Hivi tokea Yerusalema mpaka kufika katika jimbo la Iliriko nimehubiri fasi zote Habari Njema ya Kristo.

20Nayo nia moja niliyokuwa nayo ni kuhubiri tu Habari Njema fasi zote ambapo habari za Kristo zilipokuwa hazijasikilika bado. Nilikusudia vile kusudi nisijenge juu ya musingi uliowekwa na mutu mwingine,

21kama vile inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu:

“Wale ambao hawajaambiwa bado habari zake, watamwona.

Wale hawajazielezwa bado, watazifahamu.”

Paulo anakusudia kufika Roma

22Hiyo ndiyo sababu iliyonizuiza mara nyingi kufika kule kwenu.

23Lakini kwa sasa nimemaliza kazi yangu katika pande hizi za inchi, na tena tangu miaka mingi nina hamu sana ya kuja kuwaona;

24kwa hiyo nitawafikia nitakapokwenda Spania. Ninatumaini kupitia kule na kuonana nanyi, na kisha kufurahi kwanza pamoja nanyi kwa muda mufupi, ningetamani kupata musaada wenu kwa ajili ya safari ile.

25Lakini sasa ninakwenda kwanza Yerusalema kuwasaidia watu wa Mungu kule.

26Kwa maana imependeza makanisa ya Makedonia na ya Akaya kukusanya mali kwa kuwasaidia wamasikini wanaokuwa kati ya watu wa Mungu kule Yerusalema.

27Ndiyo wamefanya vile kwa mapenzi yao, lakini vilevile ilikuwa mapaswa kwao kuwasaidia. Kwa maana ikiwa watu wa mataifa wameshirikiana baraka za kiroho na Wayuda, imewapasa watu wa mataifa mengine kuwasaidia Wayuda katika mahitaji ya kimwili.

28Basi nitakapomaliza kazi ile na kuwafikishia mali iliyokusanywa, nitapitia kwenu, nikiwa katika safari yangu ya kwenda Spania.

29Nami ninajua kwamba wakati nitakapokuja kwenu, nitakuja na baraka nyingi sana kutoka kwa Kristo.

30Wandugu zangu, ninawasihi kwa ajili ya Bwana wetu Yesu Kristo na kwa ajili ya upendo unaoletwa na Roho wa Mungu, muungane nami kwa kuniombea kwa Mungu.

31Muniombee kusudi nisipate hasara toka kwa watu wale wasioamini wanaokuwa Yudea na kusudi musaada ninaoupeleka Yerusalema upate kupokelewa vizuri kule na watu wa Mungu.

32Na hivi Mungu akitaka, nitakuja kwenu kwa furaha, nami nitapata kutulizwa moyo kati yenu.

33Basi Mungu anayeleta amani akuwe pamoja nanyi wote. Amina!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help