1 Petro 1 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Salamu

1Barua hii inatoka kwangu mimi Petro, mutume wa Yesu Kristo. Ninawaandikia ninyi muliochaguliwa na Mungu na ambao mulisambazwa, na munaoishi kama wakimbizi kule Ponto, Galatia, Kapadokia, Azia na Bitinia.

2Mungu Baba aliwachagua ninyi tangu mbele kufuatana na mupango wake na kufanywa watakatifu na Roho, mupate kumutii Yesu Kristo na kusafishwa kwa damu yake. Ninawatakia neema na amani kwa uwingi.

Tumaini lenye uzima

3Tumusifu Mungu, Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo! Kwa huruma yake kubwa ametupatia uzima mupya kwa njia ya kumufufua Yesu Kristo. Na kwa hiyo tumepata tumaini lenye uzima,

4na hivyo tutapata baraka zile ambazo Mungu aliwawekea watu wake. Baraka zisizoweza kuoza wala kuchafuka wala kupunguka; nazo zinawekewa akiba kwa ajili yenu mbinguni.

5Ninyi ambao kwa imani munalindwa salama kwa nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu ambao uko tayari kufunuliwa kwa mwisho wa nyakati.

6Katika mambo hayo yote mushangilie kwa furaha ijapokuwa inawapasa sasa kuhuzunika kwa wakati kidogo kwa ajili ya majaribu ya namna mbalimbali.

7Majaribu hayo ni kwa ajili ya kupima imani yenu. Zahabu ni kitu kinachoharibika, lakini ingawa vile inapimwa kwa njia ya kuchomwa ndani ya moto. Hivi vilevile imani yenu inayokuwa ya bei kali kuliko zahabu, inapaswa kupimwa kusudi ijulikane kuwa ya kweli. Na kwa sababu hii mutapata sifa, utukufu na heshima wakati Yesu Kristo atakapotokea.

8Ninyi munamupenda ijapokuwa hamujamwona, na munamwamini ijapokuwa sasa hamumwoni. Na zaidi ya ile munashangilia kwa furaha isiyoweza kuelezwa, inayojaa utukufu,

9kwa maana munapokea shabaha ya imani yenu, ni kusema wokovu wa roho zenu.

10Manabii walifanya uchunguzi na upelelezi juu ya wokovu ule, nao walitabiri juu ya zawadi ambayo ninyi mungepewa.

11Roho wa Kristo aliyekuwa ndani yao alitangulia kushuhudia mateso yatakayomupata Kristo na utukufu utakaokuwa nyuma. Nao walijitolea kusudi wapate kuvumbua wakati gani na kwa njia gani mambo haya yatafanyika.

12Mungu aliwafunulia wale manabii kwamba ujumbe ule walioutangaza haukuwaelekea wao wenyewe, lakini uliwaelekea ninyi. Na sasa ujumbe ule umetangazwa kwenu na wale waliowahubiri Habari Njema kwa uwezo wa Roho Mutakatifu aliyetumwa toka mbinguni. Hata wamalaika vilevile wanatamani kujua mambo hayo.

Maisha ya utakatifu

13Kwa sababu hiyo, mukuwe tayari kwa kutumikisha akili yenu. Mukeshe na muweke tumaini lenu lote katika baraka ile mutakayopewa wakati Yesu atakapotokea.

14Kama watoto wenye utii, musiachilie maisha yenu kutawaliwa na tamaa mbaya mulizokuwa nazo zamani wakati mulipokuwa mukiishi katika ujinga.

15Na sawa vile Mungu aliyewaita ni mutakatifu, ninyi vilevile munapaswa kuwa watakatifu katika mwenendo wenu wote.

16Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Muwe watakatifu, kwa maana mimi ni mutakatifu.”

17Na ikiwa katika maombi yenu munamwita “Baba” yule anayehukumu kila mutu pasipo upendeleo kufuatana na matendo yake, basi muishi katika heshima mbele yake kwa muda unaowabakilia kwa kuishi hapa katika dunia.

18Kwa maana munajua namna gani mulivyokombolewa toka katika tabia za ovyo ovyo mulizoambukizwa na babu zenu. Hamukukombolewa kwa njia ya vitu vinavyoharibika kama vile feza au zahabu.

19Lakini mulikombolewa kwa njia ya damu yenye bei kali ya Kristo, aliyekuwa kama kondoo asiyekuwa na kilema wala uchafu.

20Yeye ndiye aliyechaguliwa na Mungu mbele ya kuumbwa kwa dunia, na alifunuliwa kwa ajili yenu katika nyakati hizi za mwisho.

21Kwa njia ya Kristo, ninyi munamwamini Mungu aliyemufufua na kumupa utukufu. Na kutokana na hiyo munamwamini Mungu na kumuwekea tumaini lenu.

22Ninyi mumekwisha kutakaswa kwa njia ya kutii neno la kweli kwa kuwapenda wandugu zenu pasipo unafiki. Basi mupendane kabisa, kwa moyo wenu wote.

23Kwa maana mumezaliwa upya, kwa nguvu za neno la Mungu lenye uzima na linalodumu hata milele. Nanyi si kama watoto waliozaliwa na wazazi wenye mwili huu unaokuwa wa kufa, lakini watoto waliozaliwa kwa nguvu ya uzazi usioweza kufa.

24Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema:

“Wanadamu wote ni kama majani.

Na utukufu wao wote unatoweka kama maua.

Majani yanakauka na maua yanaanguka.

25Lakini Neno la Bwana linadumu hata milele.”

Na Neno hili ni Habari Njema iliyohubiriwa kwenu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help