1Katika mwaka wa ine wa utawala wa mufalme Yoyakimu mwana wa Yosia, juu ya inchi ya Yuda, Yawe alimupa Yeremia ujumbe juu ya watu wa Yuda. Mwaka huo ulikuwa wa kwanza wa utawala wa Nebukadneza mufalme wa Babeli.
2Yeremia akawaambia ujumbe huo watu wote wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema, akisema:
3Kwa muda wa miaka makumi mbili na tatu sasa, ni kusema tangu mwaka wa kumi na tatu wa utawala wa mufalme Yosia, mufalme wa Yuda, mwana wa Amoni, mpaka hivi leo, nimekuwa nikipata neno la Mungu na kulitoa kwenu kila wakati, lakini ninyi hamukusikiliza.
4Hamukutaka kusikiliza wala kutega sikio, ingawa Yawe aliwaletea watumishi wake manabii kila wakati.
5Wao waliwaambia hivi: Kila mumoja wenu aachane na mwenendo wake mwovu na matendo yake mabaya, kusudi mupate kuishi katika inchi ambayo Yawe amewapa ninyi na babu zenu tangu zamani kuwa urizi wenu milele.
6Musifuate miungu mingine wala kuitumikia na kumukasirikisha kwa kuabudu sanamu, nami sitawatendea ubaya wowote.
7Lakini mulikataa kunisikiliza. Na kisha, mulinikasirikisha na sanamu mulizojitengenezea wenyewe, na kwa hiyo mukajiletea hasara ninyi wenyewe.
–Ni ujumbe wa Yawe.
8Kwa hiyo Yawe wa majeshi anasema hivi: Kwa sababu hamukuyatii maneno yangu,
9basi, nitayaita makabila yote ya kaskazini pamoja na mutumishi wangu Nebukadneza, mufalme wa Babeli.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
Nitawaleta waishambulie inchi hii na wakaaji wake pamoja na mataifa yote jirani. Nitawaangamiza kabisa, na kuwafanya kuwa kitu cha kuchukiza, cha kuzomewa na kuzarauliwa milele.
10Tena, nitakomesha toka kati yao sauti za furaha, sauti za wenye kufanya ndoa, wala sauti za kusaga hazitasikilika, wala mwangaza wa taa hautaonekana.
11Inchi hii yote itakuwa katika mabomoko matupu na ukiwa, na mataifa jirani yatamutumikia mufalme wa Babeli kwa muda wa miaka makumi saba.
12Hiyo miaka makumi saba itakapopita, nitamwazibu mufalme wa Babeli pamoja na taifa lake. Nitaiangamiza inchi hiyo ya Wababeli.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
Nitafanya hivyo kwa sababu ya uovu wao na kuifanya inchi ibaki mabomoko hata milele.
13Nitaleta juu ya inchi hiyo mambo yote niliyosema juu yake na yote yaliyoandikwa katika kitabu hiki ambayo Yeremia alitabiri juu ya mataifa yote.
14Wababeli nao vilevile watakuwa watumwa wa mataifa mengine na wafalme wengine. Nitawaazibu kwa kadiri ya maovu yao waliyotenda.
Kikombe cha hukumu15Yawe, Mungu wa Israeli, akaniambia hivi: Twaa toka katika mukono wangu kikombe hiki cha divai kinachojaa kasirani yangu uyakunyweshe mataifa yote ninayokutuma kwao.
16Mataifa hayo yatakunywa na yatashikwa na kizunguzungu na kupoteza akili kwa sababu ya mauaji nitakayosababisha kati yao.
17Basi, nikatwaa kikombe hicho toka mukono wa Yawe, nikayakunywesha mataifa yote ambayo Yawe alinituma kwao.
18Kwanza nikakunywesha wakaaji wa Yerusalema na miji mingine ya Yuda, wafalme wake na wakubwa wa serikali yake kusudi ikuwe jangwa, ukiwa, kitu cha kuzomewa na cha kulaaniwa, kama inavyokuwa mpaka leo. Halafu nikakunywesha:
19Mufalme wa Misri, wasimamizi wake na wakubwa wa serikali yake pamoja na watu wake wote;
20wageni wote walioishi katika inchi ya Misri;
wafalme wote wa inchi ya Uzi;
wafalme wote wa miji ya Wafilistini, Askeloni, Gaza, Ekuroni na mabaki ya Asidodi;
21watu wote wa Edomu, Moabu na Amoni;
22wafalme wote wa Tiro na Sidona;
wafalme wa inchi zinazokuwa kandokando ya bahari ya Mediteranea;
23wakaaji wa Dedani, Tema, Buzi na watu wote wanaonyoa nywele zote za pembenipembeni ya kichwa;
24wafalme wote wa Arabia;
wafalme wote wa makabila yanayokaa katika jangwa;
25wafalme wote wa Simuri, Elamu na Medi;
26wafalme wote wa kaskazini, wanaokuwa mbali na karibu, mumoja kisha mwingine.
Hivi nikakunywesha falme zote za ulimwengu. Na kwa mwisho naye mufalme wa Babeli akakunywa.
27Yawe akaniamuru: Utawaambia kwamba:
Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Mukunywe, mulewe na kutapika; muanguke wala musisimame tena, kwa sababu ya mauaji nitakayosababisha kati yenu.
28Kama wakikataa kukipokea kikombe hicho utakachowapatia kwa kunywa, utasema hivi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Ni lazima mukunywe!
29Ikiwa ninaanza kuleta hasara katika muji unaojulikana kwa jina langu, basi ninyi munazani kwamba munaweza kuepuka azabu? Hamutaachwa bila kuazibiwa, maana ninaleta mauaji juu ya wakaaji wote wa dunia.
–Ni ujumbe wa Yawe.
30Basi, wewe Yeremia utatabiri maneno haya yote juu yao, na kusema hivi:
Yawe atanguruma kutoka juu,
atatoa sauti yake kutoka kwenye makao yake matakatifu;
atanguruma kwa nguvu kwa ajili ya watu wake,
atapiga kelele kama wenye kukamua zabibu,
kwa ajili ya wakaaji wote wa dunia.
31Vishindo hivyo vitasikilika mpaka mwisho wa dunia,
maana Yawe ana mashitaki juu ya mataifa;
anawahukumu wanadamu wote,
naye atawaua waovu kwa upanga!
–Ni ujumbe wa Yawe.
32Yawe wa majeshi anasema hivi:
Hasara italifikia taifa kwa taifa,
na zoruba itavuma kutoka miisho ya dunia.
33Siku hiyo, wale watakaouawa na Yawe watasambaa kutoka upande mumoja wa dunia mpaka upande mwingine. Hakuna atakayeomboleza juu yao, wala maiti zao hazitakusanywa wala kuzikwa; zitabaki sawa mboleo juu ya udongo.
34Muomboleze, enyi wachungaji;
mulie na kugaagaa katika majivu, enyi wakubwa wa kundi.
Siku za kuchinjwa kwenu na kusambazwa zinakaribia.
Mutauawa kama kondoo dume wanene.
35Wachungaji hawana makimbilio,
wakubwa wa kundi hawataweza kutoroka.
36Musikilize kilio cha wachungaji
na malalamiko ya wakubwa wa kundi!
Yawe anayaharibu mashamba yao ya malisho.
37Mashamba ya malisho yaliyostawi vizuri yameharibiwa,
kwa sababu ya hasira kali ya Yawe.
38Yawe amewaacha watu wake,
kama vile simba anavyoacha pango lake;
inchi yao imekuwa jangwa tupu,
kwa sababu ya vita
na hasira kali ya Yawe.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.