Esteri 5 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Esteri anawaalika mufalme na Hamani kwa karamu

1Kisha siku tatu ya kufunga kwake, Esteri akavaa nguo zake za kimalkia, akaenda kusimama katika kiwanja cha ndani cha nyumba ya mufalme, kuelekea chumba cha mufalme. Mufalme alikuwa mule ndani akiikaa katika kiti chake cha kifalme, kuelekea mulango wa nyumba ya mufalme.

2Mufalme alipomwona malkia Esteri akisimama katika kiwanja, Esteri akapata kukubaliwa mbele yake, naye akamunyooshea fimbo ya zahabu aliyokuwa akishika katika mukono wake. Esteri akakaribia, akagusa incha ya fimbo.

3Hapo mufalme akauliza: “Unataka nini Esteri? Uniambie unachotaka, nawe utapata – hata kama ni nusu ya ufalme wangu.”

4Esteri akamujibu: “Ikikupendeza, ewe mufalme, ukuje leo pamoja na Hamani, kwenye karamu ninayotayarisha kwa ajili yako, mufalme.”

5Mufalme akatoa amri Hamani akuje upesi, kama vile Esteri alivyoomba. Basi, mufalme na Hamani wakaenda kwenye karamu Esteri aliyotayarisha.

6Walipokuwa wanakunywa divai, mufalme akamwuliza tena Esteri: “Unataka nini? Uniambie, nawe utapata. Ombi lako ni nini? Hata kama ni nusu ya ufalme wangu, utapewa.”

7Esteri akamujibu: “Ombi langu ni hili:

8Kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ewe mufalme, na ikikupendeza kukubali ombi langu, basi, ninaomba wewe na Hamani mukuje kesho kwenye karamu nyingine nitakayowaandalia. Wakati huo nitakujulisha ombi langu.”

Hamani anapanga kumwua Mordekayi

9Hamani akatoka kule kwenye karamu mwenye furaha tele na moyo mukunjufu. Lakini alipomwona Mordekayi kwenye mulango wa nyumba ya kifalme, hasimami wala hamupi heshima, Hamani akawaka hasira.

10Hata hivyo, akajizuia, akaenda kwake. Halafu akawaalika kwake warafiki zake, na kumwomba muke wake Zeresi ajiunge nao.

11Halafu akaanza kueleza juu ya utajiri anaokuwa nao, wana anaokuwa nao, jinsi mufalme alivyomupandisha cheo, na jinsi alivyopewa madaraka zaidi kuliko wakubwa wengine wote wa mufalme.

12Hamani akaendelea kujitapa: “Vilevile malkia Esteri hakumwalika mutu mwingine yeyote pamoja na mufalme isipokuwa mimi tu. Hata kesho tena, ametualika mimi na mufalme.

13Lakini yote haya hayanifalii kitu ikiwa nitaendelea kumwona yule Muyuda Mordekayi kwenye mulango wa nyumba ya kifalme.”

14Basi, muke wake Zeresi na warafiki zake wakamushauria hivi: “Kwa nini asitengenezewe muti wa kutundikia, wenye urefu wa metre makumi mbili na mbili? Kesho asubui, unaweza kuzungumuza na mufalme kusudi Mordekayi auawe juu yake, kisha uende ukule karamu na mufalme kwa furaha.” Wazo hilo lilimufurahisha Hamani, naye akatengeneza muti ule.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help