Isaya 50 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Yawe anasema hivi:

Kama nimeachana na mama yako Yerusalema,

barua ya kuachana iko wapi?

Nilikuwa na deni ya nani kwa kuwauzisha?

Mukumbuke kwamba muliuzishwa kwa ajili ya maovu yenu,

mama yenu alifukuzwa kwa ajili ya makosa yenu.

2Nilipokuja, kwa nini sikukuta mutu?

Nilipoita mbona hamukuitikia?

Mukono wangu ni mufupi hata nisiweze kuwaokoa ninyi?

Sina nguvu ya kuwakomboa?

Ninakausha bahari kwa kuikaripia,

na mito ninaifanya kuwa jangwa;

samaki wake wanakufa na kunuka kwa kukosa maji.

3Mimi ninafunika anga kwa giza,

na kulivalisha nguo ya kilio.

Mutumishi wa Yawe

4Bwana wetu Yawe amenifundisha jinsi ya kusema,

kusudi niwatie moyo wale waliochoka.

Kila asubui ananipa hamu

ya kusikiliza mambo anayotaka kunifundisha.

5Bwana wetu Yawe amenifanya kuwa musikilivu,

nami sikukataa

wala kurudia nyuma.

6Wale walionipiga, niliwaelekezea mugongo wangu,

wale walioziongoa ndevu zangu, mashavu yangu.

Sikuficha uso wangu wakati watu waliponitukana na kunitemea mate.

7Bwana wetu Yawe ananisaidia

kwa hiyo siwezi kufazaika.

Uso wangu nimeukaza kama jiwe;

ninajua kwamba sitapata haya.

8Muteteaji wangu yuko karibu.

Ni nani atakayepingana nami?

Akuje tusambe naye.

Adui yangu ni nani?

Ajitokeze mbele basi.

9Angalia Bwana wetu Yawe ananisaidia.

Ni nani anayeweza kusema niko na kosa?

Waadui zangu wote watachakaa kama nguo,

nondo watawatafuna.

10Nani kati yenu anayemwogopa Yawe?

Nani anayetii maneno ya mutumishi wake?

Kama kuna mutu anayetembea katika giza bila taa,

amutumainie Yawe,

na kumutegemea Mungu wake.

11Lakini ninyi munaowasha moto,

na kujifanyia silaha za mienge,

mutembee kwa mwangaza wa moto huo,

ndimi za moto muliowasha ninyi wenyewe.

Kitu mutakachopata kutoka kwa Yawe ni hiki:

ninyi mutalala chini na mateso makali.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help