Walawi 20 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Azabu kwa ajili ya maovu

1Yawe akamwambia Musa:

2Uwaambie Waisraeli hivi: Mutu yeyote kati ya Waisraeli au mugeni anayekaa kati yenu, akimutoa mutoto wake yeyote kuwa sadaka kwa mungu Moleki, mutu huyu anapaswa kuuawa. Wanainchi wa pale watamwua kwa kumupiga mawe.

3Mimi mwenyewe nitamukasirikia mutu huyu na kumutenga na watu wake kwa sababu alimutoa mumoja wa watoto wake sadaka kwa mungu Moleki na hivyo akachafua Pahali pangu Patakatifu na jina langu takatifu.

4Kama wanainchi wa pahali pale hawatamwazibu mutu yule kwa kumwua,

5mimi mwenyewe nitamukasirikia mutu huyu na jamaa yake. Nitawatenga kutoka watu wao, yeye mwenyewe pamoja na wote waliokosa uaminifu kwangu kwa kumwendea mungu Moleki.

6Kama mutu yeyote anawaendea waaguzi wa mizimu na wachawi na hivyo kukosa uaminifu kwangu, nitamukasirikia mutu huyu na kumutenga na watu wake.

7Kwa hiyo, mujitakase mukuwe watakatifu, maana mimi ni Yawe, Mungu wenu.

8Mushike masharti yangu na kuyatimiza. Mimi ni Yawe ninayewatakasa.

9Mutu yeyote anayemulaani baba yake au mama yake, anapaswa kuuawa. Amemulaani baba au mama yake, kwa hiyo damu yao itakuwa juu yake mwenyewe.

10Kama mwanaume akifanya uzinzi na muke wa mwenzake, wote wawili wanapaswa kuuawa.

11Mwanaume akilala na mumoja wa wake za baba yake, anamupatisha baba yake haya, wote wawili wanapaswa kuuawa. Mwanaume huyo na mwanamuke huyo wote wawili watauawa na damu yao itakuwa juu yao wenyewe.

12Mwanaume yeyote akilala na muke wa mwana wake, wote wawili wanapaswa kuuawa. Wamefanya machafuko na damu yao itakuwa juu yao wenyewe.

13Kama mwanaume yeyote akilala na mwanaume mwenzake sawa vile ni mwanamuke, basi, wote wawili wanapaswa kuuawa maana wamefanya jambo linalokuwa chukizo na damu yao itakuwa juu yao wenyewe.

14Kama mwanaume akioa muke na vilevile kumwoa mama yake, huo ni uovu. Wote watatu wanapaswa kuteketezwa kwa moto maana wamefanya uovu. Mutafanya hivyo kwa kukomesha uovu kati yenu.

15Kama mwanaume yeyote akilala na nyama anapaswa kuuawa na nyama huyo anapaswa kuuawa.

16Kama mwanamuke anakaribia nyama na kulala naye, mwanamuke huyo anapaswa kuuawa na nyama huyo vilevile na damu yao itakuwa juu yao wenyewe.

17Kama mwanaume yeyote akimwoa dada yake, binti ya baba yake au mama yake na binti huyo akakubaliana na mwanaume huyo ambaye ni kaka yake, na kulala naye, hilo ni chukizo. Wanapaswa kutengwa na watu wao maana wamefanya jambo la haya. Huyo mwanaume atabeba lazima ya uovu wake, maana amelala na dada yake.

18Kama mwanaume akilala na mwanamuke anayekuwa na ugonjwa wa mwezi, wote wawili wanapaswa kutengwa na watu wao; huyo mwanaume amelala na mwanamuke aliyekuwa na ugonjwa wa mwezi, na huyo mwanamuke amefunua mutiririko wa damu yake.

19Usilale na dada ya mama yako wala na shangazi yako, maana hao ni jamaa yako wa karibu. Wote wanaotenda vile watabeba lazima ya uovu wao.

20Kama mutu akilala na muke wa baba yake, mukubwa au mudogo, anamupatisha baba yake mukubwa au mudogo haya. Wote wawili watabeba lazima ya zambi yao. Wote wawili watakufa bila watoto.

21Kama mwanaume akimwoa muke wa ndugu yake, anamupatisha ndugu yake haya, huo ni uchafu; wote wawili watakufa bila watoto.

22Munapaswa kushika na kutimiza masharti yangu na maagizo yangu yote. Kama sivyo inchi ile ambamo ninawapeleka itawatapika.

23Musifuate desturi za taifa ninalofukuza mbele yenu. Maana waliyafanya hayo yote, nami nikawachukia sana.

24Lakini, nimekwisha kuwaambia: Mutarizi inchi yao, mimi ninawapa inchi hiyo ikuwe yenu, inchi inayotiririka maziwa na asali. Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatenga na mataifa mengine.

25Kwa hiyo, munapaswa kutia tofauti kati ya nyama asiyekuwa muchafu na anayekuwa muchafu, kati ya ndege asiyekuwa muchafu na anayekuwa muchafu. Musijichafue kwa kugusa nyama au ndege au chochote kinachotambaa juu ya udongo ambacho nimekitenga kuwa ni kichafu.

26Kwa sababu mimi Yawe ni mutakatifu, nami nimewatenga ninyi na mataifa mengine kusudi mukuwe mali yangu, mutakuwa watakatifu.

27Mwanaume au mwanamuke yeyote anayekuwa mulozi au muchawi, anapaswa kuuawa kwa kupigwa mawe. Damu yao itakuwa juu yao wenyewe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help