1 Samweli 24 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Daudi anayahurumia maisha ya Saulo

1Daudi aliondoka pahali pale, akaenda kuishi kwenye makimbilio ya muji wa Engedi.

2Saulo aliporudi kutoka kupigana na Wafilistini, alipata habari kwamba Daudi yuko kwenye mbuga za Engedi.

3Kisha Saulo aliwatwaa waaskari elfu tatu waliochaguliwa waliokuwa bora zaidi katika inchi yote ya Israeli, akaenda kumutafuta Daudi na watu wake pahali panapoitwa “Mawe ya Mbuzi wa Pori.”

4Saulo alipokuwa anasafiri, alifika kwenye pango moja lililokuwa karibu na zizi la kondoo, akaingia mule ndani ya pango kwa kujisaidia. Daudi na watu wake walikuwa wakiikaa ndani kabisa ya pango lile.

5Watu wa Daudi wakamwambia: “Ile siku Yawe aliyokuambia kwamba atakuja kumutia adui yako katika mikono yako nawe umutendee utakavyoona inafaa, leo imefika.”

Halafu Daudi alimwendea Saulo polepole kutoka nyuma, akakata pindo la nguo yake.

6Daudi akaanza kufazaika ndani ya moyo kwa sababu alikata pindo la nguo ya Saulo kwa siri.

7Akawaambia watu wake: “Yawe anizuie nisimutendee kitendo kama hiki bwana wangu ambaye ni muchaguliwa wa Yawe. Nisiunyooshe mukono wangu juu ya mutu ambaye Yawe amemupakaa mafuta.”

8Kwa maneno hayo, Daudi akawashawishi watu wake wasimuzuru Saulo; aliwakataza wasimushambulie. Kisha Saulo akasimama, akatoka ndani ya pango akaendelea na safari yake.

9Kisha, Daudi naye akasimama, akatoka ndani ya pango na kumwita Saulo: “Bwana wangu mufalme!” Mufalme Saulo alipoangalia nyuma, Daudi aliinama mpaka chini, kwa kumuheshimu Saulo.

10Kisha akamwambia: “Kwa nini unawasikiliza watu wanaokuambia: ‘Daudi anataka kukuzuru’?

11Sasa, leo umejionea kwa macho yako mwenyewe. Ulipokuwa ndani ya pango Yawe alikutia katika mikono yangu. Wamoja kati ya watu wangu waliniambia nikuue, lakini nilikuhurumia. Nikasema sitanyoosha mukono wangu juu ya bwana wangu maana yeye ni muchaguliwa wa Yawe.

12Angalia, baba yangu, angalia pindo hili la nguo yako katika mikono yangu. Kwa kulikata pindo la nguo yako bila kukuua, unaweza sasa kujua kwa hakika kwamba mimi si mwovu wala mwasi. Mimi sijatenda zambi juu yako ingawa wewe unaniwinda uniue.

13Yawe aamue kati yangu na wewe. Naye ndiye akulipize kisasi lakini mimi sitanyoosha mukono wangu juu yako hata kidogo.

14Kumbuka mezali ya kale inayosema ‘Uovu unatoka ndani ya mwovu’, lakini sitanyoosha mukono juu yako.

15Sasa wewe mufalme wa Israeli angalia mutu unayetaka kumwua! Unamufuatilia nani? Unafuatilia imbwa yenye kufa! Unakifuatilia kiroboto!

16Basi, Yawe akuwe mwamuzi kati yangu na wewe. Yeye aliangalie jambo hili, anitetee na kuniokoa katika mikono yako.”

17Daudi alipomaliza kusema, Saulo akasema: “Hiyo ni sauti yako mwana wangu Daudi?” Saulo akalia kwa sauti.

18Kisha akamwambia Daudi: “Wewe una haki kuliko mimi; umenilipa mazuri, wakati mimi nimekulipa mabaya.

19Leo, umeonyesha jinsi unavyokuwa muzuri kwangu. Haukuniua ijapokuwa Yawe alinitia katika mikono yako.

20Mutu akimukamata adui yake atamwacha aende salama? Kwa lile ulilonitendea, Yawe akupe zawadi njema!

21Sasa nimejua kwamba hakika utakuwa mufalme wa Israeli, na ufalme wa Israeli utaimarishwa chini yako.

22Lakini uniapie kwa jina la Yawe kwamba hautawateketeza wazao wangu, wala kufuta kabisa jina langu katika jamaa ya baba yangu.”

23Daudi akamwapia Saulo. Kisha Saulo akarudia kwake, lakini Daudi na watu wake wakaenda kwenye nafasi zao za makimbilio.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help