1 Wafalme 21 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maneno ya shamba la Naboti

1Nyuma ya mambo hayo, Naboti wa muji wa Yezereheli alikuwa na shamba lake la mizabibu kule Yezereheli, karibu na nyumba ya Ahabu, mufalme wa Samaria.

2Basi, siku moja, Ahabu akamwambia Naboti: “Unipe shamba lako la mizabibu nilifanye shamba la mboga, kwa sababu liko karibu na nyumba yangu. Nitakupa shamba lingine zuri zaidi, au ukitaka nitakulipa feza sawasawa na bei yake.”

3Lakini, Naboti akamujibu: “Jambo la kukupa wewe urizi nilioupata kwa wazee wangu, Yawe alipitishe mbali.”

4Hapo, Ahabu akarudi kwake akijaa chuki na huzuni nyingi, kwa sababu Naboti wa Yezereheli alimwambia kwamba hatamupa kile alichorizi kutoka kwa wazee wake. Basi, akalala kwenye kitanda, akaficha uso wake na kukataa chakula.

5Yezebeli, muke wake, akamwendea na kumwuliza: “Mbona umejaa huzuni ndani ya moyo hata kula haukuli?”

6Naye akamwambia: “Kwa sababu nilizungumuza na Naboti wa Yezereheli, nikataka aniuzishie shamba lake la mizabibu, au kama akipenda nimupe shamba lingine pahali pa lile. Lakini yeye akaniambia: ‘Sitakupa shamba langu la mizabibu.’ ”

7Hapo, Yezebeli, muke wake, akamwambia: “Anayetawala Israeli ni nani? Si ni wewe? Amuka, ukule na uchangamuke. Mimi peke yangu nitakupa shamba la mizabibu la Naboti wa Yezereheli.”

8Basi, Yezebeli akaandika barua kwa jina la Ahabu na kuzipiga muhuri wa mufalme. Kisha akapeleka barua hizo kwa wazee na watu wenye heshima walioishi na Naboti kule katika muji.

9Barua zenyewe ziliandikwa hivi: “Mutangaze kwa watu kwa kufanya sikukuu ya kufunga kula, mukutane na kumupa Naboti nafasi ya heshima kati ya watu.

10Kisha, mutafute watenda maovu wawili wapate kumushuhudia na kumushitaki wakisema: ‘Wewe umemutukana Mungu na mufalme.’ Kisha mumupeleke inje, mumwue kwa kumutupia mawe!”

11Basi, wakaaji wenzake na Naboti, wazee na watu wenye heshima wa muji wa Yezereheli wakafanya kama vile Yezebeli alivyowaagiza. Kwa kufuatana na barua alizowatumia,

12wakatangaza sikukuu ya kufunga kula, wakakutana na kumuweka Naboti kwenye nafasi ya heshima kati ya watu.

13Wale watenda maovu wawili wakaikaa kwa kumushuhudia Naboti, kisha wakamushitaki mbele ya watu wote wakisema: “Naboti amemutukana Mungu na mufalme.” Basi, Naboti akapelekwa inje ya muji, akauawa kwa kutupiwa mawe.

14Kisha, Yezebeli akapelekewa habari kwamba Naboti amekwisha uawa kwa kutupiwa mawe.

15Mara tu Yezebeli alipopata habari kwamba Naboti amekwisha kufa kwa kutupiwa mawe, akamwambia Ahabu: “Simama! Kwenda utwae lile shamba la mizabibu la Naboti wa Yezereheli ambalo alikataa kukuuzishia. Naboti hayuko muzima tena; amekwisha kufa.”

16Mara tu Ahabu aliposikia kwamba Naboti amekwisha kufa, akasimama na kwenda kulitwaa shamba la mizabibu la Naboti.

Nabii Elia anamukaripia Ahabu

17Basi, neno la Yawe lilimufikia Elia wa Tisibe kusema hivi:

18“Simama uende kukutana na Ahabu mufalme wa Israeli, ambaye yuko Samaria. Utamukuta katika shamba la mizabibu la Naboti kwa kulitwaa.

19Umwambie, Yawe anasema hivi: ‘Umeua na kutwaa mali yake vilevile?’ Umwambie Yawe anasema hivi: ‘Pahali pale imbwa walipoilambulia damu ya Naboti, ndipo watakapoilambulia damu yako.’ ”

20Basi, Ahabu alipomwona Elia, akasema: “Ewe adui yangu, umeninasa tena?”

Elia akamujibu: “Ndiyo! Nimekunasa, kwa sababu wewe umekusudia kabisa kutenda maovu mbele ya Yawe.

21Basi! Yawe anasema hivi: ‘Hakika, nitakuletea maangamizi. Nitakuletea hasa wewe na kuangamiza kila mwanaume wa ukoo wako katika Israeli, akuwe mutumwa au huru.

22Jamaa yako nitaifanya kama jamaa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, na kama jamaa ya Basha mwana wa Ahiya, kwa sababu umeiwasha hasira yangu na kuwasukuma watu wa Israeli watende zambi.’

23Tena, Yawe anasema hivi juu ya Yezebeli: ‘Imbwa wataukula mwili wa Yezebeli humuhumu katika muji wa Yezereheli.

24Hakika, mutu yeyote wa jamaa yake atakayekufia ndani ya muji, imbwa watamukula; na mutu yeyote atakayekufia katika shamba, ndege watamukula.’ ”

25Hakuna mutu aliyekusudia kutenda maovu mbele ya Yawe kama Ahabu, ambaye alishawishiwa na Yezebeli, muke wake.

26Alitenda machukizo kwa kuabudu sanamu za miungu kama vile Waamori walivyofanya ambao zamani Yawe aliwafukuza mbele ya watu wa Israeli.

27Lakini, Ahabu aliposikia maneno hayo, akapasua nguo zake, akavaa gunia peke yake, akafunga, akakuwa analala na gunia, na kwenda huko na huko kwa huzuni.

28Basi, neno la Yawe lilimufikia Elia wa Tisibe kusema hivi:

29“Umeona jinsi Ahabu alivyojinyenyekeza mbele yangu? Basi, kwa sababu amejinyenyekeza, sitaleta yale maangamizi atakapokuwa angali anaishi, lakini nyakati za utawala wa mwana wake nitaiangamiza jamaa ya Ahabu.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help