1Mwanamuke mwenye hekima anajenga nyumba yake, lakini mupumbafu anaibomoa kwa mikono yake mwenyewe.
2Mwenye mwenendo sawa anamwogopa Yawe, lakini mupotovu anamuzarau Mungu.
3Ndani ya kinywa cha mupumbafu kunatokea maneno ya kiburi, lakini mwenye hekima analindwa na maneno yake.
4Bila ngombe wa kulima gala za mutu ni tupu. Mavuno mengi yanapatikana kwa nguvu ya ngombe wa kulima.
5Mushuhuda mwaminifu hasemi uongo, lakini asiyeaminiwa anabubujika uongo.
6Mwenye mazarau anatafuta hekima naye haipati, lakini mwenye akili anapata maarifa kwepesi.
7Ondoka pahali mupumbafu anapokuwa, maana pale anapokuwa hakuna maneno ya hekima.
8Hekima ya mwenye akili inamwonyesha njia yake, lakini upumbafu wa wapumbafu unawadanganya wenyewe.
9Wapumbafu wanafurahia zambi, lakini watu wa usawa wanapata rehema kwa Mungu.
10Moyo unajua uchungu wake wenyewe, wala mugeni hawezi kushiriki furaha yake.
11Nyumba ya mutu mwovu itabomolewa, lakini hema ya watu wa usawa itaimarishwa.
12Kuna njia inayozaniwa kuwa sawa, lakini kwa mwisho inaongoza kwenye kifo.
13Huzuni inaweza kufichwa katika kicheko; nyuma ya furaha kunakuja huzuni.
14Mutu mupotovu atavuna matunda ya mwenendo wake, naye mutu muzuri atapata malipo ya matendo yake.
15Mujinga anaamini kila kitu anachoambiwa, lakini mwenye akili anachunguza hatua zake zote.
16Mwenye hekima ni mwangalifu na anaepuka uovu, lakini mupumbafu hajizuizi wala hana uangalifu.
17Mwenye kuwaka hasira haraka anatenda kipumbafu, lakini mwenye akili ana uvumilivu.
18Wajinga wanarizi upumbafu, lakini wenye akili wanalipwa taji ya maarifa.
19Waovu watapiga magoti mbele ya watu wazuri, watu wabaya kwenye mulango wa wenye haki.
20Masikini anachukiwa hata na jirani yake, lakini tajiri ana warafiki wengi.
21Anayemuzarau jirani yake ni mwenye zambi, lakini ana heri yule anayekuwa mwema kwa masikini.
22Anayepanga kutenda maovu kweli anakosa! Wanaopanga kutenda mazuri watapata mema na uaminifu.
23Bidii katika kila kazi inaleta faida, lakini maneno matupu yanaleta umasikini.
24Mali ni taji ya utukufu wa wenye hekima, lakini ujinga ni kitambaa cha wapumbafu.
25Mushuhuda wa kweli anaokoa maisha, lakini musema uongo ni mudanganyifu.
26Anayemwogopa Yawe ana tumaini imara, na watoto wake watapata kimbilio salama.
27Kumwogopa Yawe ni chemichemi ya uzima inayowezesha mutu kuepuka mitego ya kifo.
28Utukufu wa mufalme ni wingi wa watu wake, lakini bila watu mutawala anaangamia.
29Mutu asiyekuwa mwepesi wa hasira ana akili nyingi, lakini anayekasirika upesi anaongeza upumbafu.
30Amani ndani ya roho inamupa mutu afya, lakini wivu inaozesha mifupa.
31Anayemutesa muzaifu anamutukana Muumba wake, lakini anayemwonea huruma mukosefu anamutukuza Mungu.
32Mwovu anaangamizwa kwa matendo yake maovu, lakini mwenye haki atapata usalama kwa uaminifu wake.
33Hekima iko ndani ya moyo wa mutu mwenye akili, lakini haipatikani hata kidogo ndani ya moyo wa mupumbafu.
34Haki inainua taifa, lakini zambi ni haya kwa taifa lote.
35Mufalme anapendezwa na mutumishi anayetenda kwa hekima, lakini hasira yake inawapata wanaotenda mambo yasiyofaa.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.