Zaburi 53 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mutu asiyemwabudu Mungu

1Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo wa huzuni. Mashairi ya Daudi.

2Mupumbafu anajisemesha hivi katika moyo:

“Hakuna Mungu!”

Wote wamepotoka kabisa,

wametenda mambo ya kuchukiza;

hakuna hata mumoja anayetenda mazuri.

3Mungu anawaangalia wanadamu kutoka mbinguni,

aone kama kuna yeyote mwenye akili

kama kuna yeyote anayemutafuta Mungu.

4Lakini wote wamekosa,

wote wamepotoka pamoja;

hakuna anayetenda mazuri,

hakuna hata mumoja.

5Hao wanaotenda maovu hawajui kitu?

Wanatafuna watu wangu kama mikate;

wala hawajali Mungu.

6Hapo watashikwa na hofu,

hofu ambayo hawajapata kuiona;

maana Mungu ataitawanya mifupa ya waadui,

hao watafezeheka maana Mungu amewakataa.

7Heri ukombozi wa Israeli ungefika kutoka Sayuni!

Mungu atakapotengeneza hali ya watu wake,

wazao wa Yakobo watashangilia;

watu wa Israeli watafurahi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help