Matendo ya Mitume 12 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Katika siku zile mufalme Herode akaanza kutesa watu wamoja wa kanisa.

2Akaamuru Yakobo, ndugu ya Yoane, auawe kwa upanga.

3Basi, alipoona kwamba jambo lile liliwapendeza Wayuda, akaamuru Petro afungwe vilevile. (Mambo haya yalitokea kwa wakati wa sikukuu ya Mukate Usiotiwa Chachu.)

4Alipokwisha kumukamata Petro, na kumutia katika kifungo, akamuweka chini ya ulinzi wa vikundi vine vya waaskari waliogomboana wane kwa wane. Naye alikusudia kumusambisha mbele ya watu nyuma ya sikukuu ya Pasaka.

5Basi Petro akabaki akichungwa katika kifungo, lakini kanisa likaendelea kumwombea kwa Mungu pasipo kuchoka.

Petro anafunguliwa

6Usiku, mbele ya kutimia kwa siku Herode aliyotaka kumusambisha mbele ya watu, Petro alikuwa amelala ndani ya chumba katikati ya waaskari wawili. Alikuwa amefungwa na minyororo miwili, nao walinzi walikuwa wakichunga mulango wa kifungo.

7Kwa rafla malaika wa Bwana akatokea na mwangaza ukajaa ndani ya chumba kile. Malaika akamutikisa Petro na kumwamusha, akimwambia: “Simama upesi!”

Nayo minyororo ikaanguka toka kwenye mikono yake.

8Kisha malaika akamwambia: “Funga mukaba na uvae viatu vyako.”

Petro akafanya vile, naye malaika akamwambia tena: “Vaa koti yako na kunifuata.”

9Petro akamufuata mpaka inje ya kifungo. Lakini hakutambua kwamba mambo yale malaika aliyofanya yalikuwa ya kweli; alizani kwamba amepata maono.

10Wakapita kikundi cha kwanza cha waaskari na cha pili, na kufikia kwenye mulango wa chuma wa kuingilia ndani ya muji. Ule mulango ukajifungua wenyewe mbele yao, nao wakatoka inje na kuendelea katika barabara moja. Na kwa rafla yule malaika akamwacha.

11Petro alipotambua kwamba mambo yaliyotokea ni ya kweli akasema: “Sasa ninajua hakika kwamba Bwana alimutuma malaika wake kuniokoa katika mikono ya Herode na katika mabaya yote Wayuda waliotaka kunitendea.”

12Alipokwisha kufahamu mambo yale yaliyotokea, akaenda kwa Maria, mama ya Yoane aliyeitwa Marko. Watu wengi walikuwa wamekusanyika mule, wakiomba.

13Petro alipiga hodi kwenye mulango wa inje, mujakazi mumoja aliyeitwa Roda akakuja kwenye mulango.

14Naye akatambua sauti ya Petro akafurahi sana hata kwa pahali pa kufungua mulango akarudi mbio kuwapasha wengine kwamba Petro anasimama mbele ya mulango.

15Nao wakamwambia: “Uko na wazimu!”

Lakini akakaza kusema kwamba ni kweli. Basi wakasema: “Ni malaika wake.”

16Kwa wakati ule Petro akaendelea tu kupiga hodi. Walipofungua mulango wakamwona, na kushangaa.

17Naye akawanyamazisha kwa kunyoosha mukono, kuwaelezea namna Bwana alivyomwondoa katika kifungo. Akawaambia tena: “Muwaelezee Yakobo na wandugu wengine waamini habari hizi.”

Kisha Petro akaondoka na kwenda nafasi ingine.

18Kulipokucha, waaskari wakapigwa na hofu sana. Wakaanza kuulizana: “Jambo gani lililomupata Petro?”

19Herode akaomba wamutafute, lakini hawakumwona. Kwa hiyo kisha kusambisha wale walinzi, akaamuru wauawe. Halafu Herode akaondoka Yudea kwenda katika muji Kaisaria na kukaa kule kwa muda.

Kufa kwa Herode

20Herode alikuwa amechunga hasira sana juu ya watu wa muji Tiro na wa Sidona. Lakini wakapatana kwa nia moja kwa kumwendea. Kwanza wakasikilizana na Balasto, aliyekuwa musimamizi wa nyumba ya mufalme. Kisha wakaomba mapatano ya amani kwa mufalme Herode, kwa sababu inchi yao ilitegemea inchi ya mufalme huyo kwa kupata chakula.

21Halafu kwa siku ile iliyopangwa, Herode akavaa nguo zake za kifalme, akaikaa katika kiti chake cha kifalme na kuwatolea watu hotuba.

22Nao watu wakalalamika wakisema: “Hii ni sauti ya Mungu, wala si ya mutu.”

23Na pale pale malaika wa Bwana akamwazibu Herode kwa ugonjwa kwa sababu alijitukuza kwa pahali pa Mungu. Herode akakuliwa na michango ya tumbo na kisha akakufa.

24Lakini Neno la Mungu likaendelea mbele na kuenea fasi nyingi.

25Barnaba na Saulo walipomaliza kazi yao, wakarudi toka Yerusalema, wakiwa pamoja na Yoane, aliyeitwa vilevile Marko.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help