Yeremia 38 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yeremia ndani ya kisima

1Sefatia mwana wa Matani, Gedalia mwana wa Pashuri, na Yukali mwana wa Selemia, pamoja na Pushuri mwana wa Malkia walisikia maneno ambayo Yeremia aliwatangazia watu wote akisema:

2Yawe anasema hivi: Yeyote atakayebaki katika muji huu atakufa kwa vita, njaa na ugonjwa mukali; lakini yule atakayeondoka na kujitoa kwa Wakaldea, ataishi. Maisha yake yatatekwa naye ataishi.

3Yawe anasema hivi: Hakika muji huu utatiwa katika mikono ya waaskari wa mufalme wa Babeli na kutekwa.

4Wakubwa wakamwambia mufalme: Inafaa mutu huyu auawe kwa maana anawavunja moyo waaskari ambao wameachwa katika muji huu na watu wote kwa jumla, kwa kusema maneno kama hayo. Yeye hawatakii watu hawa mema lakini mabaya.

5Mufalme Zedekia akasema: Basi! Mutu huyu yuko katika mikono yenu; mimi siwezi kuwapinga.

6Basi, wakamutwaa Yeremia wakamutia katika kisima cha Malkia mwana wa mufalme ambacho kilikuwa katika kiwanja cha walinzi. Walimushusha Yeremia ndani kwa kamba. Ndani ya kisima hicho hamukukuwa maji lakini matope, naye Yeremia akazama katika matope.

7Lakini Ebedimeleki, towashi Mwetiopia aliyetumika katika nyumba ya kifalme, alipata habari kwamba walikuwa wamemutia Yeremia katika kisima. Wakati huo mufalme alikuwa anafanya baraza kwenye mulango wa Benjamina.

8Basi, Ebedimeleki akamwendea mufalme, akamwambia:

9Bwana wangu mufalme, watu hawa wamefanya kitu kibaya. Wamemutia yule nabii Yeremia katika kisima ambamo kwa kweli atakufa kwa njaa, kwa maana hakuna chakula tena katika muji.

10Halafu mufalme akamwamuru yule Mwetiopia Ebedimeleki hivi: Twaa watu watatu kutoka hapa uende umutoe nabii Yeremia katika kisima, mbele hajakufa.

11Basi, Ebedimeleki akatwaa watu hao na kwenda pamoja nao katika nyumba ya kifalme, wakaingia katika gala ya nyumba ya kifalme; Ebedimeleki akatwaa nguo zilizopasukapasuka na kuchakaa, akaziteremushia Yeremia ndani ya kisima kwa kamba.

12Kisha yule Mwetiopia Ebedimeleki akamwambia Yeremia: Weka nguo hizo katika makwapa yako, kisha upitishe kamba hizo chini ya nguo hizo. Yeremia akafanya hivyo.

13Kisha wakamukokota Yeremia kwa kamba, wakamutosha ndani ya kisima. Kisha hayo, Yeremia akaendelea kukaa katika chumba cha walinzi.

Zedekia anaomba shauri kwa Yeremia

14Wakati fulani mufalme Zedekia alitaka kumwona nabii Yeremia. Basi, akaagiza Yeremia aletwe kwenye mulango wa tatu wa nyumba ya Yawe. Huko, mufalme alimwambia Yeremia: Ninataka kukuuliza jambo fulani; usinifiche kitu chochote.

15Yeremia akamujibu Zedekia: Nikikuambia ukweli hautaniua? Na kama nikikushauria, hautanisikiliza.

16Halafu, mufalme Zedekia alimwapia Yeremia kwa siri akisema: Kama vile Yawe, yule aliyetupatia uzima, anavyoishi, sitakuua wala sitakutia katika mikono ya hawa wanaotaka kukuua.

17Hapo Yeremia akamwambia Zedekia: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kama ukijitoa mwenyewe na kujitia katika mikono ya wakubwa wa mufalme wa Babeli, utayaokoa maisha yako na muji hautateketezwa kwa moto; nawe pamoja na jamaa yako mutaendelea kuishi.

18Lakini usipojitoa mwenyewe na kujitia katika mikono ya wakubwa wa mufalme wa Babeli, basi, muji huu utatekwa na Wakaldea nao watauteketeza kwa moto, nawe hautaweza kujiepusha toka katika mikono yao.

19Mufalme Zedekia akamwambia Yeremia: Ninawaogopa Wayuda waliokimbilia kwa Wakaldea. Labda nitatolewa kwao, wanitese.

20Yeremia akamujibu: Hautatolewa kwao. Wewe sasa utii kile Yawe anachosema, kama ninavyokuambia, na mambo yote yatakuendekea vema, na maisha yako yataokolewa.

21Lakini kama ukikataa kujitoa mwenyewe na kujitia katika mikono yao, haya ndiyo maono ambayo Yawe amenionyesha.

22Katika maono hayo, niliona wanawake waliobaki katika nyumba ya kifalme ya mufalme wa Yuda wakipelekwa kwa wakubwa wa mufalme wa Babeli, nao walikuwa wakisema hivi:

Warafiki zako uliowaaminia wamekudanganya,

nao wamekushinda.

Miguu yako imezama ndani ya matope,

nao wanakugeuka na kukuacha.

23Wake wako wote na watoto wako watapelekwa kwa Wakaldea, nawe mwenyewe hautaponyoka. Utakamatwa mateka na mufalme wa Babeli na muji huu utateketezwa kwa moto.

24Zedekia akamwambia Yeremia: Mutu yeyote asijue habari hizi, nawe hautauawa.

25Kama wakubwa wakisikia kwamba nimeongea nawe, kisha wakikuja na kukuambia: Basi utuambie, ulizungumuza nini na mufalme. Usitufiche chochote nasi hatutakuua;

26wewe utawaambia hivi: Nilikuwa ninamusihi mufalme kwa unyenyekevu asinirudishe katika kifungo ndani ya nyumba ya Yonatani, nisikuje kukufia huko.

27Kisha, wakubwa walimufikia Yeremia wakamwuliza mambo hayo, naye akawajibu kama vile mufalme alivyomwelekeza. Halafu waliacha kuzungumuza naye kwa sababu hakuna mutu aliyekuwa amesikia mazungumuzo yake na mufalme.

28Yeremia alibaki katika chumba cha walinzi mpaka siku muji Yerusalema ulipotekwa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help