1Musikilize! Hekima inaita!
Akili inapiga kelele yake!
2Juu kwenye vilima karibu na njia
na katika masanganjia ndipo ilipojiweka.
3Karibu na milango ya kuingilia katika muji,
pahali wanapoingilia watu inaita kwa sauti:
4“Enyi watu wote, ninawaita ninyi!
Wito wangu ni kwa ajili ya wanadamu.
5Enyi wajinga, mujifunze kuwa na akili;
musikilize kwa uangalifu, enyi wapumbafu.
6Musikilize maana nitakachosema ni jambo la lazima;
katika midomo yangu mutatoka mambo ya haki.
7Kinywa changu kitasema kweli mutupu;
uovu ni chukizo katika midomo yangu.
8Kinywa changu kitasema maneno ya haki,
hakuna udanganyifu wala upotevu katika midomo yangu.
9Kwa mutu mwenye ufahamu kila kitu ni wazi,
kwa mwenye maarifa yote imesawanishwa.
10Chagua mafundisho yangu pahali pa feza;
na maarifa pahali pa zahabu safi.
11“Hekima ina maana sana kuliko mawe ya bei kali;
kitu chochote unachotamani hakiwezi kulingana nayo.
12Mimi Hekima nina ujuzi;
nina maarifa na akili.
13Kumwogopa Yawe ni kuchukia uovu.
Ninachukia kiburi, majivuno maisha mabaya,
na luga mbaya.
14Nina uwezo wa kushauri na kuamua vizuri.
Nina ufahamu na nina nguvu.
15Kwa musaada wangu watawala wanatawala
na wakubwa wanaagiza kwa haki.
16Kwa musaada wangu viongozi wanaongoza
na wakubwa wanaamua.
17Ninawapenda wale wanaonipenda;
wanaonitafuta kwa bidii wananipata.
18Utajiri na heshima viko kwangu,
mali ya kudumu na fanaka.
19Matunda yangu ni mazuri kuliko zahabu safi,
na faida yangu inashinda ya feza bora.
20Ninatembea katika njia ya haki;
ninafuata sheria ya Mungu.
21Ninawatajirisha wale wanaonipenda,
ninajaza tele hazina za wanaonipenda.
22“Yawe aliniumba kwa mwanzo wa kazi yake,
zamani za kale mbele ya kuumbwa kwa kitu chochote.
23Nilifanywa kwa mwanzo wa nyakati,
nilikuwa niko mbele ya dunia kuanza.
24Nilizaliwa mbele ya vilindi vya bahari,
mbele ya chemichemi zinazobubujika maji.
25Nilizaliwa mbele milima na vilima havijaumbwa,
26mbele Mungu hajaumba dunia na mashamba yake,
wala chembe za kwanza za mavumbi ya dunia.
27Nilikuwa niko wakati alipoweka mbingu,
wakati alipofanya muviringo juu ya bahari;
28wakati alipoimarisha mawingu mbinguni,
alipofanya imara chemichemi za bahari,
29wakati alipowekea bahari mupaka wake kusudi maji yake yasipate kuvunja amri yake,
wakati alipoweka misingi ya dunia.
30Nilikuwa pamoja naye kama fundi wa kazi,
nilikuwa furaha yake kila siku,
nikishangilia mbele yake siku zote,
31nikifurahia dunia na wakaaji wake,
na kupendezwa kuwa pamoja na wanadamu.
32“Sasa basi, wana wangu, munisikilize:
heri wale wanaofuata njia zangu.
33Musikilize mafundisho mupate hekima,
wala musiyakatae.
34Heri mutu anayenisikiliza,
anayeikaa kila siku kwenye mulango wangu,
anayekesha karibu na milango yangu.
35Anayenipata mimi amepata uzima,
na upendeleo kutoka kwa Yawe.
36Asiyenipata anajizuru mwenyewe;
wote wanaonichukia wanapenda kifo.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.