1Solomono alijijengea nyumba ya kifalme, naye alitumia muda wa miaka kumi na mitatu kwa kuimaliza.
2Kisha, akajenga jengo lililoitwa Nyumba ya pori ya Lebanoni. Urefu wake ulikuwa metre makumi ine na ine na nusu, upana wake metre makumi mbili na mbili na sentimetre makumi mbili na tano, na urefu wake wa kwenda juu metre kumi na tatu na nusu. Ilikuwa imejengwa juu ya mistari mitatu ya nguzo za mierezi, nguzo ambazo zilishikilia boriti za mierezi kwa upande wa juu.
3Kila mustari ulikuwa na nguzo kumi na tano; basi zote pamoja zilikuwa nguzo makumi ine na tano. Vyumba vilivyojengwa juu ya nguzo hizo, alivitilia dari ya mbao za mierezi.
4Kulikuwa mistari mitatu ya madirisha yaliyoelekeana.
5Milango yote ilikuwa ya muraba, na miimo ya madirisha hayo yaliyoelekeana ilikuwa ya muraba vilevile.
6Alijenga uwanja wa nguzo, ambao urefu wake ulikuwa metre makumi mbili na mbili na sentimetre makumi mbili na tano, na upana wake metre kumi na tatu na nusu. Kwenye sehemu ya mbele ya jengo hilo kulikuwa baraza. Mbele ya baraza kulikuwa nguzo; na mbele ya nguzo kulitokeza paa dogo.
7Solomono alijenga uwanja wa kiti cha kifalme ambamo aliamulia maneno ya watu. Huu uliitwa vilevile Uwanja wa Hukumu. Ulipambwa kwa mbao za mierezi kutoka sakafu mpaka dari.
8Nyumba yake ya kukaa mwenyewe iliyokuwa nyuma ya Uwanja wa Hukumu. Ilijengwa kama zile zingine. Solomono alijenga vilevile nyumba kama uwanja huo kwa ajili ya binti ya mufalme wa Misri, ambaye alikuwa amemwoa.
9Majengo hayo yote yalijengwa kwa mawe ya bei kali kutoka musingi mpaka juu, mawe ambayo yalikuwa yamechongwa kwa vipimo vilivyoamuriwa, na kukatwa kwa musumeno upande wa ndani na wa inje.
10Musingi ulikuwa wa mawe ya bei kali na makubwa yenye urefu wa metre tatu na nusu, na upana metre ine na nusu.
11Sehemu za juu zilijengwa kwa mawe mengine yaliyochongwa kwa vipimo vilivyoamuriwa, na kwa mbao za mierezi.
12Kiwanja cha nyumba ya mufalme kilikuwa na kuta zenye mustari moja wa mbao za mierezi na mistari mitatu ya mawe ya kuchongwa kila moja; ndivyo ilivyokuwa hata kwa kiwanja cha ndani cha nyumba ya Yawe na kwa baraza la nyumba.
Kazi za Hiramu13Kisha mufalme Solomono alimwita Hiramu kutoka Tiro.
14Huyo alikuwa mwana wa mujane wa kabila la Nafutali, na baba yake alikuwa mukaaji wa Tiro, mufua-shaba. Hiramu alikuwa na hekima nyingi na akili, fundi kabisa wa kazi yoyote ya shaba. Basi, alikuja kwa mufalme Solomono, akamufanyia kazi yake yote.
Nguzo mbili za shaba za hekalu(2 Sik 3.15-17)15Hiramu alitengeneza nguzo mbili za shaba, kila moja ikiwa na urefu wa metre ine, na muzunguko wa metre tano na nusu. Ndani zilikuwa na tundu ambalo unene wa pande zake ulikuwa sentimetre mbili.
16Halafu akatengeneza taji mbili za shaba, kila moja ikiwa na urefu wa kwenda juu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano. Akaziweka juu ya nguzo hizo.
17Halafu, alifuma nyavu mbili zenye mapambo ya murabamuraba, akatengeneza taji kwa kusokota mukufu: vyote hivyo kwa ajili ya kupamba taji za shaba zilizowekwa juu ya zile nguzo.
18Vilevile, alitengeneza matunda aina ya makomamanga, akayapanga kwa mistari miwili kuzunguka zile taji juu ya kila nguzo.
19Na taji hizo zilizokuwa juu ya nguzo mbele ya baraza, zilipambwa kwa mufano wa maua ya yungiyungi, urefu wa kwenda juu metre moja na sentimetre makumi munane.
20Taji hizo zilikuwa juu ya hizo nguzo mbili, na vilevile zilikuwa juu ya sehemu ya muviringo iliyojitokeza karibu na zile nyavu. Kulikuwa mifano mia ine ya matunda ya makomamanga, imepangwa kwa mistari miwili kuzunguka kila taji.
21Hiramu aliziweka nguzo hizo kwenye baraza ya hekalu; nguzo aliyoisimika upande wa kusini iliitwa Yakini, na ile aliyoisimika upande wa kaskazini iliitwa Boazi.
22Vichwa vya nguzo hizo vilipambwa kwa mufano wa maua ya yungiyungi. Na hivyo kazi ya kutengeneza nguzo ikamalizika.
Birika la shaba(2 Sik 4.2-5)23Hiramu alitengeneza birika la maji la muviringo lenye upana wa metre ine na nusu kutoka ukingo mpaka ukingo, na urefu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na muzunguko wa metre kumi na tatu na nusu.
24Chini ya ukingo wake, kulizunguka birika hilo, kulikuwa mistari miwili ya vibuyu, kila kimoja metre kumi na tatu na nusu. Vibuyu hivyo vilikuwa vimetengenezwa wakati uleule birika lile lilipofanywa.
25Nalo birika lilikuwa limewekwa juu ya sanamu za ngombe dume kumi na wawili; tatu zikielekea upande wa kaskazini, tatu zikielekea upande wa magaribi, tatu kusini, na nyingine tatu mashariki. Birika liliwekwa juu ya ngombe dume hao, sehemu zao za nyuma zikiwa ndani.
26Unene wa ukingo wake ulikuwa sentimetre saba na nusu; nao ulikuwa ukifanana na ukingo wa kikombe na kama ua la yungiyungi. Birika liliweza kujaa maji kadiri ya litre elfu makumi ine.
Magari ya shaba27Hiramu alitengeneza vilevile magari kumi ya shaba, kila gari likiwa na urefu wa metre moja na sentimetre makumi nane, upana wa metre moja na sentimetre makumi nane, na urefu wa kwenda juu metre moja na sentimetre makumi mbili.
28Magari hayo yalikuwa yameundwa hivi: kulikuwa vibandiko vya chuma ambavyo vilikuwa vimeshikiliwa na mitalimbo. Juu ya vibandiko vile vilivyoshikiliwa na mitalimbo,
29kulikuwa sanamu za simba, ngombe dume na makerubi. Sanamu hizo za simba na ngombe dume, zilikuwa zimefunikwa na kutandikwa juu ya mapambo yaliyosokotwa vizuri.
30Kila gari lilikuwa na magurudumu mane ya shaba, na vyuma vya katikati vya kuyashika magurudumu hayo, vilikuwa vya shaba. Kwenye pembe ine za gari kulikuwa vikingio vya shaba kwa ajili ya birika kubwa. Karibu ya kila kikingio kuliwekwa mapambo ya maua ya kusokotwa.
31Mulango wa gari ulikuwa katika sehemu iliyotokeza juu kwa kipimo cha nusu metre. Kwa inje, mulango ulikuwa umetiwa michoro; na vibandiko vyake vilikuwa vya muraba, si ya muviringo.
32Na hayo magurudumu mane yalikuwa chini ya vile vibandiko; vyuma vya katikati kwa kushika magurudumu hayo vilikuwa vimeunganishwa na majengo ya gari lenyewe; na urefu wa kwenda juu wa magurudumu hayo ulikuwa sentimetre makumi saba na tano.
33Hayo magurudumu yalikuwa kama magurudumu ya magari ya vita; na vyuma vyake vya katikati, kingo zake za miviringo, sambo zake na vyuma vya ndani: hivyo vyote vilikuwa vya shaba iliyoyeyushwa.
34Chini ya kila gari kulikuwa vikingio vine kwenye pembe zake, navyo vilifungamana na gari.
35Na juu ya kila gari kulikuwa muviringo wa sentimetre makumi mbili na tano kwenda juu; na vikingio na vibandiko vilivyokuwa upande wa juu vilishikamana na gari lenyewe.
36Kwenye nafasi wazi iliyopatikana katika vikingio na vibandiko vya kila gari, Hiramu alichonga michoro ya makerubi, simba na miti ya ngazi, akazungusha mashada ya mapambo.
37Mifano hiyo yote kumi ya magari ilifanana, ikiwa na kimo kimoja na umbo lilelile.
38Hiramu alitengeneza vilevile mabeseni kumi ya shaba, moja kwa kila gari. Kila beseni ilikuwa na upana wa metre moja na sentimetre makumi ine na tano, na iliweza kujaa maji kadiri ya litre elfu moja na mia sita.
39Akaweka magari matano upande wa kusini wa nyumba, na matano upande wa kaskazini; na birika akaliweka kwenye pembe ya kusini-mashariki ya nyumba.
Vifaa vya hekalu(2 Sik 4.11–5.1)40-45Hiramu alitengeneza vilevile vyungu, kanya na mabakuli. Basi, Hiramu akamaliza kazi aliyoamuriwa na mufalme Solomono juu ya nyumba ya Yawe:
nguzo mbili,
mabakuli mawili ya taji zilizowekwa juu ya nguzo,
nyavu mbili kwa ajili ya kufunika hizo taji mbili,
mifano ya makomamanga mia ine kwa ajili ya nyavu hizo mbili, mistari miwili ya makomamanga kwa kila wavu kwa kupamba zile taji mbili zilizokuwa juu ya nguzo,
magari kumi,
vikingio kumi katika magari hayo,
birika lile moja,
sanamu za ngombe dume kumi na wawili, chini ya hilo birika,
la vyungu vya kuwekea majivu, majembe, na mabeseni.
Vitu hivi vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Yawe ambavyo Hiramu alimutengenezea mufalme Solomono, vilikuwa vya shaba iliyoangarishwa.
46Vitu hivyo vyote mufalme alivitengeneza katika kiwanda cha Yordani, sehemu ya udongo wa mufinyanzi iliyokuwa kati ya Sukoti na Zaretani.
47Solomono hakupima uzito wa vifaa hivi vyote kwa kuwa vilikuwa vingi sana, na kwa sababu uzito wa shaba haukujulikana.
48-50Solomono alitengeneza vifaa vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Yawe:
mazabahu ya zahabu
meza kwa ajili ya mikate ya kuwekwa mbele ya Mungu
–meza ile ilifunikwa na zahabu–
vinara vya taa vilivyowekwa mbele ya Pahali Patakatifu Sana, vitano upande wa kusini na vitano upande wa kaskazini
–vilifunikwa na zahabu safi–
maua
taa
koleo
–vilifunikwa na zahabu–
vikombe
makasi ya kukata tambi za mishumaa
mabakuli
vyetezo vya kuwekea ubani
miko ya kuopoa moto
–vilifunikwa na zahabu safi–
vyuma vya kushika milango ya sehemu ya Pahali Patakatifu Sana
vyuma vya kushika milango ya hekalu
–vilifunikwa na zahabu.
51Basi, mufalme Solomono akamaliza kazi zote zilizoelekea nyumba ya Yawe. Kisha Solomono akaleta mali yote ambayo baba yake Daudi, alikuwa ameitoa kwa Bwana, ni kusema: feza, zahabu na vyombo; akaiweka katika hazina za nyumba ya Yawe.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.