Ufunuo 12 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mwanamuke na nyoka mukubwa

1Kisha kukaonekana kitambulisho kikubwa mbinguni. Kulikuwa mwanamuke aliyekuwa amefunikwa na jua, na mwezi chini kwenye miguu yake. Na juu ya kichwa kulikuwa taji lenye nyota kumi na mbili.

2Mwanamuke yule alikuwa mimba, naye alikuwa akilia kwa sababu ya uchungu na maumivu ya kuzaa.

3Kisha kukaonekana kitambulisho kingine mbinguni. Kulikuwa nyoka mukubwa mwekundu mwenye vichwa saba na pembe kumi. Juu ya kila kichwa kulikuwa taji saba.

4Mukia wake ulikokota sehemu moja ya tatu ya nyota za mbingu na kuzitupa katika dunia. Yule nyoka akasimama mbele ya yule mwanamuke aliyekuwa tayari kuzaa, kusudi amumeze mutoto wakati atakapozaliwa.

5Halafu yule mwanamuke akazaa mutoto mwanaume atakayetawala mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Lakini mutoto yule akanyanyuliwa na kupelekwa kwa Mungu kwenye kiti chake cha kifalme.

6Na yule mwanamuke akakimbilia katika jangwa kwenye nafasi Mungu aliyomutayarishia kusudi apate kulishwa kule kwa muda wa siku elfu moja mia mbili makumi sita.

7Halafu kukatokea vita katika mbingu. Mikaeli na wamalaika zake wakapigana na yule nyoka mukubwa. Naye yule nyoka akapigana nao pamoja na wamalaika zake,

8lakini akashindwa na haikuwezekana tena kwake kukaa mbinguni pamoja na wamalaika zake.

9Basi yule nyoka mukubwa akafukuzwa. Yeye ndiye yule nyoka wa zamani anayeitwa “Mwovu” au “Shetani,” anayedanganya watu wote. Akatupwa katika dunia pamoja na wamalaika zake.

10Kisha nikasikia sauti kubwa kutoka mbinguni, ikisema: “Sasa wokovu, uwezo na ufalme wa Mungu, na mamlaka ya Kristo wake vimefika. Ni vile, kwa yule aliyekuwa akiwashitaki wandugu zetu mbele ya Mungu wetu muchana na usiku ametupwa chini ya mbingu.

11Wandugu zetu wamemushinda kwa nguvu ya damu ya Mwana-Kondoo na kwa njia ya ukweli walioshuhudia. Wao walikubali kutoa maisha yao mpaka kufa.

12Kwa sababu hii, ninyi munaokaa mbinguni, nayo mbingu kwa jumla, mushangilie! Ole kwenu ninyi munaokaa katika dunia na katika bahari kwa maana yule Mwovu ameshuka kwenu, naye anajaa na hasira, kwa sababu anajua kwamba wakati unaomubakilia ni mudogo.”

13Na wakati yule nyoka alipotambua kwamba ametupwa katika dunia, akaanza kumufuatilia yule mwanamuke aliyezaa mutoto mwanaume.

14Lakini yule mwanamuke akapewa mabawa mawili yanayokuwa kama ya tai, kusudi apate kuruka kwenda katika jangwa kwenye nafasi aliyotengenezewa, mbali na yule nyoka. Na kule apate kukulishwa kwa muda wa miaka mitatu na nusu.

15Basi yule nyoka akatokeza maji kwa uwingi ndani ya kinywa chake, nayo yakatelemuka kama muto nyuma ya yule mwanamuke kusudi yapate kumupeleka.

16Lakini udongo ukamusaidia yule mwanamuke; ukabomoka kama vile kinywa na kumeza ule muto uliotoka katika kinywa cha yule nyoka.

17Yule nyoka akamukasirikia yule mwanamuke na kwenda kufanya vita na wazao wake wengine; ndio wale wanaoshika amri za Mungu na kufuata ukweli ulioshuhudiwa na Yesu Kristo.

18Na yule nyoka akasimama kwenye kivuko cha bahari.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help