Yeremia 16 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yeremia anaamuriwa kukaa peke yake

1Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

2Wewe usioe wala kuzaa watoto pahali hapa.

3Maana Yawe anasema hivi juu ya wana na wabinti watakaozaliwa pahali hapa na juu ya wazazi wao:

4Hao watakufa kwa magonjwa makali, na hakuna atakayeomboleza juu yao wala kuwazika. Maiti zao zitabaki kama vile mboleo juu ya udongo. Wataangamia kwa vita na kwa njaa; na maiti zao zitakuwa chakula cha ndege na nyama wa pori.

5Yawe anasema hivi: Usiingie katika nyumba yenye kilio wala usiende kuomboleza wala kuwalilia. Kwa maana sitawapatia watu hawa amani tena. Sitawatendea tena mema wala kuwasikilia huruma.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

6Wote, wakubwa kama vile wadogo, watakufa katika inchi hii; nao hawatazikwa, wala hakuna atakayeomboleza juu yao. Hakuna atakayejikatakata wala kunyolewa upaa kwa ajili ya kifo chao.

7Hakuna atakayechangia chakula na yule aliyekufiwa kwa kumufariji, wala kumupatia kinywaji cha kumufariji kwa ajili ya kukufiwa na mama au baba yake.

8Usiingie katika nyumba watu wanamofanya karamu. Usiikae kula na kunywa pamoja nao.

9Maana Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nitazikomesha kabisa kutoka pahali hapa sauti za furaha na shangwe, nazo nyimbo za wenye kufanya ndoa. Nitayafanya hayo yote katika nyakati zenu, na mutayaona waziwazi.

10Nawe utakapowaambia watu hao maneno haya yote, wao watakuuliza: Kwa nini Yawe amekusudia hasara hii kubwa juu yetu? Tumefanya uovu gani? Tumetenda zambi gani mbele ya Yawe, Mungu wetu?

11Nawe utawajibu hivi: Babu zenu waliniacha. Wakafuata miungu mingine, wakaitumikia na kuiabudu. Waliniacha, wala hawakuzitii sheria zangu.

12Ninyi mumefanya vibaya zaidi kuliko babu zenu, maana kila mumoja wenu ni mwenye moyo mugumu na mwenye nia mbaya, wala hamunisikilizi.

13Kwa hiyo, nitawafukuza toka katika inchi hii na kuwapeleka mpaka kwenye inchi ambayo ninyi wenyewe wala babu zenu hawakuijua. Kule mutaitumikia miungu mingine usiku na muchana, wala sitawasikilia ninyi huruma.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Kurudi kutoka katika uhamisho

14Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo watu hawataapa tena wakisema: Kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyewaondoa Waisraeli kutoka inchi Misri.

15Lakini wataapa wakisema: Kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyewaondoa Waisraeli kutoka katika inchi ya kaskazini na kutoka katika inchi zote ambapo alipowasambaza. Maana, nitawarudisha katika inchi yao niliyowapatia babu zao.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Azabu inayokuja

16Nitaita wavuvi wengi kuja kuwanasa watu hawa. Kisha, nitaita wawindaji wengi kuja kuwawinda juu ya kila mulima, kila kilima na katika mapango ya chini ya mawe.

17Maana, mimi ninayaona matendo yao yote, hakuna hata moja linalofichama mbele yangu. Maovu yao yote ni wazi mbele yangu.

18Nitalipiza kisasi mara mbili zaidi juu ya zambi zao na makosa yao, kwa sababu wameichafua inchi yangu na mizoga ya miungu yao yenye kuchukiza, wameijaza inchi yangu na hayo machukizo yao.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Tumaini la Yeremia

19Ee Yawe!

Wewe ndiwe nguvu yangu na upango wangu;

wewe ni kimbilio langu wakati wa taabu.

Mataifa toka pande zote za dunia yatakufikia na kusema:

Miungu ya babu zetu ilikuwa ya uongo,

ilikuwa ya bure, isiyofaa kitu.

20Mwanadamu anaweza kujitengenezea miungu?

Kweli hiyo si miungu hata kidogo!

21Kwa hiyo, Yawe anasema: Wakati huu nitawafundisha kusudi wapate kutambua waziwazi nguvu zangu na uwezo wangu, nao watajua kwamba jina langu ni Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help