Isaya 14 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kurudi kutoka katika uhamisho

1Yawe atawahurumia tena watu wa Yakobo, atawachagua tena Waisraeli. Atawarudisha katika inchi yao wenyewe, na wageni watakuja na kukaa pamoja na watu wa Yakobo.

2Watu wa mataifa watawasaidia Waisraeli kurudi katika inchi waliyopewa na Yawe. Na hapo watawatumikia Waisraeli kama watumwa. Wale waliowateka sasa watatekwa na Waisraeli, na watawatawala wale waliowatesa.

Mufalme wa Babeli kati ya wafu

3Ewe Israeli, wakati Yawe atakapokufariji nyuma ya mateso, mahangaiko na utumwa uliofanyiwa,

4utaimba wimbo huu wa kumuchekelea mufalme wa Babeli:

Jinsi gani mutesaji alikomeshwa!

Ukali wake umekomeshwa!

5Yawe amelivunja gongo la waovu,

ameivunja fimbo ya kifalme ya watawala,

6ambayo walipiga nayo watu kwa hasira bila kukoma,

na kuwatawala kwa kuwatesa bila huruma.

7Sasa dunia yote ina utulivu na amani,

kila mutu anaimba kwa furaha.

8Miti ya shindano inafurahia kuanguka kwako,

nayo mierezi ya Lebanoni pamoja inasema:

Kwa vile sasa umeangushwa,

hakuna mukata miti atakayekuja juu yetu!

9Kuzimu nako kumechangamuka,

kusudi ya kukupokea wakati utakapokuja.

Kunaiamusha mizimu ikuje kukusalimia

na wote waliokuwa wakubwa wa dunia;

kunawasimamisha kutoka kwenye viti vyao vya kifalme

wote waliokuwa wafalme wa mataifa.

10Wote kwa pamoja watakuambia:

Nawe sasa umekuwa zaifu kama sisi!

Umekuwa kama sisi wenyewe!

11Utukufu wako umeteremushwa kuzimu

pamoja na muziki wa vinubi vyako.

Chini mafunza ndio kitanda chako,

na wadudu ndio blanketi yako!

12Jinsi gani ulivyoporomoshwa toka mbinguni,

wewe uliyekuwa nyota yenye kuangaza kwa mapambazuko.

Jinsi gani ulivyoangushwa chini,

wewe uliyeyashinda mataifa!

13Wewe ulijisemesha ndani ya moyo wako:

Nitapanda mpaka mbinguni;

nitaweka kiti changu juu ya nyota za Mungu,

nitaikaa juu ya mulima pahali miungu wanapokutana,

huko mbali pande za kaskazini.

14Nitapanda juu ya mawingu

nitajifanya kuwa sawa na Mungu Mukubwa.

15Lakini umeporomoshwa mpaka kuzimu;

umeshushwa chini kabisa ndani ya shimo.

16Watakaokuona watakutonolea macho,

watakushangaa wakisema:

Huyu ndiye aliyetetemesha dunia

na kuzitikisa falme,

17aliyegeuza dunia kuwa kama jangwa,

akaangamiza miji yake,

na kukataa kuwafungua wafungwa wake?

18Wafalme wote wa mataifa wamezikwa kwa heshima

kila mumoja ndani ya kaburi lake.

19Lakini wewe umetupwa inje ya kaburi lako,

kama mutoto wa kuchukiza aliyezaliwa mufu,

kama maiti ambayo imekanyagwakanyagwa.

Umelundikiwa maiti za waliouawa kwa upanga,

waliotupwa ndani ya mashimo penye mawe.

20Lakini wewe hautaunganishwa nao katika mazishi,

maana uliiharibu inchi yako,

uliwaua watu wako.

Wazao wa waovu wasahauliwe kabisa!

21Mujitayarishe kuwachinja watoto wake

kwa sababu ya makosa ya baba zao,

wasipate kuamuka na kukamata inchi,

na kuijaza dunia yote miji yao.

Mungu ataangamiza Babeli

22Nitaushambulia muji wa Babeli na kuuangamiza kabisa. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.– Nitaharibu kila kitu, muji wote, watoto na yeyote aliyebaki muzima. –Ni ujumbe wa Yawe.–

23Nitaufanya kuwa makao ya nungunungu, na utakuwa tingitingi ya maji. Nami nitaufagilia mbali kwa ufagio wa maangamizi. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.

Mwisho wa mateso yote

24Yawe wa majeshi ameapa:

Kama nilivyopanga,

ndivyo itakavyokuwa;

kama nilivyokusudia,

ndivyo itakavyokamilika.

25Nitauvunja uwezo wa Waasuria katika inchi yangu;

nitawakanyagakanyaga katika milima yangu.

Nitawaondolea watu wangu nira yao ya unyanganyi,

na muzigo wa mateso yao.

26Huu ndio uamuzi wa Yawe

juu ya dunia yote;

hii ndiyo azabu atakayotoa

juu ya mataifa yote.

27Kama Yawe wa majeshi ameamua,

nani atakayeweza kuvunja uamuzi wake?

Kama anaunyoosha mukono wake kutoa azabu,

ni nani atakayemupinga?

28Mwaka mufalme Ahazi alipokufa, Mungu alitoa ujumbe huu:

29Musishangilie, enyi Wafilistini wote,

kwamba Asuria, fimbo iliyowapiga, imevunjika;

maana, nyoka wa kawaida atazaa nyoka mwenye sumu,

na nyoka mwenye sumu atazaa nyoka mukubwa mwenye kuruka.

30Wazaliwa wa kwanza wa wazaifu watashiba,

na wakosefu watakaa kwa usalama.

Lakini chipukizi wenu nitawaua kwa njaa;

na yeyote kati yenu atakayebaki nitamwua.

31Ulie ewe mulango; ulalamike ewe muji;

tetemeka kwa hofu, ewe inchi yote ya Filistia.

Maana moshi wa waaskari unakuja kutoka kaskazini,

wala hakuna atakayechelewa katika makundi yake.

32Basi watapewa jibu gani wajumbe wa taifa hilo?

Wataambiwa: Yawe ameijenga imara Sayuni,

na wamasikini kati ya watu wake watakimbilia kule.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help