1Samweli akawaambia Waisraeli wote: “Maneno yote muliyoniambia, nimeyasikiliza. Nimemusimika mufalme juu yenu.
2Sasa, munakuwa na mufalme wa kuwaongoza. Kwa upande wangu, mimi ni muzee mwenye imvi, na wana wangu wako pamoja nanyi. Nimekuwa kiongozi wenu tangu nilipokuwa kijana mpaka sasa.
3Niko hapa, na kama nimefanya tendo lolote baya, basi, mutoe ushuhuda mbele ya Yawe na mbele ya mufalme wake muchaguliwa. Nimenyanganya ngombe dume au punda wa mutu yeyote? Nimemugandamiza mutu yeyote? Nimemutesa mutu yeyote? Nimepokea kituliro kwa mutu yeyote kusudi nifunge macho mbele ya matendo yake? Museme nami nitamurudishia kitu chochote kile.”
4Watu wakamujibu: “Haujatudanganya hata kidogo, haujatugandamiza, wala haujakamata kitu chochote kwa mutu.”
5Samweli akajibu: “Yawe ni mushuhuda juu yenu, na mufalme wake muchaguliwa leo ni mushuhuda kuwa mumeniona sina kosa.”
Wao wakajibu: “Yeye ni mushuhuda.”
6Samweli akawaambia: “Yawe ndiye aliyemuchagua Musa na Haruni na kuwaondoa babu zenu katika inchi ya Misri.
7Sasa musimame palepale munapokuwa kusudi mimi na ninyi tuhukumiwe mbele ya Yawe, nami nitawahutubia juu ya matendo yake ya ajabu ambayo aliyatenda kwa kuwaokoa ninyi na babu zenu.
8“Yakobo na jamaa yake walipokwenda Misri, na Wamisri walipowagandamiza, babu zenu walimulilia Yawe. Naye akawatuma Musa na Haruni ambao waliwatoa babu zenu katika inchi ya Misri na kuwafanya mukae katika inchi hii.
9Lakini wao walimusahau Yawe, Mungu wao, naye akawatia katika mikono ya Sisera, jemadari wa waaskari wa muji wa Hazori, na katika mikono ya Wafilistini na katika mikono ya mufalme wa Moabu. Mataifa hayo yalipigana na babu zenu na kuwashinda.
10Babu zenu wakamulilia Yawe, wakisema: ‘Tumefanya zambi kwa sababu tumekuacha wewe Yawe, kwa kutumikia sanamu za mungu Bali na Astaroti. Utuokoe kutoka katika mikono ya waadui zetu, nasi tutakutumikia’.
11Halafu Yawe alimutuma Yerubali, na kisha akamutuma Bedani, kisha Yefuta, na kwa mwisho akanituma mimi Samweli. Kila mumoja wetu aliwaokoa kutoka waadui zenu waliowazunguka, nanyi mukaishi kwa amani.
12Lakini mulipomwona mufalme Nahasi wa Waamoni amekuja kuwashambulia, mukamukataa Yawe ambaye ndiye Mufalme wenu, mukaniambia: ‘Hapana! Mufalme ndiye atakayetutawala’.
13Sasa, mufalme muliyejichagulia ndiye huyu hapa. Mulimwomba Yawe awape mufalme, naye amewapa.
14Kama mukimutii Yawe na kumutumikia na kusikiliza sauti yake bila kuiasi amri yake, kama ninyi wenyewe pamoja na mufalme anayewatawala mukimufuata Yawe, Mungu wenu, basi mutafanikiwa.
15Lakini kama hamutasikiliza sauti ya Yawe, mukiasi amri yake, basi yeye atapambana nanyi pamoja na mufalme wenu.
16Kwa hiyo basi, mutulie na kulitazama jambo hilo kubwa ambalo Yawe atatenda mbele yenu.
17Sasa si wakati wa kuvuna ngano? Lakini mimi nitamwomba Yawe alete radi na mvua, nanyi mutatambua na kuona kwamba uovu wenu muliotenda mbele ya Yawe kwa kujitakia mufalme, ni mukubwa.”
18Basi, Samweli akamwomba Yawe, naye akatuma radi na mvua katika siku hiyo. Watu wote wakamwogopa sana Yawe na Samweli.
19Hivyo wakamwambia Samweli: “Tafazali, utuombee sisi watumishi wako kwa Yawe, Mungu wako, kusudi tusikufe; kwa sababu tumezidisha zambi zetu kwa uovu huo wa kujitakia mufalme.”
20Samweli akawajibu: “Musiogope. Ingawa mumefanya uovu huu, musiache kumufuata Yawe, lakini mumutumikie kwa moyo wenu wote.
21Musiifuate miungu ya uongo isiyokuwa na faida wala haiwezi kuwaokoa, maana ni ya uongo.
22Kwa heshima ya jina lake kubwa, Yawe hatawatupa watu wake kwa sababu amependa kuwafanya ninyi mukuwe watu wake.
23Tena kwa upande wangu haitatokea niache kuwaombea kwa Yawe; kufanya hivyo itakuwa kumukosea Yawe. Nitaendelea kuwafundisha njia njema na ya haki.
24Basi, ninyi mumutii Yawe na kumutumikia kwa uaminifu, kwa moyo wenu wote. Mukumbuke yale mambo makubwa aliyowatendea.
25Lakini kama mukiendelea kutenda maovu, mutaangamia ninyi wenyewe pamoja na mufalme wenu.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.