ZAKARIA 8 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Muji Yerusalema utakuwa tena muji wa amani

1Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

Yawe wa majeshi anasema hivi:

2Ninachomwa na upendo mukubwa kwa ajili ya Sayuni, na ninawaka kasirani nyingi juu ya waadui zake.

3Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitaurudilia Sayuni na kufanya makao yangu katika Yerusalema. Muji Yerusalema utaitwa “Muji Mwaminifu”, na mulima wa Yawe wa majeshi utaitwa “Mulima Mutakatifu”.

4Yawe wa majeshi anasema hivi: Wazee, wanaume na wanawake, wataonekana tena wakiikaa kwenye barabara za Yerusalema, kila mumoja na fimbo yake kwa sababu ya kuishi miaka mingi.

5Barabara za Yerusalema zitajaa vijana wanaume na wanawake, wakichezacheza mule.

6Yawe wa majeshi anasema hivi: Kwa watu hawa waliobaki, hali hii inaonekana kuwa kitu kisichowezekana; lakini munazani haiwezekani kwangu mimi?

–Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.

7Yawe anasema hivi: Nitawaokoa watu wangu kutoka inchi ya mashariki na kutoka inchi ya magaribi

8na kuwafanya wakae katika Yerusalema. Wao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; nitatawala juu yao kwa uaminifu na haki.

9Yawe wa majeshi anasema hivi: Mujipe moyo! Sasa munayasikia maneno ambayo mulitangaziwa na manabii wakati musingi wa hekalu langu ulipowekwa kulijenga upya.

10Mbele ya wakati huo, watu hawakupata mushahara kwa kazi zao wala mali kwa ajili ya kutumikisha nyama. Hamukuwa na usalama kwa sababu ya waadui zenu, maana nilisababisha uadui kati ya watu wote.

11Lakini sasa sitawatendea hao watu wa taifa hili wanaobaki kama vile zamani.

–Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.–

12Sasa nitaleta tena amani katika dunia, mvua itanyesha kama kawaida, udongo utatoa mazao, na mizabibu itazaa kwa wingi. Nitawapa watu wanaobaki wa taifa hili yale yote yakuwe mali yao.

13Enyi watu wa Yuda na watu wa Israeli! Wakati uliopita ninyi mulionekana kuwa watu waliolaaniwa kati ya watu wa mataifa. Lakini sasa mimi nitawaokoa, nanyi mutakuwa watu waliobarikiwa. Basi, musiogope tena, lakini mujipe moyo!

14Yawe wa majeshi anasema hivi: Kama nilivyokusudia kuwatendea ninyi maovu kwa sababu babu zenu walinikasirikisha wala sikuwaonea huruma,

15vile vile nimekusudia kuutendea wema Yerusalema na watu wa Yuda. Basi, musiogope.

16Hivi ndivyo munavyopaswa kufanya: Kila mumoja wenu amwambie mwenzake ukweli. Tribinali zenu zitoe siku zote hukumu za haki zinazoleta amani. Ang. Efe 4.25

17Mutu yeyote asikusudie kumutendea mwenzake ubaya wala musiape uongo, maana ninayachukia sana matendo hayo. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo.

18Yawe wa majeshi akanitolea mimi Zakaria ujumbe huu:

19Yawe wa majeshi anasema hivi: Siku za mafungo ya kula chakula ya mwezi wa ine, mwezi wa tano, mwezi wa saba na mwezi wa kumi, zitakuwa nyakati za furaha na shangwe; zitakuwa sikukuu za shangwe kwa watu wa Yuda. Basi, mupende ukweli na amani.

20Yawe wa majeshi anasema hivi: Watu wengi wa mataifa ya kigeni na wakaaji wa miji mingi watajaa katika Yerusalema.

21Wakaaji wa muji mumoja watawaendea wakaaji wa muji mwingine na kuwaambia: Tuende pamoja kumwabudu Yawe wa majeshi na kumwomba baraka!

22Kweli, mataifa yenye nguvu na watu wengi watakuja Yerusalema kumwabudu Yawe wa majeshi na kumwomba baraka.

23Yawe wa majeshi anasema hivi: Wakati ule, watu kumi kutoka mataifa ya kila luga watamukamatilia Muyuda mumoja na kushika nguo yake na kumwambia: Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa sababu tumesikia kwamba Mungu yuko pamoja nanyi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help