1Watu wote wa Israeli, kutokea Dani mpaka Beri-Seba, pamoja na watu wa inchi ya Gileadi, wakakusanyika kule Misipa, mbele ya Yawe.
2Viongozi wote wa makabila ya Israeli wakajitokeza mbele ya mukusanyiko wa watu wa Mungu. Wote kwa jumla walikuwa waaskari elfu mia ine wa miguu wenye silaha.
3Nao watu wa kabila la Benjamina, wakapata habari kwamba watu wale wengine wa Israeli walikuwa wamekusanyika kule Misipa.
Basi Waisraeli wakamwuliza yule mwanaume Mulawi: “Utuelezee, uovu ule ulifanyika namna gani?”
4Yule Mulawi, mume wa yule muke, akawajibu: “Mimi na habara yangu tulifika katika muji wa Gibea, muji wa kabila la Benjamina kusudi tulale kule usiku.
5Lakini watu wa muji wa Gibea wakakuja usiku wakaizunguka nyumba nilimokuwa nimelala. Wakataka kuniua, wakamutendea kwa kinguvu habara yangu mpaka akakufa.
6Mimi nikabeba maiti yake, nikamukatakata vipande na kuvipeleka kwa makabila yote ya Israeli, maana wamefanya jambo la kuchukiza na potovu katika Israeli.
7Sasa enyi Waisraeli, mushauriane na mutoe uamuzi wenu.”
8Watu wote kwa pamoja, wakasimama na kusema: “Hakuna yeyote kati yetu atakayerudi katika hema yake au katika nyumba yake.
9Hivi ndivyo tutakavyofanya juu ya Gibea: Tutapiga kura namna ya kuwashambulia.
10Tutachagua watu kumi katika kila watu mia moja wa Israeli, watu mia moja katika kila watu elfu moja, watu elfu moja katika kila watu elfu kumi. Hao watakuwa na kazi ya kuwaletea chakula wenzao watakaokuwa na kazi ya kuuazibu muji wa Gibea katika inchi ya Benjamina kwa ajili ya ubaya wao na upotovu walioufanya katika Israeli.”
11Kwa hiyo wanaume wote wa Israeli wakakusanyika kwa moyo mumoja kwa kushambulia muji wa Gibea.
12Watu wa makabila ya Israeli wakatuma wajumbe mpaka kila sehemu ya kabila la Benjamina, wakisema: “Ni uovu gani huu uliotukia kati yenu?
13Sasa mutupe hao watu watenda maovu wa Gibea kusudi tuwaue na kuondoa uovu huu kutoka Israeli.” Lakini watu wa kabila la Benjamina hawakuwasikiliza wandugu zao, Waisraeli.
14Basi wakakusanyika kule Gibea kutoka katika kila muji wao, kwa kupigana na Waisraeli.
15Watu wa kabila la Benjamina wakakusanya kutokea miji yao jeshi la watu elfu makumi mbili na sita wenye kutumia silaha, nao wakaaji wa muji wa Gibea wakakusanya watu mia saba waliochaguliwa.
16Kati ya watu hao waliochaguliwa kulikuwa watu mia saba waliotumia zaidi mukono wa kushoto; kila mumoja aliweza kurusha jiwe kwa mujeledi na kupiga unywele bila kukosa.
17Waisraeli, bila kuhesabu kabila la Benjamina, wakakusanya watu elfu mia ine wanaozoea kutumia silaha. Wote walikuwa hodari wa vita.
18Waisraeli wakaenda Beteli kuomba shauri kwa Mungu, wapate kujua kabila ambalo litakwenda kwanza kupigana na watu wa kabila la Benjamina. Yawe akataja kabila la Yuda liende kwanza.
19Basi, Waisraeli wakaenda asubui, wakapiga kambi yao karibu na muji wa Gibea.
20Waisraeli wakatoka kwa kupigana na watu wa kabila la Benjamina karibu na Gibea.
21Watu wa kabila la Benjamina wakatoka inje ya muji wa Gibea, wakapigana na Waisraeli, wakawaangusha chini siku hiyo, watu wa Israeli elfu makumi mbili.
22Lakini Waisraeli wakajipa moyo, wakajipanga tena kwa vita pahali pale walipojipanga kwa mara ya kwanza.
23Basi Waisraeli wakaenda juu, wakamulilia Yawe mpaka magaribi. Kisha wakaomba shauri kwa Yawe: “Twende tena kupigana na wandugu zetu, wa kabila la Benjamina?” Yawe akawajibu: “Muende mupigane nao.”
24Hivyo, kwa siku ya pili Waisraeli wakakaribia kupigana na watu wa kabila la Benjamina.
25Kwa siku hiyo ya pili watu wa kabila la Benjamina walitoka Gibea na kuwashambulia Waisraeli, wakawaangusha chini Waisraeli elfu kumi na nane.
26Watu wote wa jeshi la Waisraeli wakaenda Beteli. Wakaikaa kule mbele ya Yawe wakiomboleza na kufunga mpaka magaribi. Wakamutolea Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani.
27Waisraeli wakamwomba Yawe awape shauri. Wakati ule Sanduku la Agano la Yawe lilikuwa kule Beteli.
28Finehasi mwana wa Eleazari mwana wa Haruni alikuwa na kazi ya kutumika mbele yake. Waisraeli wakamwuliza Yawe: “Twende tena kupigana na wandugu zetu, watu wa kabila la Benjamina?” Yawe akawaambia: “Muende. Kesho nitawatia katika mikono yenu.”
29Hivyo, Waisraeli wakaweka watu kwenye maficho kuuzunguka muji wa Gibea.
30Waisraeli wakaenda kupigana na watu wa kabila la Benjamina katika siku ya tatu. Wakajipanga kwa kushambulia muji wa Gibea kama walivyofanya nyakati za mbele.
31Kisha watu wa kabila la Benjamina walipotoka katika muji kwa kuanza kupigana na Waisraeli, walivutwa kutoka inje ya muji. Ilitokea tena kama walivyofanya nyakati za mbele. Wakawaua wamoja kati ya watu wa Israeli kwenye njia kubwa zinazoelekea miji ya Beteli na Gibea, mpaka katika mbuga. Waliua Waisraeli yapata makumi tatu.
32Watu wa Benjamina wakafikiri: “Tumewapiga kama nyakati zilizopita.” Lakini Waisraeli wakasema: “Sisi tukimbie kusudi tuwavute mbali na muji mpaka kwenye njia kubwa.”
33Hivyo watu wote wa Israeli wakatoka kwenye sehemu yao na kujipanga tena kule Bali-Tamari. Wenzao waliokuwa wanafichama wakatoka haraka pahali pao upande wa magaribi wa muji wa Gibea.
34Waaskari hodari waliochaguliwa kutoka makabila yote ya Israeli wakafika pale mbele ya muji wa Gibea. Vita ya siku hiyo ilikuwa kali. Lakini watu wa Benjamina hawakufahamu kwamba kuangamia kwao kulikuwa karibu.
35Yawe akawashinda watu wa Benjamina mbele ya Waisraeli. Waisraeli wakawaua watu wa Benjamina elfu makumi mbili na tano na mia moja. Hao wote waliouawa walikuwa waaskari walioweza kutumia silaha.
36Kwa hiyo watu wa kabila la Benjamina wakaona kwamba wameshindwa.
Waisraeli wakarudi nyuma sawa vile wanawakimbia watu wa kabila la Benjamina, maana walitegemea wenzao waliokuwa wamewekwa kufichamia muji wa Gibea.
37Wale waliowekwa kufichamia muji walitoka haraka na kuushambulia muji wa Gibea na kuwaua wote waliokuwa mule kwa upanga.
38Walikuwa wamekubaliana na wale watu wengine wa Israeli juu ya kitambulisho kimoja. Walikubaliana kwamba wale waliokuwa wanajificha watakapoona moshi mukubwa unapanda juu kutoka katika muji,
39basi, wageuke kwa kupigana. Wakati ule, watu wa kabila la Benjamina walikuwa wamekwisha kuua watu yapata makumi tatu wa Israeli na kuambiana: “Tumewapiga kama pale mbele.”
40Lakini kile kitambulisho cha moshi kilipoanza kutokea katika muji, watu wa kabila la Benjamina wakaangalia nyuma yao, wakashangaa kuona kwamba muji wao ulikuwa unateketezwa kwa moto.
41Halafu Waisraeli wakageuka kwa kupigana, na watu wa kabila la Benjamina wakashikwa na woga maana sasa waliona kwamba kuangamia kwao kulikuwa kumekaribia.
42Wakawakimbia Waisraeli kuelekea katika jangwa, lakini vita ikawapata. Wakajikuta wako katikati ya majeshi mawili ya Israeli, na waaskari waliotoka wakawaangamiza.
43Waisraeli waliwazunguka watu wa kabila la Benjamina, wakawafuatilia kutoka Noha mpaka upande wa mashariki wa muji wa Gibea wakiwaua wengi kati yao.
44Siku hiyo watu elfu kumi na nane wa kabila la Benjamina, wote waaskari hodari, wakauawa.
45Watu wengine wa kabila la Benjamina wakakimbia kuelekea upande wa jangwa mpaka kwenye mulima wa Rimoni. Wengine elfu tano waliuawa kwenye njia kubwa walipokuwa wanakimbia. Waisraeli waliendelea kuwafuatilia vikali watu wa kabila la Benjamina mpaka kwenye muji wa Gidomu, wakawaua watu elfu mbili.
46Jumla ya watu wote wa kabila la Benjamina waliouawa siku hiyo ilikuwa elfu makumi mbili na tano, waaskari hodari wa kutumia silaha.
47Lakini wanaume mia sita wa kabila la Benjamina walipata kukimbilia katika jangwa mpaka kwenye mulima wa Rimoni, wakakaa kule kwa muda wa miezi mine.
48Waisraeli wakawageukia watu wengine wa kabila la Benjamina, wakawaua wote: wanaume, wanawake, watoto na nyama. Na miji yote waliyoikuta kule wakaiteketeza kwa moto.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.