1Basi wandugu zangu, kufuatana na vile Mungu alivyoonyesha huruma yake kwetu, ninawasihi mujitoe wenyewe kwake kuwa sadaka yenye uzima, takatifu na yenye kumupendeza. Hii ndiyo njia ya kweli ya kumwabudu.
2Musifuate mwenendo wa siku hizi, lakini muache Mungu awabadilishe kwa kugeuza upya nia zenu, hata mukuwe na mawazo mapya. Kwa hiyo mutaweza kutambua mapenzi ya Mungu. Mutajua mambo gani yanayokuwa mema, yanayomupendeza Mungu na yanayokuwa makamilifu.
3Kufuatana na neema niliyopewa na Mungu, ninawaambia ninyi wote: mutu asijiwazie kuwa na ukubwa kupita vile inavyomustahili. Lakini mukuwe na mawazo ya ukadirifu, kila mumoja kulingana na kipimo cha imani aliyopewa na Mungu.
4Katika mwili mumoja kuna viungo vingi, lakini viungo hivi vyote havina kazi moja.
5Hivi vilevile, sisi tunaokuwa wengi tumekuwa mwili mumoja katika kuungana kwetu na Kristo, na sisi wote ni viungo kila mumoja kwa mwingine.
6Tuko na zawadi mbalimbali kwa kadiri ya neema tuliyopewa na Mungu. Aliyepewa zawadi ya unabii, anapaswa kutabiri kwa kadiri ya imani yake.
7Aliyepewa zawadi ya utumishi, atumike. Aliyepewa zawadi ya kufundisha, afundishe.
8Aliyepewa zawadi ya kuonya wengine, awaonye. Aliyepewa zawadi ya kutoa, atoe kwa moyo mweupe. Anayesimamia wengine, awasimamie kwa bidii. Aliyepewa zawadi ya kuhurumia wengine, afanye vile kwa furaha.
9Upendo wenu ukuwe pasipo udanganyifu. Muchukie chochote kinachokuwa kibaya, mushikamane na kinachokuwa chema.
10Mupendane ninyi kwa ninyi kwa kweli kama vile wandugu, nanyi muheshimiane ninyi kwa ninyi.
11Musikuwe wavivu katika kazi lakini mukuwe na bidii, mukimutumikia Bwana kwa juhudi.
12Mufurahi mukiwa na tumaini, muvumilie katika mateso, mudumu katika kuomba.
13Muwasaidie watu wa Mungu katika mahitaji yao na muwakaribishe wageni.
14Mumwombe Mungu awabariki wale wanaowatesa; muwaombee baraka wala musiwalaani.
15Mufurahi pamoja na wenye kufurahi. Mulie pamoja na wenye kulia.
16Mukuwe na masikilizano kati yenu. Musikuwe na nia ya kujitukuza, lakini mukubali kuishi katika unyenyekevu. Musijiwazie kuwa wenye akili sana.
17Musimurudishie mutu ubaya kwa ubaya. Mukuwe na roho ya kufanya mema mbele ya watu wote.
18Kama ikiwezekana, kwa upande wenu, muishi katika amani na watu wote.
19Wandugu wapendwa, musilipize kisasi ninyi kwa ninyi, lakini mumwachie Mungu wakati wa kutenda kufuatana na kasirani, maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Ni kazi yangu kulipiza kisasi. Ni mimi nitakayelipiza.”
20Lakini kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Adui yako akisikia njaa, umupe chakula; kama akisikia kiu, umupe kinywaji. Maana kwa kufanya hivi utamupatisha haya kama vile ungemubebesha makaa ya moto juu ya kichwa.”
21Usijiachilie kushindwa na ubaya, lakini ushinde ubaya kwa kutenda mema.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.