Kutoka 30 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mazabahu ya kufukizia ubani(Kut 37.25-28)

1Utatengeneza mazabahu kwa mbao za mujohoro kusudi pawe pahali pa kufukizia ubani.

2Mazabahu hiyo ikuwe ya muraba, urefu na upana wake sentimetre makumi ine na tano, na urefu kwenda juu sentimetre makumi tisa. Pembe zake za juu zitatokeza zote zikiwa kitu kimoja na mazabahu yenyewe.

3Yote utaipakaa zahabu safi: upande wake wa juu, pande zake zote za ubavu na pembe zake. Vilevile utaizungushia ukingo wa zahabu.

4Utaitengenezea pete mbili za zahabu na kuzitia chini ya ukingo wake kwenye pande mbili zinazoelekeana. Hizo pete zitatumiwa kwa kushikilia miti wakati wa kuibeba.

5Miti hiyo ikuwe ya mujohoro na ipakwe zahabu.

6Mazabahu hiyo iwekwe mbele ya pazia kando ya Sanduku la Agano, mbele ya kiti cha rehema ambapo nitakutana nawe.

7Kila siku Haruni anapoingia kwa kutayarisha taa zinazokuwa pale, atafukiza ubani wenye harufu nzuri juu ya mazabahu hiyo.

8Tena atafukiza ubani wakati wa magaribi anapowasha taa. Sadaka hii ya ubani itatolewa siku zote bila kukoma katika vizazi vyenu vyote.

9Kwenye mazabahu hiyo, musifukize hata kidogo ubani usiokuwa mutakatifu, wala musitoe sadaka ya kuteketezwa, wala sadaka ya ngano, wala kumimina juu yake sadaka ya kinywaji.

10Haruni atafanya upatanisho juu ya pembe za mazabahu hiyo mara moja kwa mwaka. Ataifanyia upatanisho kwa damu ya sadaka ya maondoleo ya zambi mara moja kila mwaka katika vizazi vyenu vyote, maana mazabahu hiyo ni takatifu kabisa kwangu, mimi Yawe.

Matoleo za hema la mukutano

11Yawe akamwambia Musa:

12Kila mara utakapowahesabu Waisraeli, kila mumoja atatoa malipo kwa Yawe kwa ajili ya nafsi yake kusudi kusikuwe hasara kati yao wakati wa kuhesabiwa.

13Kila mumoja atakayehesabiwa anapaswa kulipa nusu ya shekeli kulingana na vipimo vya hema la mukutano. Hii ni sadaka yake atakayonitolea. Ang. Kut 38.25-26; Mat 17.24

14Kila mumoja atakayehesabiwa, tangu umri wa miaka makumi mbili na zaidi, atanitolea sadaka hiyo.

15Tajiri asitoe zaidi wala masikini asitoe chini ya nusu ya shekeli wakati munaponitolea sadaka hiyo kwa kufanya upatanisho.

16Wewe utaipokea feza hiyo ya upatanisho kutoka kwa Waisraeli, nawe utaitumia kwa shuguli za kazi za hema takatifu, nayo ikuwe ni ukumbusho wa Waisraeli mbele yangu, malipo ya maisha yenu.

17Yawe akamwambia Musa:

18Utatengeneza birika la shaba kwa kuoga lenye tako la shaba, uliweke katikati ya hema la mukutano na mazabahu, na kutia maji ndani yake. Ang. Kut 38.8

19Haruni na wana wake watatumia maji hayo kwa kunawa mikono na miguu,

20mbele ya kuingia kwenye hema la mukutano au kukaribia mazabahu kwa kunitolea sadaka mimi Yawe, sadaka za kuteketezwa kwa moto. Watafanya hivyo kusudi wasikufe.

21Wanapaswa kunawa mikono na miguu yao kusudi wasikufe. Hili ni sharti kwao siku zote, tangu Haruni na uzao wake, vizazi kwa vizazi.

Mafuta ya kupakaa

22Yawe akamwambia Musa: Ang. Kut 37.29

23Utatwaa viungo bora kabisa kama hivi: manemane ya maji kilo sita, mudalasini wenye harufu nzuri kilo tatu, miwa yenye harufu nzuri kilo tatu,

24na aina nyingine ya mudalasini kilo sita – vipimo hivyo vyote vikuwe kufuatana na vipimo vya hema takatifu. Twaa vilevile litre ine za mafuta.

25Kutokana na viungo hivyo utatengeneza mafuta matakatifu uyachanganye kama vile fundi wa manukato anavyofanya. Hayo yatatumika kwa kutakasa vitu.

26Kisha utamiminia hema la mukutano mafuta hayo, Sanduku la Agano,

27meza na vyombo vyake vyote, kinara cha taa na vyombo vyake, mazabahu ya kufukizia ubani,

28mazabahu ya sadaka za kuteketezwa kwa moto na vyombo vyake vyote, na birika na tako lake.

29Utavitakasa, kusudi vikuwe vitakatifu kabisa. Chochote kitakachogusa vifaa hivyo, kitakuwa kitakatifu.

30Kisha umupakae Haruni mafuta na wana wake na kuwatakasa kusudi wanitumikie kama vile makuhani.

31Uwaambie Waisraeli kwamba haya yatakuwa mafuta yangu matakatifu ya kupakaa katika vizazi vyenu vyote.

32Mafuta haya yasimiminiwe hata kidogo mutu yeyote wa kawaida, wala kusitengenezwe mafuta mengine ya aina hii. Haya ni mafuta matakatifu na yanapaswa kuwa siku zote matakatifu kwenu.

33Yeyote atakayetengeneza mafuta kama haya, au kumupakaa mutu asiyestahili kupakwa mafuta haya, mutu huyu atatengwa mbali na watu wake.

34Yawe akamwambia Musa: Utatwaa vipimo vinavyolingana vya viungo vitamu hivi: utomvu wa natafi, utomvu wa shekeleti, utomvu wa kelbena na ubani safi.

35Utatumia vitu hivyo kwa kutengeneza ubani kama vile unavyotengenezwa na fundi wa manukato, utiwe chumvi upate kuwa safi na mutakatifu.

36Kisha utasagwa na kufanya unga laini, upate kutumiwa ndani ya hema la mukutano na kulipakaa Sanduku la Agano, pahali nitakapokutana nawe. Huo utakuwa ubani mutakatifu kabisa kwenu.

37Musifanye hata kidogo ubani wa muchanganyiko huo kwa matumizi yenu wenyewe maana ubani huo utakuwa mutakatifu mbele yangu.

38Yeyote atakayejitengenezea ubani wa aina hiyo na kuutumia kama manukato yake pekee, atatengwa mbali na watu wake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help