1Basi kuna faida gani kuwa Muyuda? Na kutahiriwa kuna mafaa gani?
2Kuna faida kubwa sana kila upande. Kwanza, Mungu alifunua Neno lake kwa Wayuda kusudi walishike.
3Tuseme nini basi? Ikiwa wamoja kati yao hawakukuwa waaminifu, jambo hilo litaweza kuonyesha kwamba Mungu ataacha kuwa mwaminifu?
4Hapana hata kidogo! Sherti Mungu ajulikane kuwa mwenye ukweli, na kila mutu kuwa mwongo, kama inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu:
“Ee Mungu, sherti ujulikane kuwa mwenye haki katika masemi yako.
Nawe ushinde wakati unaposhitakiwa.”
5Lakini ikiwa kwa njia ya ubaya tunaofanya, Mungu anaonekana kuwa mwenye haki, basi tutasema kama Mungu hana haki wakati anapotuazibu? (Ninasema kwa mafikiri ya kimutu.)
6Hapana hata kidogo! Ingekuwa vile, namna gani basi Mungu angeweza kuhukumu dunia?
7Lakini ikiwa kwa njia ya uongo wangu ukweli wa Mungu unaonekana naye anatukuzwa zaidi, basi kwa nini tena ninahukumiwa kama mwenye zambi?
8Ikiwa ni vile, basi tuseme: “Tufanye mabaya kusudi kutokee mema”? Hakika kuna watu wamoja wanaonisingizia wakisema kwamba nimesema vile. Watu hawa wataazibiwa sawa inavyowapasa!
Hakuna mwenye haki mbele ya Mungu9Basi tuseme nini? Sisi Wayuda tunawapita watu wa mataifa mengine nini? Hatuwapiti kitu hata kimoja! Kwa maana nimekwisha kuonyesha kwamba Wayuda na watu wa mataifa mengine wote wako chini ya utawala wa zambi.
10Ni sawa ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu:
“Hakuna hata mutu mumoja mwenye haki!
11Hakuna mutu mwenye ufahamu,
hakuna mwenye kushugulika na Mungu.
12Wote wamepotea, wote kwa jumla wamepotoka.
Hakuna mwenye kufanya mema, hata mumoja.
13Vinywa vyao ni kama kaburi wazi,
ndimi zao ni za kudanganya,
ndani ya midomo yao munatoka sumu kali sawa ya nyoka.
14Vinywa vyao vinajaa laana na maneno ya uchungu.
15Wao ni wepesi kwa kumwanga damu.
16Wanaharibu na kuangamiza popote wanapopita,
17hawawazi juu ya njia ya kuleta amani,
18nao hawamwogopi Mungu hata kidogo.”
19Basi tunajua kama maneno yote yanayosemwa na Sheria, yanawaelekea wale wanaolazimishwa kutii Sheria, kusudi mutu yeyote asikuwe na namna ya kujitetea, na dunia nzima ipaswe kuhukumiwa na Mungu.
20Kwa sababu hakuna mutu atakayehesabiwa haki mbele ya Mungu kwa kuwa anatii Sheria, maana Sheria inamusaidia mutu tu kwa kutambua kwamba amefanya zambi.
Namna Mungu anavyowahesabia watu haki21Lakini sasa Mungu ameonyesha njia ya kumuhesabia mutu haki mbele yake, na si kwa njia ya Sheria. Maandiko ya Sheria na manabii yanashuhudia kwamba
22kuhesabiwa haki na Mungu kunapatikana kwa njia ya imani katika Yesu Kristo kwa wote wanaoamini, kwa maana hakuna tofauti yoyote kati yao,
23kwa maana wote wamefanya zambi na kukosa utukufu wa Mungu.
24Lakini kwa neema ya Mungu wanahesabiwa haki kwa bure kwa njia ya Kristo Yesu anayewakomboa.
25-26Kristo alitolewa na Mungu kuwa sadaka ya usamehe wa zambi kwa njia ya damu yake kwa ajili ya wenye kumwamini. Mungu alifanya hivi kwa kuonyesha haki yake. Zamani, katika uvumilivu wake, aliacha kuazibu zambi za watu. Lakini kwa wakati wa sasa anaonyesha haki yake kusudi akuwe mwenye haki na kumuhesabia haki kila mutu anayemwamini Yesu.
27Basi sasa mutu ataweza kujivuna? Hapana! Kwa sababu gani? Kwa sababu anatii Sheria? Hapana. Lakini kwa sababu anamwamini Yesu.
28Kwa maana tunaona kama mutu anahesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya imani wala si kwa njia ya kutii Sheria.
29Au Mungu ni Mungu wa Wayuda tu? Yeye si Mungu wa watu wa mataifa mengine vilevile? Ndiyo, yeye ni Mungu wa watu wa mataifa mengine vilevile,
30kwa sababu kuna Mungu mumoja tu. Na ni yeye atakayewahesabia Wayuda na watu wa mataifa mengine haki mbele yake kwa njia ya imani ya kila wamoja.
31Basi ni kusema kwa sababu ya imani ile tunaitupilia Sheria? Hapana hata kidogo! Lakini tunasimamisha Sheria.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.