1Kisha Yobu akajibu:
2Kweli ninajua kama ni hivi.
Lakini mutu anaweza namna gani kuwa haki mbele ya Mungu?
3Kama mutu angesubutu kushindana naye,
hataweza kufika mbali,
hata kujibu ulizo moja kati ya elfu.
4Yeye ni mwenye hekima sana na nguvu nyingi.
Nani aliyepingana naye, akashinda?
5Yeye anahamisha milima bila yenyewe kutambua,
anaipindua mbali kwa hasira yake.
6Yeye anaitikisa dunia kutoka pahali pake,
na nguzo zake zinatetemeka.
7Anaamuru jua lisipande,
anafunika nyota zisiangaze.
8Yeye peke yake alitandaza mbingu,
na kuyakanyaga mawimbi ya bahari.
9Yeye aliweka makundi ya nyota katika anga:
Dubu, Orioni, Kilimia, na Vyumba vya Kusini.
10Ndiye anayetenda mambo makubwa yasiyoeleweka,
mambo ya ajabu yasiyokuwa na hesabu.
11Anapita karibu nami lakini simwoni,
kisha anajiendea zake bila mimi kumutambua.
12Yeye akitwaa kitu kwa rafla,
nani anayeweza kumuzuia?
Nani anayeweza kumwuliza:
“Unafanya nini?”
13Mungu hatazuia hasira yake;
Rahabu na wasaidizi wake wanainama chini mbele yake.
14Nitaweza namna gani basi kumujibu Mungu?
Nitachagua wapi maneno ya kumwambia?
15Ingawa sina kosa, siwezi kumujibu.
Ninapaswa kumwomba mwamuzi wangu huruma.
16Hata kama ningemwita naye akijibu,
nisingeweza kuamini kwamba ananisikiliza.
17Yeye ananiponda kwa zoruba,
anaongeza vidonda vyangu bila sababu.
18Haniachi hata nipumue;
maisha yangu anayajaza uchungu.
19Kama ni kushindana, yeye ana nguvu sana!
Na kama ni kutafuta juu ya haki,
nani atakayemuleta mbele ya tribinali?
20Ingawa sina kosa,
maneno yangu yenyewe yangenihukumu.
Ingawa mimi ni mukamilifu,
yangehakikisha kwamba mimi ni mupotovu.
21Mimi ni mukamilifu.
Siangalii nafsi yangu.
Ninachukia maisha yangu.
22Yote ni mamoja, kwa hiyo ninasema:
Mungu anawaangamiza wakamilifu na waovu.
23Musiba unapoleta kifo cha rafla,
anachekelea hasara ya wasiokuwa na kosa.
24Inchi ikitiwa katika utawala wa mwovu,
Mungu anafunga macho ya waamuzi wake!
Kama si yeye anayefanya hivyo, ni nani basi?
25Siku zangu zinaenda mbio kuliko mukimbiaji,
zinakimbia bila kuona faida.
26Zinapita mbio kama mashua ya matete,
kama tai anayerukia mawindo yake.
27Ninasema: “Nitasahau malalamiko yangu,
niondoe uso wangu wa huzuni na kuwa na furaha!”
28Lakini ninaogopa maumivu yangu yote,
maana ninajua Mungu hataniona kuwa sina kosa.
29Ikiwa nitahukumiwa kuwa na kosa,
kwa nini basi nijisumbue bure?
30Hata kama nikinawa na teluji,
na kujitakasa mikono kwa sabuni,
31hata hivyo, atanitumbukiza katika shimo kwenye uchafu,
na nguo zangu zitanichukia.
32Mungu si mutu kama mimi nipate kumujibu,
hata tuweze kwenda katika tribinali pamoja.
33Hakuna mwamuzi kati yetu
ambaye angetuamua sisi wawili.
34Mungu aniondolee hiyo fimbo ya kunipiga,
na kitisho chake kisinitie hofu!
35Halafu ningeweza kusema bila kumwogopa;
maana si vile ninavyokuwa ndani yangu.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.