Matendo ya Mitume 24 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Wayuda wanamushitaki Paulo

1Kulipopita siku tano, Kuhani Mukubwa Anania akaenda Kaisaria pamoja na wasimamizi wamoja wa watu na mutetezi mumoja wa sheria aliyeitwa Tertulo. Nao wakafika mbele ya liwali Feliki kwa kumushitaki Paulo.

2Walipomwita Paulo, Tertulo akaanza kumushitaki, akisema:

“Muheshimiwa Feliki, kwa njia yako tumepata amani ya kweli. Na kwa uongozi wako umeleta mabadiliko mengi mazuri kwa ajili ya taifa hili.

3Kwa yote hatutasahau mambo hayo yote kila wakati na kila fasi, nasi tunakushukuru sana.

4Lakini, sababu sitaki kukupotezea wakati murefu, ninakusihi usikilize kwa wema wako maneno tutakayosema kwa kifupi.

5Tumetambua kwamba mutu huyu ni wa hatari sana, ameanzisha fujo kati ya Wayuda wote katika dunia. Tena yeye ni mukubwa wa chama cha Wanazareti.

6Naye alijaribu kuchafua hekalu, lakini tukamukamata. Na wewe mwenyewe utaweza kumusambisha mutu huyu, na kufahamu vizuri mambo yale tunayomushitakia.”

9Wayuda wakamwunga mukono, wakisema kwamba maneno yale yote ni ya kweli.

Paulo anajitetea mbele ya liwali Feliki

10Kisha liwali akamufanyia Paulo alama kwa kumuruhusu kusema, naye akasema: “Ninajua kwamba wewe umekuwa mwamuzi wa taifa hili tangia miaka mingi. Sababu hii sina wasiwasi kwa kujitetea mbele yako.

11Kama unavyoweza kuhakikisha wewe mwenyewe, hakujapita zaidi ya siku kumi na mbili tangu nilipoenda Yerusalema kwa kumwabudu Mungu.

12Watu hawa hawakunikuta ndani ya hekalu wala ndani ya nyumba za kuabudia, wala nafasi ingine katika muji nikibishana na mutu au nikisukuma watu kufanya fujo.

13Nao hawawezi kuhakikisha maneno wanayonishitakia sasa.

14Lakini ninakubali mbele yako kwamba ninamutumikia Mungu wa babu zetu nikifuata Njia ile wanayosema kwamba ni ya uongo. Mimi ninaamini maneno yote yaliyoandikwa katika kitabu cha Sheria na katika vitabu vya manabii.

15Ninatumaini toka kwa Mungu sawa vile watu hawa wanavyotumaini, kwamba watu wema na wabaya wote watafufuliwa.

16Kwa sababu hii ninajikaza siku zote kuishi maisha safi bila kuhukumiwa na zamiri yangu mbele ya Mungu na mbele ya watu.

17“Nyuma ya kupitisha miaka mingi mbali na muji, nilirudi kule Yerusalema kuwaletea watu wa taifa langu musaada wa mali na kumutolea Mungu sadaka.

18Na wakati ule nilipokuwa nikifanya mambo hayo, walinikuta katika hekalu, nami nilikuwa nimekwisha kufanya ibada ya kutakaswa. Sikukuwa na kundi la watu wala kuleta fujo.

19Lakini Wayuda wamoja waliotoka katika jimbo la Azia walikuwa pale, na ni hao ndio wangepaswa kuja mbele yako kunishitaki ikiwa wako na neno lolote juu yangu.

20Au watu hawa wanaokuwa hapa waseme kosa waliloniona nalo wakati niliposambishwa mbele ya Baraza Kubwa.

21Neno moja tu nililosema kwa sauti nilipokuwa nikisimama ni hili: ‘Ninahukumiwa leo kwa sababu ninatumaini kama wafu watafufuliwa.’ ”

22Halafu Feliki, aliyekuwa akifahamu vizuri mambo yanayoelekea Njia ya Bwana, akaamuru maneno yale yarudiliwe, akisema: “Nitakata maneno yenu wakati jemadari Lusia atakapokuja.”

23Kisha akamwamuru yule mukubwa wa jeshi kwamba wamulinde Paulo katika kifungo wakimwachia uhuru kidogo, na wasiwazuize warafiki zake kumusaidia.

Liwali Feliki na muke wake Drusila wanamusikiliza Paulo

24Nyuma ya siku chache, liwali Feliki akakuja pamoja na muke wake Drusila, aliyekuwa Muyuda. Akaamuru wamwite Paulo, naye akasikiliza maneno aliyosema juu ya kumwamini Kristo Yesu.

25Lakini Paulo alipokuwa akihubiri juu ya haki, juu ya kujizuiza na juu ya siku ya hukumu ya Mungu itakayokuja, Feliki akaogopa na kumwambia: “Kwa sasa unaweza kujiendea. Nitakuita tena nitakapopata wakati.”

26Vilevile alikuwa akitazamia kwamba Paulo atamupatia feza. Ni kwa sababu hii alimwita kila mara kwa kuzungumuza naye.

27Kulipopita miaka miwili, Porkio Festo akamukomboa Feliki kama liwali. Na kwa sababu Feliki alitaka kujipendekeza kwa Wayuda, akamwacha Paulo katika kifungo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help