1Nyuma ya hayo, mufalme Daudi aliwashinda na kuwanyenyekeza Wafilistini. Akakamata muji wa Gati pamoja na vijiji vyake vilivyokuwa vya Wafilistini.
2Akawashinda Wamoabu vilevile, wakakuwa watumishi wake na wakakuwa wanalipa kodi.
3Daudi akamushinda vilevile Hadadezeri mufalme wa Zoba, inchi iliyokuwa karibu na Hamati, alifanya hivyo wakati alipokuwa akienda kujisimamishia nguzo ya ukumbusho kwenye sehemu za muto Furati.
4Daudi akanyanganya magari ya vita elfu moja, waaskari wapanda-farasi elfu saba na wa miguu elfu makumi mbili. Kisha Daudi akakata mishipa ya miguu ya nyuma ya farasi wote wa magari, lakini akaacha mia moja.
5Nao Waaramu wa Damasiki, walipokwenda kumusaidia Hadadezeri mufalme wa Zoba, Daudi akawashambulia na kuwaua watu elfu makumi mbili na mbili.
6Halafu Daudi akaweka kambi za waaskari katika muji wa Damasiki wa Aramu. Basi Waaramu wakakuwa watumishi wake, na wakakuwa wanalipa kodi. Yawe akamupa Daudi ushindi kokote alikokwenda.
7Daudi alitwaa ngao za zahabu ambazo waaskari wa Hadadezeri walizobeba, na kuzipeleka Yerusalema.
8Daudi alichukua vilevile shaba nyingi sana kutoka muji wa Tibuhati na muji wa Kuni iliyokuwa miji ya Hadadezeri. Solomono alitumia shaba hiyo kwa kutengeneza nguzo na vyombo vya shaba.
9Wakati Toi, mufalme wa Hamati aliposikia kwamba Daudi ameshinda waaskari wote wa Hadadezeri mufalme wa Zoba,
10akatuma mwana wake Hadoramu kwa mufalme Daudi, kumupelekea salamu na shukrani kwa sababu alikuwa amepigana na Hadadezeri na kumushinda. Maana Hadadezeri alipigana na Toi mara nyingi. Hadoramu alimupelekea Daudi zawadi za vyombo vya feza, zahabu na shaba.
11Zawadi zile, mufalme Daudi alizitakasa kwa ajili ya Yawe pamoja na feza na zahabu aliyonyanganya kwa mataifa yote, kutoka kwa: Waedomu, Wamoabu, Waamoni, Wafilistini na Waamaleki.
12Abisai mwana wa Zeruya, akaua Waedomu elfu kumi na nane katika Bonde la Chumvi.
13Basi akaweka kambi za waaskari kule Edomu. Nao Waedomu wote wakakuwa watumishi wa Daudi. Yawe alimupa Daudi ushindi kokote alikokwenda.
14Halafu Daudi akatawala juu ya Israeli yote. Aliimarisha haki na sheria ya Mungu kwa watu wote.
15Yoabu mwana wa Zeruya alikuwa jemadari wa makundi ya waaskari; Yehosafati mwana wa Ahiludi alikuwa mwandishi wa habari za kifalme;
16Zadoki mwana wa Ahitubu na Ahimeleki mwana wa Abiatari walikuwa makuhani; Sausa alikuwa katibu;
17na Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa mwangalizi wa waaskari walinzi wa Daudi; wana wa Daudi walikuwa na vyeo vikubwa katika utawala wake.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.