1Siku hiyo, Yawe atakamata upanga wake mukubwa, mukali na imara, na kuiazibu Leviatani, ile nyoka inayoruka na kuzongazonga. Yawe ataua nyoka mukubwa anayeishi katika bahari.
2Siku hiyo, muimbe juu ya shamba zuri la mizabibu:
3Mimi, Yawe, ni mulimaji wake;
ninalimwangilia maji kila wakati.
Ninalilinda usiku na muchana,
kusudi lisiharibiwe na mutu yeyote.
4Silikasirikii tena shamba hili;
kama miiba na michongoma ingelilishambulia,
mimi ningepambana nayo na kuichoma kwa moto.
5Wakitaka ulinzi wangu,
basi, wafanye amani nami.
Wafanye amani nami!
6Itakuja siku wazao wa Yakobo watatoa mizizi;
watu wa Israeli watachanua na kuchipuka,
na kuijaza dunia yote kwa matunda.
7Mungu hakuwaazibu Waisraeli vikali
kama alivyowaazibu waadui zao;
Waisraeli waliouawa
ni wachache kuliko wale waliokuwa wanawaua.
8Aliwaazibu watu wake kwa kuwapeleka katika uhamisho.
Wakati wa upepo mukali wa mashariki,
aliwaondoa kwa pigo kali.
9Hivi ndivyo uovu wa wazao wa Yakobo utakavyoondolewa,
hivi ndivyo zambi yake itakavyofutwa kabisa:
ataziharibu mazabahu za miungu;
mawe yake yatasagwasagwa kama chokaa.
Sanamu za Ashera wala mazabahu za kufukizia ubani hazitabaki.
10Muji ule wenye kuta sasa umekuwa mutupu,
umeachwa na kuhamwa kama jangwa,
humo ngombe wanakula na kupumzika.
11Matawi ya miti yamekauka na kuvunjika;
wanawake wanayaokota na kuyawasha moto.
Watu hawa hawajaelewa kitu,
kwa hiyo Mungu, Muumba wao, hatawahurumia,
yeye aliyewafanya, hatawatendea mema.
12Siku hiyo, Yawe atapepeta ngano yake kutokea kwenye muto Furati mpaka kwenye mupaka wa Misri, nanyi Waisraeli mutakusanywa mumojamumoja.
13Siku hiyo, baragumu kubwa itapigwa na watu wote wa Israeli waliopotea katika inchi ya Asuria au waliotawanywa katika inchi ya Misri watarudi na kumwabudu Yawe juu ya mulima mutakatifu kule Yerusalema.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.