Maombolezo 3 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Azabu, kugeuka na tumaini

1Mimi ni mutu niliyepata mateso

kwa fimbo ya kasirani ya Mungu.

2Amenikamata na kunitembeza

katika giza ambako hakuna mwangaza.

3Amenyoosha mukono wake juu yangu mimi tu,

akiniazibu tena na tena muchana kutwa.

4Amenichakalisha ngozi na nyama,

ameivunja mifupa yangu.

5Amenikusanyia na kunizungushia

uchungu na mateso.

6Amenikalisha katika giza

kama watu waliokufa zamani.

7Amenizungushiia ukuta na siwezi kutoka,

amenifunga kwa minyororo mizito.

8Ingawa ninaita na kuomba musaada

anazuiza maombi yangu yasimufikie.

9Amezifunga njia zangu kwa mawe makubwa,

amepotosha mapito yangu.

10Alikuwa kwangu kama dubu anayevizia,

kama simba katika maficho.

11Alinifukuza katika njia yangu,

akanirarua na kuniacha ukiwa.

12Aliuvuta upinde wake,

akanielekezea mushale wake.

13Alinichoma ndani ya moyo kwa mishale,

kutoka katika kifuko chake.

14Nimekuwa kitu cha kuchekelewa kwa watu wote,

muchana kutwa nimekuwa mutu wa kuzomewa.

15Amenijaza taabu,

akanishibisha uchungu.

16Amenisagisha meno katika mawe,

akanifanya nigaegae katika majivu.

17Moyo wangu haujui tena amani,

nimesahau furaha.

18Nimewaza: Nimekata tamaa kabisa,

tumaini langu kwa Yawe limetoweka.

19Kukumbuka taabu na kutangatanga kwangu

kunanipa uchungu na sumu.

20Ninafikiri juu ya hayo siku zote,

nayo roho yangu imejaa huzuni.

21Lakini ninakumbuka jambo hili moja,

nami ninakuwa na tumaini:

22Wema wa Yawe haukomi,

huruma zake hazina mwisho.

23Uaminifu wake ni mukubwa sana,

kila mara kunapokucha ni mupya kabisa.

24Yawe ndiye sehemu yangu,

hivyo nitamuwekea tumaini langu.

25Yawe ni muzuri kwa wanaomutegemea,

kwa wote wanaomutafuta.

26Ni vizuri kwa mutu kungojea kwa utulivu

wokovu unaotoka kwa Yawe.

27Ni vizuri kwa mutu kujifunza uvumilivu

tangu wakati wa ujana wake.

28Heri kwa mutu kukaa peke yake na kimya,

mambo mazito yanapomupata kutoka kwa Mungu.

29Inamupasa kuinama na kujinyenyekeza,

labda tumaini litakuwa likingali.

30Inamupasa kumugeuzia shavu mwenye kumupiga,

na kuwa tayari kupokea matusi yake.

31Yawe hatatutupilia milele.

32Ingawa atatufanya tuhuzunike,

atakuwa na huruma tena,

kadiri ya wingi wa wema wake.

33Yeye hapendelei kuwatesa

wala kuwahuzunisha wanadamu.

34Wafungwa wote katika inchi

wanapoteswa na kupondwa,

35haki za wanadamu zinapopotoshwa

mbele ya Mungu Mukubwa,

36wanapomunyima mutu haki katika tribinali,

basi, Yawe haoni hayo?

37Nani anayeweza kusema kusudi kitu kifanyike

ikiwa Yawe asipoamuru ikuwe hivyo?

38Maovu na mema yanatokea tu

kwa amri ya Mungu Mukubwa.

39Kwa nini mutu anungunike

ikiwa ameazibiwa kwa ajili ya zambi zake?

40Tupime na kuchunguza mwenendo wetu

tupate kumurudilia Yawe.

41Tumufungulie Mungu mioyo yetu

na kumwomba kule juu mbinguni:

42Tulikukosea na kukuasi,

nawe haujatusamehe bado.

43Umejifunika hasira yako na kutufuatilia,

ukatuua bila huruma.

44Umejifunika wingu

kusudi maombi yoyote yasipite.

45Umetufanya kuwa takataka na uchafu

kati ya mataifa.

46Waadui zetu wote wanatuzomea.

47Woga na hofu vimetuandama

tumepatwa na uharibifu na maangamizi.

48Macho yangu yanabubujika mito ya machozi

kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu.

49Macho yangu yanatelemusha machozi bila kukoma,

50mpaka Yawe kutoka kule mbinguni

aangalie chini na kuona.

51Ninahuzini sana kuona

yale yaliyowapata wabinti wa muji wangu.

52Nimewindwa kama ndege

na hao wanaonichukia bila sababu.

53Walinitupa ndani ya shimo nikiwa muzima

na juu yangu wakalundika mawe.

54Maji yalianza kunifunika kichwa,

nami nikafikiri: Huu ni mwisho wangu.

55Kutoka chini ndani ya shimo,

nilikulilia ee Yawe.

56Wewe umenisikia nikikulilia:

Usiache kusikiliza maombi yangu ya musaada.

57Nilipokuita ulifika karibu nami

ukaniambia: Usiogope!

58Ulinitetea katika maneno yangu, ee Yawe,

uliyakomboa maisha yangu.

59Uliuona uovu niliotendewa, ee Yawe;

uniamulie kwa wema maneno yangu.

60Umeuona uovu wa waadui zangu,

na mipango yao yote juu yangu.

61Umesikia matukano yao, ee Yawe,

na mipango yao yote juu yangu.

62Maneno na mawazo ya waadui zangu siku nzima,

ni juu ya kuniangamiza mimi.

63Wakiikaa au wakienda,

ni mimi ndiye wanayemuzomea.

64Uwalipize, ee Yawe,

sawasawa na matendo yao,

sawasawa na kazi ya mikono yao.

65Uifanye mioyo yao kuwa migumu,

na laana yako iwashukie.

66Uwafuatilie kwa hasira na kuwaangamiza

toka katika dunia.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help