1Ilipofika mwisho wa miaka miwili mizima, mufalme wa Misri akaota ndoto: alijikuta amesimama kando ya muto Nili,
2akaona ngombe saba wazuri na wanono wakitoka ndani ya muto na kula nyasi.
3Halafu, nyuma ya wale, ngombe wengine saba waliokonda sana wakatoka katika muto Nili, wakakuja na kusimama karibu na wale ngombe wazuri na wanono, kando ya muto.
4Wale ngombe waliokonda sana wakakula wale wengine saba wazuri na wanono. Hapo mufalme akaamuka toka usingizi.
5Alipolala tena, akaota mara ya pili. Aliona masuke saba makubwa na mazuri yanachipuka katika bua moja.
6Halafu, nyuma ya hayo, masuke mengine saba membamba na yaliyokaushwa na upepo mukali wa jangwa yakatokea.
7Yale masuke saba membamba yakameza yale masuke saba makubwa yaliyojaa ngano. Basi, mufalme alipoamuka akatambua kwamba ilikuwa ndoto.
8Kulipokuwa asubui, yeye akiwa na wasiwasi sana, aliwaita wachawi wote wa Misri, na wenye hekima, akawaambia ndoto zake. Lakini hakuna hata mumoja aliyeweza kumutafsiria ndoto zile.
9Halafu, yule mutunza vinywaji mukubwa akamwambia mufalme: “Leo ninakumbuka makosa yangu!
10Wakati ule ulipotukasirikia sisi watumishi wako, mimi na mupishi mukubwa wa mikate, ulitufungia ndani ya nyumba ya mukubwa wa waaskari walinzi.
11Usiku mumoja tuliota ndoto, kila mumoja ndoto yake tofauti.
12Basi, kijana mumoja Mwebrania, mutumishi wa jemadari wa waaskari walinzi, alikuwa pamoja nasi katika kifungo. Tulipomwelezea ndoto zetu, yeye aliweza kutuelezea kila mumoja wetu kulingana na ndoto yake.
13Alivyoeleza ndivyo ilivyotokea: mimi nikarudishwa ndani ya kazi yangu na yule mupishi mukubwa wa mikate akatundikwa juu ya muti.”
14Basi, mufalme akaamuru Yosefu aitwe; naye akaondolewa katika kifungo haraka. Kisha kunyoa na kubadilisha nguo zake, Yosefu akakuja mbele yake.
15Mufalme akamwambia Yosefu: “Mimi nimeota ndoto, lakini hakuna mutu aliyeweza kunitafsiria. Nimesikia sifa zako kwamba wewe ukiambiwa ndoto unaweza kuieleza.”
16Yosefu akamujibu: “Sina uwezo ule; lakini Mungu atakupa jibu linalofaa.”
17Halafu mufalme akamwambia Yosefu: “Niliota kwamba nimesimama kando ya muto Nili,
18nikaona ngombe saba wazuri na wanono wakitoka katika muto na kula nyasi.
19Hao wakafuatwa na ngombe wengine saba zaifu, wembamba na wamekonda sana. Mimi sijapata kuona ngombe wa hali hiyo katika inchi ya Misri.
20Basi, wale ngombe waliokonda sana wakakula wale ngombe saba wanono.
21Lakini hata nyuma ya kuwakula wale wanono, mutu yeyote asingeweza kutambua kwamba wamewakula wenzao, maana walikuwa tu wamekonda sana kama vile mwanzo. Halafu nikaamuka katika usingizi.
22Kisha nikaota ndoto ingine: nikaona masuke saba mazuri yaliyojaa ngano yakichipuka katika bua moja.
23Halafu yakafuatwa na masuke mengine saba matupu, membamba na yaliyokaushwa na upepo mukali wa jangwa.
24Yale masuke saba membamba yakameza yale masuke saba mazuri. Basi, mimi nikawaambia wachawi ndoto hizo lakini hakuna mutu aliyeweza kunifafanulia.”
25Halafu Yosefu akamwambia mufalme: “Ndoto zako zote mbili zina maana moja tu. Mungu amekufunulia mambo atakayofanya sasa hivi.
26Ngombe wale saba wazuri ni miaka saba, na yale masuke saba mazuri vilevile ni miaka saba. Ndoto hiyo tafsiri yake ni moja.
27Wale ngombe saba waliokonda sana, ambao waliwafuata wale wanono, na yale masuke matupu saba, yaliyokaushwa na upepo mukali wa jangwa, maana yake ni miaka saba ya njaa.
28Kama vile nilivyokuelezea, ee mufalme, Mungu amekufunulia mambo atakayofanya sasa hivi.
29Kutakuwa miaka saba ya shibe katika inchi nzima ya Misri.
30Lakini kisha itafuata miaka saba ya njaa, hata hiyo shibe isahaulike kabisa. Njaa hiyo itaangamiza inchi hii.
31Shibe hiyo itasahaulika kabisa kwa sababu njaa itakayofuata itakuwa kali sana.
32Ndoto yako ilirudiliwa mara mbili kwa mifano inayofanana kwa kukuonyesha kwamba Mungu ameamua, naye atatimiza jambo hili sasa hivi.
33“Kwa hiyo inafaa sasa, ee mufalme, uchague mutu mwenye ujuzi na hekima, umupe kazi ya kuangalia inchi yote ya Misri.
34Tena, ee mufalme, uchague wasimamizi wamoja hapa katika inchi, uwaagize wakusanye sehemu ya tano ya mavuno yote ya Misri katika kipindi hiki cha miaka saba ya shibe.
35Uwaagize wasimamizi wale wakusanye chakula chote katika miaka saba inayokuja ya mavuno kwa wingi. Ngano hiyo iwekwe chini ya mamlaka yako, ee mufalme, ikuwe akiba ya chakula kwa miji yote, nao waitunze ngano hiyo.
36Chakula hicho kitakuwa akiba ya kukinga inchi ya Misri isiangamie kutokana na njaa ya miaka saba itakayofuata.”
Yosefu anapewa cheo37Shauri Yosefu alilotoa likaonekana kuwa jema mbele ya mufalme wa Misri na watumishi wake wote.
38Kwa hiyo mufalme akawauliza watumishi wake: “Huyu mutu ana roho wa Mungu! Tunaweza kumupata mutu mwingine kama huyu?”
39Kisha akamwambia Yosefu: “Kwa sababu Mungu amekufunulia haya yote, hakuna mutu mwingine mwenye akili na hekima kama wewe.
40Wewe ndiwe utakayeisimamia inchi yangu, na watu wangu wote watakuwa chini ya amri yako. Mimi tu ndiye mukubwa kuliko wewe kwa kuwa ninaikalia kiti cha kifalme.
41Basi, sasa ninakuchagua kuwa mukubwa wa inchi yote ya Misri!”
42Halafu, mufalme akavua pete yake ya muhuri kwenye kidole chake na kumuvalisha Yosefu. Akamuvalisha na nguo za kitani safi na mukufu wa zahabu kwa shingo.
43Mufalme akamupandisha katika gari lake la pili na walinzi wakatangulia mbele ya Yosefu wakilalamika kwa sauti na kusema: “Mupige magoti!”
Ndivyo mufalme alivyomupa Yosefu madaraka makubwa juu ya inchi yote ya Misri.
44Zaidi ya hayo, mufalme akamwambia Yosefu: “Mimi ni mufalme wa Misri! Ninasema hivi: mutu yeyote katika inchi nzima ya Misri asiinue mukono wala muguu wake bila ruhusu yako.”
45Mufalme akamupa Yosefu jina la Kimisri: Safenati-Panea. Akamupa Asenati, binti ya Potifera, kuhani wa muji wa Oni kuwa muke wake. Basi, Yosefu akaanza kutembelea inchi nzima ya Misri.
46Yosefu alikuwa na umri wa miaka makumi tatu alipoanza kumutumikia mufalme. Alitoka katika nyumba ya mufalme na kuitembelea inchi yote ya Misri.
47Katika miaka ile saba ya shibe, mashamba ya Misri yakatoa mazao kwa wingi sana.
48Yosefu akakusanya chakula chote wakati ule wa miaka saba ya shibe na kukiweka akiba katika miji ya Misri. Katika kila muji akaweka akiba ya chakula kutoka mashamba yanayokuwa karibu na muji ule.
49Yosefu akaweka akiba ya ngano kwa wingi sana ikakuwa nyingi kama muchanga wa bahari, hata isiweze kupimika.
50Mbele ya miaka ya njaa kuanza, Yosefu alikuwa amekwisha kupata wana wawili kwa muke wake Asenati, binti ya Potifera kuhani wa muji wa Oni.
51Yosefu akamwita mwana wake wa kwanza Manase, akisema: “Mungu amenifanya nisahau taabu zangu zote na jamaa ya baba yangu.”
52Mwana wake wa pili akamwita Efuraimu, akisema: “Mungu amenipa watoto katika inchi ya mateso yangu.”
53Miaka ile saba ya shibe katika inchi ya Misri ikapita.
54Ikaanza miaka saba ya njaa kama vile Yosefu alivyokuwa amesema pale mbele. Inchi zingine zote zikakuwa na njaa, lakini inchi yote ya Misri ilikuwa na chakula.
55Wakati wanainchi wa Misri walipoanza kuona njaa, wakamulilia mufalme awape chakula. Naye akawaambia Wamisri wote: “Mwende kwa Yosefu; mufanye neno lolote atakalowaambia.”
56Njaa ikazidi kuwa kali na kuenea katika inchi yote. Kwa hiyo Yosefu akafungua gala zote, akawauzishia Wamisri chakula.
57Zaidi ya hayo, watu toka kila pahali katika dunia walikuja Misri kwa Yosefu kununua ngano, maana njaa ilikuwa kali katika dunia yote.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.