1 Mambo ya Siku 21 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Daudi anahesabu Waisraeli(2 Sam 24.1-25)

1Shetani akaenda kinyume cha Waisraeli, akamushawishi Daudi kuwahesabu watu.

2Halafu, Daudi akamwambia Yoabu na wale majemadari wengine: “Mwende muwahesabu Waisraeli, kutokea Beri-Seba mpaka Dani. Muniletee habari kusudi nijue hesabu yao.”

3Lakini Yoabu akasema: “Yawe aongeze Waisraeli mara mia kuliko jinsi wanavyokuwa sasa! Bwana wangu mufalme, hawa wote si watumishi wako? Kwa nini basi unataka kufanya jambo ambalo litawatia Waisraeli katika kosa?”

4Lakini amri ya mufalme ilikuwa na nguvu zaidi mbele ya Yoabu. Halafu, Yoabu akaenda katika inchi ya Israeli yote, kisha akarudia Yerusalema.

5Yoabu akamupelekea mufalme Daudi hesabu ya watu: katika inchi yote wa Israeli kulikuwa wanaume milioni moja na elfu mia moja, wenye ujuzi wa kutumia mapanga, na katika inchi ya Yuda kulikuwa watu elfu mia ine na makumi saba wenye kutumia mapanga.

6Lakini Yoabu hakuwahesabu Walawi na watu wa kabila la Benjamina, kwa sababu alichukizwa sana na amri ya mufalme.

7Mungu hakupendezwa na jambo lile kwa hiyo akaazibu Waisraeli.

8Daudi akamwambia Mungu: “Nimetenda zambi kubwa kwa tendo hili nililofanya! Lakini ninakuomba unisamehe mimi mutumishi wako, maana nimefanya jambo la kipumbafu kabisa.”

9Basi, Yawe akasema na Gadi, mutabiri wa Daudi, akamwambia:

10“Kwenda kumwambia Daudi hivi: ‘Yawe anasema hivi: Ninakupa mambo matatu, nawe ujichagulie moja kati yao, nami nitakutendea vile.’ ”

11Halafu Gadi akamwendea Daudi na kumwambia: “Yawe anasema hivi: ‘Ujichagulie jambo moja unalotaka kati ya haya:

12njaa ya miaka mitatu; au miezi mitatu ya maangamizi kutokana na waadui zako ambapo upanga wa waadui zako utakushinda; au siku tatu ambazo Yawe atawashambulia kwa upanga wake, awaletee ugonjwa mukali katika inchi, na malaika wake apite kuwaangamiza katika inchi nzima ya Israeli. Sasa amua. Ni jibu gani nitakalomupa yeye aliyenituma.’ ”

13Daudi akamujibu Gadi: “Nimeingia katika mashaka makubwa! Lakini afazali niazibiwe na Yawe maana yeye ana huruma sana. Lakini nisianguke katika mukono wa mwanadamu.”

14Basi, Yawe akawaletea Waisraeli ugonjwa mukali, ambao ulisababisa vifo vya Waisraeli elfu makumi saba.

15Halafu Mungu akatuma malaika aende kuharibu Yerusalema. Lakini mbele hajafanya vile, Yawe akageuza nia yake na kumwambia malaika yule aliyetimiza maangamizi: “Basi, inatosha!” Malaika alikuwa amesimama karibu na uwanja wa kupepetea ngano wa Ornani wa kabila ya Yebusi.

16Daudi akainua macho yake, akamwona yule malaika wa Yawe akisimama kati ya mbingu na dunia, naye akiinua upanga wake juu ya Yerusalema tayari kuangamiza. Halafu Daudi na wazee wote walikuwa wakivaa nguo ya gunia, wakaanguka uso mpaka chini.

17Daudi akamwambia Mungu: “Si mimi ndiye niliyetoa amri watu wahesabiwe? Ni mimi niliyetenda zambi na kufanya uovu. Lakini kondoo hawa wamefanya nini? Ninakusihi sana, ee Yawe, Mungu wangu, mukono wako ukuwe juu yangu na juu ya jamaa ya baba yangu, lakini ugonjwa huu mukali usiwapate watu wako.”

18Halafu malaika wa Yawe akamwamuru Gadi amwambie Daudi aende kumujengea Yawe mazabahu, katika kiwanja cha kupepetea ngano cha Ornani wa kabila ya Yebusi.

19Daudi akatii amri ya Yawe, akapanda juu kufuatana na neno Gadi alilosema kwa jina la Yawe.

20Ornani alipogeuka na kumwona yule malaika, halafu yeye na wana wake wane waliokuwa pamoja naye wakajificha. Naye Ornani alikuwa akipepeta ngano.

21Daudi alipomwendea Ornani akaangalia na kumwona Daudi. Basi Ornani akatoka kwenye uwanja wa kupepetea na kwenda mbele, kisha akainama mbele yake uso mpaka chini.

22Daudi akamwambia Ornani: “Unipe nafasi ya uwanja wako wa kupepetea ngano kusudi nimujengee Yawe mazabahu juu yake, kusudi ugonjwa mukali upate kuzuiliwa katika watu. Uniuzishie kwa bei yake kamili.”

23Naye Ornani akamwambia Daudi: “Utwae kiwanja hiki, bwana wangu mufalme, na ukitumie vile unavyopenda mwenyewe. Angalia, ninawatoa ngombe dume kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa kwa moto, na vifaa vya kupepetea kwa kuni, pamoja na ngano ikuwe sadaka ya unga. Vyote hivyo ninakupa.”

24Lakini mufalme Daudi alimwambia Ornani: “Hapana; nitavinunua kwa bei yake kamili. Sitamutwalia Yawe kitu chako au kumutolea sadaka za kuteketezwa kwa moto ambazo sikununua.”

25Hivyo, Daudi akamulipa Ornani kwa bei ya vikoroti mia sita kamili vya zahabu kwa kulipia uwanja ule.

26Kisha Daudi akamujengea Yawe mazabahu pahali pale na kumutolea sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani. Akamwomba Yawe, naye akakubali maombi yake kwa kuleta moto kutoka mbinguni na kuteketeza sadaka kwenye mazabahu.

27Halafu, Yawe akamwamuru malaika, naye akaweka upanga wake ndani ya mufuko wake.

28Wakati ule, Daudi alipoona kwamba Yawe amekubali maombi yake kwenye uwanja wa kupepetea ngano wa Ornani, Muyebusi, akatoa sadaka palepale.

29Hema la Yawe ambalo lilitengenezwa na Musa katika jangwa, na mazabahu ya sadaka ya kuteketezwa, wakati ule vilikuwa bado pale pahali pa kuabudia kule Gibeoni.

30Lakini Daudi hakuweza kwenda kule kumwomba Mungu shauri kwa sababu alikuwa anaogopa upanga wa malaika wa Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help