Yeremia 26 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yeremia anahukumiwa

1Kwa mwanzo wa utawala wa Yoyakimu mwana wa Yosia, juu ya inchi ya Yuda, Yawe alimwambia Yeremia hivi:

2Yawe anasema hivi: Simama katika kiwanja cha nyumba ya Yawe, uwatangazie watu wa miji yote ya Yuda wanaofika kuabudu katika nyumba ya Mungu, mambo yote niliyokuamuru kuwaambia, bila kuacha hata neno moja.

3Labda watayasikiliza na kila mumoja wao ataacha njia yake mbaya. Wakifanya hivyo, nitabadilisha nia yangu juu ya hasara niliyokusudia kuleta juu yao kwa sababu ya matendo yao maovu.

4Utawaambia kwamba:

Yawe anasema hivi: Kama hamutanisikiliza na kufuata sheria zangu nilizowawekea,

5na kuyajali maneno ya watumishi wangu manabii ambao ninawatuma kwenu kila mara, ingawa hamukuwasikiliza,

6basi, nitaiharibu nyumba hii kama nilivyoharibu ile ya Shilo, na nitaufanya muji huu kuwa mufano kwa mataifa yote ya dunia yatakaoutumia kwa kutoa laana.

7Makuhani, manabii na watu wote wakamusikia Yeremia akisema maneno haya katika nyumba ya Yawe.

8Basi Yeremia alipomaliza kutangaza mambo yote ambayo Yawe aliyomwamuru kutangaza kwa watu wote, makuhani, manabii na watu wote walimukamata na kusema: Wewe unapaswa kuuawa!

9Kwa nini umetabiri kwa jina la Yawe, ukisema kwamba nyumba hii itaharibiwa kama ile ya Shilo na muji huu utakuwa ukiwa, bila wakaaji? Na watu wote wakamuzunguka Yeremia katika nyumba ya Yawe.

10Basi, wakubwa wa Yuda waliposikia mambo hayo, wakapanda kutoka kwa nyumba ya mufalme, wakaenda kwenye nyumba ya Yawe, wakaikaa kwenye mulango ulioitwa: “Mulango Mupya”.

11Kisha makuhani na manabii wakawaambia wakubwa na watu wote: Mutu huyu anastahili hukumu ya kifo, kwa maana ametabiri juu ya muji huu, kama vile ninyi wenyewe mulivyosikia kwa masikio yenu.

12Halafu Yeremia akawaambia wakubwa na watu wote: Yawe alinituma niwatabirie mambo yote muliyosikia nikisema juu ya hekalu hili na muji huu.

13Sasa basi, mugeuze mienendo yenu na matendo yenu na kutii sauti ya Yawe, Mungu wenu. Mukifanya hivyo, Yawe atabadilisha nia yake na kuacha kuwaletea hasara aliyokusudia kuleta juu yenu.

14Lakini mimi niko sasa katika mikono yenu. Munitendee kama vile munavyoona vema na haki.

15Lakini mujue kwa hakika kwamba mukiniua, mutakuwa mumejiletea laana ninyi wenyewe kwa kumwanga damu isiyokuwa na kosa, na kuleta laana juu ya muji huu na wakaaji wake. Maana, ni kweli kwamba Yawe alinituma niwaambie mambo hayo kusudi muyasikie.

16Basi wakubwa na watu wote wakawaambia makuhani na manabii: Mutu huyu hastahili hukumu ya kifo. Amesema nasi kwa jina la Yawe, Mungu wetu.

17Basi, wasimamizi wamoja wa inchi wakasimama na kuwaambia watu waliokuwa wamekusanyika:

18Katika siku Hezekia alipokuwa mufalme wa Yuda, Mika wa Moreseti aliwatangazia watu wote kwamba Yawe wa majeshi alisema hivi:

Sayuni utalimiwa kama shamba,

Yerusalema utabaki mabomoko,

nao mulima wa hekalu utakuwa pori.

19Hezekia, mufalme wa Yuda, na watu wote wa Yuda hawakumwua Mika. Hezekia alimwogopa Yawe na kuomba rehema kwake. Naye Yawe akabadilisha nia yake ya kuleta hasara aliyokusudia juu yao. Lakini sisi tuko mbio kwa kujiletea hasara wenyewe.

20Kulikuwa mutu mwingine vilevile aliyetabiri kwa jina la Yawe. Mutu huyu aliitwa Uria mwana wa Semaya, wa muji wa Kiriyati-Yearimu. Yeye alitabiri juu ya muji huu na juu ya inchi hii sawasawa na maneno yale Yeremia aliyotabiri.

21Naye mufalme Yoyakimu pamoja na waaskari shujaa wake na wakubwa wote wa serikali yake waliposikia mambo yale Uria aliyosema, mufalme alitaka kumwua. Lakini Uria alipopata habari ile, alishikwa na hofu, akatoroka na kwenda Misri.

22Mufalme Yoyakimu akamutuma Elnatani mwana wa Akibori, pamoja na watu wengine kwenda Misri.

23Wao wakamurudisha Uria kutoka Misri, wakamupeleka kwa mufalme Yoyakimu. Mufalme akamwua kwa upanga na maiti yake ikatupwa katika kaburi.

24Lakini Yeremia alikuwa akilindwa na Ahikamu mwana wa Safamu kusudi asitiwe katika mikono ya watu na kuuawa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help